LATEST POSTS

Tuesday, October 15, 2013

MKASA WA TUKIO LA UFOO SARO KUPIGWA RISASI NA MAMA YAKE KUUAWA HUU HAPA

Mwandishi wa Kituo cha Televisheni cha ITV, Ufoo Saro amejeruhiwa vibaya baada ya kupigwa risasi mbili jana alfajiri huko Kibamba, Dar es Salaam.

Katika tukio hilo linalodaiwa kufanywa na mzazi mwenzake, Anthery Mushi ambaye alijiua baadaye, pia anadaiwa kumuua mama yake Ufoo, Anastazia Saro.
Ufoo alipigwa risasi moja tumboni na kutokea kwenye mbavu na nyingine ilipita kifuani hadi kwenye ziwa lake la kulia na kutokea kwenye mkono wa kulia.

Baada ya tukio hilo, Ufoo alipelekwa katika Hospitali ya Tumbi, Kibaha kabla ya kuhamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambako alifanyiwa upasuaji.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova alithibitisha kutokea kwa tukio hilo lililosababisha vifo hivyo na kumjeruhi mwandishi huyo.

Kova alimtaja Mushi, ambaye alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Saro akidai kuhusika na tukio hilo.
“Mushi alimpiga risasi za kifuani mama yake Ufoo, ambaye alifariki palepale. Pia alimpiga risasi mwandishi huyo na baadaye alijiua kwa kujipiga risasi chini ya kidevu, risasi ambayo ilifumua kwa kiasi kikubwa eneo la juu la kichwa chake.”
Kova aliwaambia waandishi wa habari waliokuwa katika Hospitali ya Muhimbili kuwa, vifo hivyo vimetokana na wivu wa mapenzi.
Mashuhuda wa tukio
Akizungumzia tukio hilo, mdogo wa mwandishi huyo, Goodluck Saro alisema dada yake Ufoo na shemeji yake Mushi walikwenda nyumbani kwa mama yao huko Kibamba saa 12.00 asubuhi na kwamba baada ya kufika huko walikuwa na mazungumzo na mama yao ambayo hata hivyo, hakuyafuatilia kwa kuwa alikuwa amelala.

Goodluck alisema, muda mfupi baadaye alisikia sauti ya mama yake, ikimwita; “Goodluck nakufa... Goodluck nakufa.”
Alisema alitoka chumbani na kwenda sebuleni ambako alimkuta Ufoo akiwa ameanguka chini huku akichuruzika damu.

“Ufoo aliponiona aliniagiza nirudi chumbani mara moja. Niliporudi chumbani, Mushi akaanza kupiga risasi ovyo,” alidai Goodluck.
Goodluck alisema alikuwa chumbani na ndugu zake Jonas Saro na Abel Innocent, ambao walilazimika kupanda darini ili kuokoa maisha yao.

Alidai kuwa baada ya Mushi kuona amewakosa ndugu zake Ufoo alikusanya nguo zote na kuziweka karibu na mtungi wa gesi, ambao aliupiga risasi na kusababisha kuwaka moto.
“Tukiwa darini tulizidiwa na moshi tukalazimika kupasua paa na kuruka nje ya nyumba,” alisema Goodluck.
Baada ya kutoka nje alisema walipiga simu polisi na ilipotimu takriban saa tatu asubuhi polisi mmoja alifika lakini baadaye waliongezeka na hivyo kupata ujasiri wa kuingia ndani ya nyumba.

Mtuhumiwa akutwa na tindikali, kamba na shoka
Goodluck alidai kwamba walimkuta shemeji yao akiwa amejiua huku akiwa ameketi kwenye kiti na kichwa chake kikiwa kimefumuka jambo ambalo alisema wanaamini kuwa alijipiga risasi.

Goodluck alisema baada ya ukaguzi, askari walimkuta akiwa na kitu kinachoaminika kuwa ni tindikali, shoka, mifuko ya plastiki, kompyuta  ndogo, kamba, pingu na risasi nane.
“Tunahisi alikuwa na risasi kama 17 hivi kwani alitumia tisa hivi wakati wa tukio hilo na zikabaki nane,” alisema Goodluck.
Baadhi ya majirani walisema walisikia milio ya risasi na wakati wakiulizana kulikoni, alitokea mtoto anayeishi kwenye nyumba ya marehemu na kuwaomba msaada akisema kulikuwa na ugomvi.

“Tulipokwenda tulichungulia na kuona damu zimetapakaa chumba kizima, pembeni tuliuona mwili wa mama yake Ufoo Saro ukiwa umelala chini. Nyumba ilikuwa imejaa moshi mzito, tulipiga simu polisi kutoa taarifa,” alisema mmoja wa majirani, Bobroy Ngowi.
Licha ya kuwa katika maumivu makali, hadi polisi wanafika, Ufoo alikuwa ameshatoka katika eneo la tukio mwenyewe. Ufoo aelezea mkasa mzima

Akizungumza kwa taabu wakati akiwa kwenye gari la wagonjwa kutoka Tumbi kuelekea Muhimbili, Ufoo alisema alijivuta kutoka nje na kutembea mwenyewe hadi barabarani.
Alisema baada ya madereva wa Boda Boda kumwona anavuja damu nyingi, walimpakia na kumpeleka Tumbi.

Hata hivyo, alipofika Tumbi, anasema hakuchukuliwa vipimo kutokana na kutokuwepo kwa mtaalamu wa x-ray ndipo ilipoamuliwa kuwa apelekwe Muhimbili.
Akiwa amefuatana na Mwandishi Wetu, Julieth Ngarabali Ufoo licha ya kuwa na maumivu makali, alisimulia kilichomsibu.
Ilikuwa baada ya kufika Kibaha mizani Ufoo alipomwita mwandishi wetu: “Julieth naomba uiname nikusimulie kitu... Unajua aliyefanya haya ni Baba Alvin (Mushi). Amempiga risasi mama na mimi mwenyewe.”
Baada ya kusema hivyo, alinyamaza na kuanza kububujikwa na machozi.

Baada ya kufika Kibamba alipata nguvu na kusimulia kuwa mama yake alikuwa amefariki katika tukio hilo... Huku akilia, alisema kuwa alipewa taarifa hizo na polisi.
“Masikini mtoto wangu Alvin sijui itakuwaje, baba yake amejiua, amemuua mama yangu na babu yake alishafariki... sijui atabakia na nani, maana sijui kama nitapona,” alisema huku akilia.
Ufoo ambaye alitoka katika chumba cha upasuaji saa 12 jioni, alisema atakapopata nafuu ataweka hadharani mkasa mzima uliosababisha mauti na majeraha hayo.
Mushi ni nani?

Mushi alikuwa mfanyakazi kitengo cha mawasiliano cha Umoja wa Mataifa huko Darfur, Sudan na alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Ufoo kwa zaidi ya miaka 10.
Pia aliwahi kufanya kazi ITV na Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), akiwa mpigapicha wa televisheni.

Baada ya kuondoka kwenye fani ya habari alijiunga na Mahakama ya Kimataifa inayoshughulikia kesi za Rwanda (ICTR), kabla ya kwenda Sudan.
Ofisa wa Kitengo cha Habari cha Umoja wa Mataifa huko Darfur, Said Msonda alisema kuwa Mushi alikuwa amehamishwa kutoka kituo cha El-Jenina na kupelekwa kile cha Al-Fasha.
“Tulikuwa tumepanga kumwandalia tafrija ya kumuaga baada ya kurudi kutoka Tanzania na haya ndiyo yametokea,” alisema.
Kaka mkubwa wa marehemu, Silva Mushi alisema mdogo wake alikuwa Moshi kabla ya kuja Dar es Salaam.
“Nilikuwa sijawasiliana naye siku nyingi na nilikuwa sijawahi kusikia kama alikuwa na matatizo yoyote na Ufoo,” alisema.
Msemaji wa familia ya kina Saro, Iddi Lema alisema kuwa mazishi ya mama yake Ufoo yamepangwa kufanyika Ijumaa katika Kijiji cha Mashari, Machame mkoani Kilimanjaro.

Lema alisema msafara wa kuelekea huko utaondoka Dar es Salaam Alhamisi na kwamba ndugu, jamaa na marafiki watakutana kesho saa 10.00 kwenye Ukumbi wa Urafiki kwa ajili ya kufanikisha taratibu hizo.
Imeandikwa na Julieth Ngarabali, Aidan Mhando, Fidelis Butahe, Pamela Chilongola na Sanjito Msafiri

Monday, October 14, 2013

UFOO SARO AFANYIWA UPASUAJI WA KUONDOLEWA RISASI MWILINI.

 

Ufoo Saro baada ya kufanyiwa upasuaji huo.
Muuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), akimpeleka wodini Mtangazaji wa Kituo cha Televisheni cha ITV, Ufo Saro, baada ya kufanyiwa upasuaji wa kuondolewa risasi kufuatia kushambuliwa kwa silaha ya moto nyumbani kwa mama yake Kibamba jijini Dar es Salaam leo na mtu aliyedaiwa ni mchumba wake ambaye pia alimuua mama yake na kisha kujiua.
Wanahabari wakimpiga picha Ufoo Saro baada ya kuondolewa chumba cha upasuaji.
Wanahabari kutoka vyombo mbalimbali wakimsindikiza Ufoo Saro

Sunday, October 13, 2013

MWANDISHI WA HABARI WA ITV&RADIO ONE UFOO SARO AJERUHIWA KWA RISASI NA MCHUMBA WAKE NA MAMA YAKE MZAZI AUAWA PAPO HAPO..


Mwandishi wa Habari wa ITV na Radio One Ufoo Saro amejeruhiwa kwa risasi na mtu mmoja anaedaiwa kuwa mchumba wake ambaye inasemekana anafanya kazi UN. Katika tukio hilo ambalo limetokea katika maeneo ya Kibamba jijini Dar-es-saalam.
Kamanda wa polisi wa Mkoa wa kipolisi wa Kinondoni Kamanda Wambura amesema kuwa tukio hilo limetokea majira ya Alfajiri leo.
 
Kamanda wambura ameongeza kuwa mwanaume aliyefanya tukio hilo anafanya kazi Umoja wa Mataifa (UN) huko Sudani ila bado haijafahamika kwamba anafanyia kitengo gani (japo kwa habari za mtaani zinasema mtu huyo ni mwanajeshi ila bado hazijathibitishwa)
 
Kamanda Wambura alisema kuwa, inasemekana kulikua kuna ugomvi kati ya wawili hao ambapo walishindwa kuelewana na ndipo walipoamua kwenda kwa mama mzazi wa Ufoo Saro (mama mkwe) na ndipo mwanaume huyo alipomshutumu mama mkwe wake kwamba anamtetea mwanae ndipo alipotoa bastola na kumpiga mama yake na Ufoo Saro Risasi ya kichwa na kumuua papo hapo na kisha akampiga Ufoo Saro risasi mbili moja ya tumboni na ingine ya mguuni na kudhani kwamba amemuua kumbe amemjeruhi tu kisha kujipiga mwenyewe risasi ya kidevuni na kufariki dunia hapo hapo.
Kwa sasa Ufoo yupo katika hospitali ya Muhimbili chumba cha wagonjwa mahututi.
Urambonews inatoa pole kwa familia ya Bi.Ufoo Saro na tunamwomba Mwenyezi Mungu ampe afueni/ahueni. Na mama Ufoo Saro apumzike kwa amani.

Saturday, October 5, 2013

HOTUBA YA MHE.RAIS JAKAYA KIKWETE KWA WANANCHI OKTOBA 4,2013

Rais Jakaya Kikwete akitoa hotuba.
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WANANCHI, TAREHE 4 OKTOBA, 2013

Ndugu Wananchi;
Namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kumaliza mwezi Septemba salama na kuwasiliana kwa kutumia utaratibu wetu huu mzuri.  Naomba radhi kuzungumza nanyi siku ya leo kwa sababu nilikuwa safari na nilirejea jioni ya tarehe 30 Septemba, 2013.   Awali nilifikiria nisiseme, nisubiri mwisho wa mwezi wa Oktoba.  Lakini, baada ya kupata taarifa ya yaliyojiri, nimeshauriwa na nimekubali angalau niyasemee baadhi ya mambo huenda itasaidia.  Niwieni radhi nisipoyasemea baadhi ya mambo siyo kwa kuyapuuza, bali kwa kuepuka hotuba kuwa ndefu mno.  Nitayatafutia mahali pengine pa kuyasemea.
Uhusiano na Rwanda
Ndugu Wananchi;
Katika hotuba yangu ya mwisho wa mwezi wa Julai, nilizungumzia hali ya uhusiano wetu na Rwanda kutokuwa mzuri na tatizo la ujambazi na wahamiaji haramu katika Mikoa ya Kigoma, Geita na Kagera.  Nafurahi kusema kuwa kwa yote mawili kuna maendeleo ya kutia moyo.
Tarehe 5 Septemba, 2013, nilikutana na kuzungumza na Mheshimiwa Rais Paul Kagame wa Rwanda mjini Kampala.  Tuliitumia fursa ya ushiriki wetu katika Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu kuzungumzia uhusiano baina yetu na nchi zetu.  Mazungumzo yalikuwa mazuri na sote tulikubaliana kuwa yaliyopita si ndwele tugange yajayo.  Kwa sababu hiyo tulielewana kuwa tutengeneze mazingira yatakayosaidia kutuliza hali na kurudisha nchi zetu katika uhusiano mwema kama ilivyokuwa siku zote.  Nawaomba ndugu zangu hususan wanasiasa, watumishi wa umma, wanahabari na wenye mitandao ya kijamii na blog na wananchi kwa ujumla tusaidie kuimarisha uhusiano mwema baina ya Rwanda na Tanzania na watu wake.
Majambazi na Wahamiaji Haramu
Ndugu Wananchi;
Katika hotuba hiyo pia nilisema kuwa tutachukua hatua thabiti dhidi ya majambazi na wageni wanaoishi nchini bila ya kuzingatia taratibu zinazohusika.  Niliwataka majambazi wajisalimishe wao na silaha zao kwa hiari.  Wale wanaoishi nchini bila ya kuwa na kibali halali wahalalishe ukaazi wao au warejee makwao.  Nilitoa siku 14 kuanzia tarehe 29 Agosti, 2013 wafanye hivyo kwani baada ya hapo tungeanzisha operesheni maalum ya kushughulika na watu wa makundi yote mawili.
Ndugu Wananchi;
Kumekuwepo na mafanikio ya kutia moyo.  Kwa upande wa wahamiaji wanaoishi nchini kinyume cha sheria watu wapatao 21,254 waliondoka kwa hiari.  Hali kadhalika zaidi ya ng’ombe 8,000 waliondolewa na silaha 102 zilisalimishwa.   Baada ya operesheni kuanza tarehe 6 Septemba, 2013 na kumalizika tarehe 20 Septemba, 2013, wahamiaji haramu 12,828 walirejeshwa makwao na watuhumiwa 279 wa unyang’anyi wa kutumia silaha walikamatwa.  Aidha, mabomu 10 ya kutupa kwa mkono (offensive hand grenades), silaha 80, risasi 780 na mitambo 2 ya kutengeneza magobole vilikamatwa.  Pia, ng’ombe 8,226 walikamatwa wakichungwa katika mapori ya hifadhi.  Kwa upande wa mazao ya misitu, mbao 2,105 zilikamatwa pamoja na nyara mbalimbali za Serikali.
Ndugu Wananchi;
Agizo la kuwataka watu wanaoishi nchini isivyo halali wahalalishe ukaazi wao au waondoke kwa hiari au wataondolewa lilipotoshwa hasa na vyombo vya habari vya nje ya Tanzania.  Walikuwa wanadai eti Tanzania ilikuwa inafukuza wakimbizi.  Madai hayo si ya kweli hata kidogo.   Hadi kufikia tarehe 30 Septemba, 2013 wakimbizi 68,711 walikuwepo kwenye Kambi ya Nyarugusu, Mkoani Kigoma.  Hakuna mkimbizi ye yote aliyetakiwa kuondoka.  Ukweli ni kwamba hakuna mtu ye yote kati ya wale watu walioondoka kwa hiari au kusaidiwa kuondoka wakati wa operesheni ambaye ni mkimbizi.  Kama ingekuwa hivyo, wa kwanza kulalamika wangekuwa wenzetu wa Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa.  Bahati nzuri jambo hilo halikutokea.
Ndugu Wananchi;
Yalikuwepo pia madai kwamba tunawaonea na kuwatesa watu walioishi nchini miaka mingi.  Ati iweje sasa ndiyo waambiwe kuwa siyo raia.  Siku zote Serikali ilikuwa wapi? Uraia haupatikani kwa kuishi nchi ya kigeni kwa miaka mingi.  Unapatikana kwa kutimiza masharti ya kuomba na kupewa uraia.  Kama mtu hakufanya hivyo anabaki kuwa raia wa nchi aliyotoka au walikotoka wazazi wake.  Ipo mifano ya watu mashuhuri ambao walilazimika kuachia nyadhifa zao baada ya kugundulika kuwa siyo raia.  Hawakuwa wanaonewa, ndiyo matakwa ya Katiba na Sheria za nchi yetu.
Ndugu Wananchi;
Katika kutekeleza operesheni hii niliagiza kuwa wale watu ambao wameishi hapa nchini miaka mingi ambao wana nyumba, mashamba au mali mbalimbali au wameoa au kuolewa na wana watoto au hata wajukuu waelekezwe kuhalalisha ukaazi wao.  Iwapo watakataa kufanya hivyo basi wasaidiwe kurejea kwao.  Pia niliagiza watu wasiporwe mali zao wala kudhulumiwa.  Sijapata taarifa ya kufanyika kinyume na maelekezo yangu.  Lakini kama wapo watu waliotendewa tofauti, taarifa itolewe kwa Wakuu wa Wilaya na Mikoa au hata Ofisi ya Rais ili hatua zipasazo zichukuliwe.  Hatutaki watu wadhulumiwe au kuonewa.
Napenda kutumia nafasi hii kumpongeza Waziri wa Ulinzi na JKT, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa Emmanuel Nchimbi kwa uongozi wao mzuri katika zoezi hili.  Pia, nawapongeza Makamanda na askari wa JWTZ na Polisi pamoja na maafisa wa Idara ya Uhamiaji, Idara ya Mifugo, Idara ya Wanyamapori, Idara ya Misitu na Idara nyinginezo za Serikali kwa kazi kubwa na nzuri waliyofanya.  Najua awamu ya kwanza imeisha tarehe 20 Septemba, 2013 na kama nilivyosema kuwa safari hii operesheni itakuwa endelevu, muda si mrefu awamu ya pili itafuata.  Nawaomba waendelee kuchapa kazi kwa bidii, maarifa na nidhamu ya hali ya juu.
Ziara ya Canada na Marekani
Ndugu Wananchi;
Kati ya tarehe 17 na 28 Septemba, 2013 nilifanya ziara ya kikazi katika nchi za Canada na Marekani.  Nchini Canada nilitembelea Chuo Kikuu cha Guelph ambapo nilitunukiwa Shahada ya Heshima ya Uzamivu kwa kutambua jitihada zetu tuzifanyazo kujiletea maendeleo na mafanikio ya kutia moyo tunayoendelea kupata licha ya changamoto zinazotukabili.  Katika mazungumzo yangu na uongozi wa chuo hicho wamekubali kuwa na ushirikiano wa karibu na Wizara zinazohusika na Elimu, Kilimo na Mifugo pamoja na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine,  Morogoro na Chuo Kikuu cha Dodoma.  Nimewataka Mawaziri wa Wizara hizo na viongozi wa vyuo hivyo kuchangamkia fursa hiyo bila kuchelewa.
Ndugu Wananchi;
Nchini Marekani nilikutana na kuzungumza na maafisa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya nchi hiyo wakiwemo Rais Barack Obama na baadhi ya Wabunge wa Bunge la Marekani.  Mazungumzo yetu yalilenga kuimarisha ushirikiano baina ya nchi zetu na mambo yalienda vizuri.  Wote walituhakikishia kuwa mambo tuliyoyazungumza na kukubaliana na Rais Barack Obama wakati wa ziara yake nchini yanaendelea kufanyiwa kazi.  Miongoni mwa hayo maombi yetu ya kupatiwa vitabu milioni 2.4 vya sayansi na hisabati yamekubaliwa na utekelezaji umeanza.  Upatikanaji wa vitabu hivyo utamwezesha kila mwanafunzi wa sekondari kuwa na kitabu chake.
Ndugu Wananchi;
Jambo lingine kubwa na la faraja kwetu ni kuwa mapendekezo yetu ya miradi ya umeme na barabara za vijijini za kugharamiwa na Serikali ya Marekani kupitia Shirika lao la Changamoto za Milenia yamepokelewa vizuri.  Kinachosubiriwa ni miradi ipi itakubaliwa na Bodi ya MCC na kiasi gani cha fedha kitatengwa na Bunge la Marekani kwa ajili hiyo.
Tuzo ya Uhifadhi
Jambo lingine muhimu katika safari yangu ya Marekani ni kutunukiwa tuzo na “International Congressional Conservation Foundation” kwa kutambua juhudi zetu katika kuhifadhi wanyama pori na mafanikio tuliyoyapata.  Licha ya changamoto mbalimbali tunazokabiliana nazo, tuzo hii imetupa moyo wa kuongeza nguvu katika jitihada tunazozifanya sasa kupambana na ujangili na matatizo mengine ya uhifadhi wa wanyama na misitu.
Ndugu Wananchi;
Kilichotupa moyo zaidi ni kauli za utayari wa kutusaidia katika mapambano hayo zilizotolewa wakati wa kupewa tuzo na katika mkutano wa mfuko wa Maendeleo wa Clinton na katika mkutano maalum wa kupambana na ujangili na biashara ya meno ya tembo duniani.
Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa
Ndugu Wananchi;
Shabaha kuu ya safari yangu ya Marekani ilikuwa kuhudhuria Mkutano wa 68 wa Umoja wa Mataifa unaoendelea jijini New York mpaka Desemba, 2013.  Mada kuu ya mkutano wa mwaka huu ni kuandaa agenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015 yaani: Post 2015 Development Agenda:  Setting the Stage. Kama mtakavyokumbuka Malengo ya Milenia yaliyoamuliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2000, yanafikia ukomo wa utekelezaji wake mwaka 2015.
Katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka huu mjadala umehusu nini kifanyike baada ya mwaka 2015.  Hata hivyo, mjadala huo unaanza kwa kufanya tathmini ya utekelezaji wa yale Malengo Manane ya Milenia ya mwaka 2000 umefikia wapi mpaka sasa na utafikia wapi mwaka 2015 kwa kila nchi na kwa dunia kwa ujumla.  Tathmini ya jumla inaonesha kuwa kumekuwepo na jitihada kubwa ya kutekeleza malengo haya katika kila nchi.  Yapo malengo ambayo utekelezaji wake umefikia shabaha hivi sasa na yapo ambayo upo uwezekano wa shabaha kufikiwa ifikapo mwaka 2015.  Vile vile yapo ambayo shabaha haitafikiwa.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wetu, Tanzania, tumefikia shabaha katika mambo yafuatayo:
  1.  Lengo la Milenia namba 2 kuhusu uandikishaji wa watoto wenye umri wa kwenda shule ya msingi;
  2. Lengo la Milenia namba 3 hasa kuhusu usawa wa kijinsia katika Shule za Msingi na Sekondari.  Ukweli ni kwamba, wasichana wanaanza kuwa wengi kuliko wavulana.  Hatujafikia shabaha kwa upande wa usawa wa kijinsia katika elimu ya juu na ni vigumu kulifikia ifikapo 2015.  Pia hatujafikia lengo kwa upande wa usawa wa Wabunge wanawake na wanaume.  Hata hivyo, kwa kutumia mchakato wa Katiba unaoendelea sasa tunaweza kufikia lengo katika uchaguzi wa 2015 iwapo tutaamua iwe hivyo;
  3. Lengo la Milenia namba 4 kuhusu kupunguza idadi ya vifo vya watoto wachanga na wale wenye umri chini ya miaka mitano;
  4. Tumefikia shabaha kwa Lengo la Milenia Namba 6 kuhusu  kupunguza maambukizi ya UKIMWI; na
  5. Kwa upande wa lengo namba 7 kuhusu mazingira, tumefikia shabaha kwa upande wa upatikanaji wa maji mijini.  Bado tuko nyuma kwa maji vijijini ingawaje tunaweza kufikia lengo ifikapo mwaka 2015 kama tutaendeleza uwekezaji tulioamua kufanya katika bajeti ya mwaka huu.  Lakini, hatutaweza kufikia shabaha kwa upande wa usafi wa mazingira mijini na vijijini ifikapo mwaka 2015.  Safari bado ndefu sana.

Ndugu Wananchi;
Malengo ya Milenia namba 1 na namba 5 ambayo bado tuko nyuma sana ya shabaha hatutafikia lengo ifikapo 2015.  Tumeendelea kutekeleza lengo la Milenia namba 1 kuhusu kupunguza umaskini na njaa kwa zaidi ya nusu kutoka kiwango cha mwaka 2000.  Hatua tunazochukua kuleta mageuzi katika kilimo zina lengo la kuhakikisha usalama wa chakula na kuongeza mapato ya wakulima.  Mafanikio yanaanza kuonekana lakini si ya kiwango cha kutufikisha kwenye lengo ifikapo mwaka 2015.  Tunao, pia, mpango wa kupanua programu ya TASAF ya Conditional Cash Transfer ili tuwafikie watu wengi maskini.   Hata kama tutafanikiwa kuutekeleza mapema mpango huu utatusogeza sana mbele lakini bado tutakuwa chini ya lengo kwa upande wa kupunguza umaskini ifikapo 2015.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa Lengo  la Milenia namba 5, kuhusu afya ya kina mama wajawazito bado tuko nyuma katika kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na kuongeza idadi ya wajawazito wanaojifungua chini ya uangalizi wa wataalamu wa afya.  Hatutaweza kufikia shabaha ifikapo mwaka 2015.  Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi (2007 – 2017) una nia ya kukabiliana na matatizo haya.  Tumeongeza ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na hospitali, tumeboresha upatikanaji wa dawa na tumepanua sana mafunzo ya madaktari, wauguzi na wakunga mambo ambayo yamesaidia kutufikisha hatua tuliyopiga mpaka sasa. Naamini juhudi zetu tukiziendeleza zitatusogeza mbele zaidi ingawaje bado tutakuwa chini ya lengo.  Miaka michache ijayo, tatizo hili nalo litakuwa historia.
Ndugu Wananchi;
Lengo la Milenia namba 8 linazihusu nchi tajiri kuongeza michango yao kusaidia nchi zinazoendelea kutekeleza Malengo ya Milenia.  Bahati mbaya sana mataifa tajiri hayajafikia viwango wanavyotarajiwa kutoa na hata vile wanavyoahidi wenyewe kutoa katika majukwaa mbalimbali.  Kama wangetimiza ahadi zao, sura ya utekelezaji wa Malengo ya Milenia ingekuwa tofauti kabisa.
Ndugu Wananchi;
Hiyo ndiyo hali ya utekelezaji wa Malengo ya Milenia hapa nchini. Hakuna nchi ye yote duniani iliyofanikiwa kutekeleza shabaha za malengo yote kwa ukamilifu.  Ushauri wa viongozi wote waliozungumza ulitaka mataifa yaliyoendelea yatimize ahadi zao za kuchangia utekelezaji wa Malengo ya Milenia.  Ilionekana suala la upatikanaji wa fedha halina budi kuangaliwa kwa makini sasa na baada ya mwaka 2015.  Bila ya hivyo ufanisi utakuwa mdogo katika kuongeza kasi ya utekelezaji kwa pale paliposalia kufikia malengo ya 2015 na hata kwa Malengo ya baada ya mwaka 2015.
Mashambulizi ya Kigaidi ya Westgate, Nairobi
Ndugu Wananchi;    
Wakati nikiwa safarini, tarehe 21 Septemba, 2013  kulitokea shambulilizi la kigaidi katika Jengo la Biashara la Westgate, huko Nairobi, Kenya.  Watu 67 walipoteza maisha na zaidi ya 200 walijeruhiwa.  Nilituma salamu za pole na rambirambi kwa Mheshimiwa Rais Uhuru Kenyatta na wananchi wa Kenya na kuwahakikishia kuwa tupo pamoja nao katika wakati huu wa majonzi.
Nafahamu kuwa baada ya tukio hilo watu wengi hapa nchini wameingiwa na hofu kuhusu usalama wetu.  Ni hofu ya msingi kwani tarehe 8 Agosti, 1998 Ubalozi wa Marekani hapa nchini ulishambuliwa na magaidi na ndugu zetu 11 wasio na hatia walipoteza maisha.
Ndugu Wananchi;
Napenda kuwafahamisha kuwa tangu shambulio la mwaka 1998, Serikali imekuwa inajenga uwezo wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kupambana na ugaidi katika nyanja mbalimbali.  Tunaendelea kujiimarisha bila kusita siku hadi siku.  JWTZ, Polisi na Idara ya Usalama wa Taifa wamekuwa na ushirikiano wa karibu kwa ajili hiyo.  Juhudi zetu hizo ndizo zinazotufanya tuwe salama hadi sasa.
Baada ya tukio la Kenya, vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimeimarisha mikakati yao maradufu.  Pamoja na kujizatiti kwetu huko hatuwezi kusema kuwa tukio la kigaidi halitaweza kutokea nchini.  Uhakika huo hatuna kwani hata mataifa makubwa na tajiri yameshambuliwa.  Kilicho muhimu ni kuendelea kuchukua tahadhari na wananchi kusaidia ili  vyombo vyetu vifanikiwe zaidi. 
Hali kadhalika, tumewataka watu wote wenye shughuli zinazokusanya watu wengi kama vile maduka, maofisi, mahoteli, migahawa n.k. waweke kamera za ulinzi nje na ndani ya maeneo yao.  Pia waangalie uwezekano wa kuweka vifaa vya upekuzi (metal detectors and x-rays).  Najua watu wanaweza kulalamikia usumbufu au gharama, lakini gharama na hasara ya kushambuliwa ni kubwa zaidi kuliko ya usumbufu huo.
Ndugu Wananchi;
Nawaomba muendelee kufanya shughuli zenu bila ya hofu ingawaje msiache kuwa makini na kuchukua tahadhari.  Watu watoe taarifa kwa vyombo vya usalama wanapoona mtu au watu au kitu cha kutilia shaka.  Ni muhimu kwa usalama wake, wa kila mtu, jamii na taifa.  Maafisa husika wa vyombo vya ulinzi na usalama wataendelea kuelimisha umma kuhusu hatua mbalimbali za tahadhari za kuchukua.  Sisi Serikalini tumejipanga kuchukua hatua zaidi kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi yetu na watu wake.
Mchakato wa Katiba Mpya
Ndugu Wananchi;
Kama mtakavyokumbuka, Bunge lilitunga Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Novemba, 2011.  Sheria hii imeweka mchakato mzima wa kupata Katiba hiyo na kuunda taasisi zake.  Mwezi Mei, 2012, Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliundwa na imekamilisha hatua tatu muhimu katika mchakato huo.  Hatua hizo ni kupokea maoni ya wananchi, kutayarisha rasimu ya kwanza ya Katiba Mpya na kupokea maoni ya Mabaraza ya Katiba ya Wilaya na ya taasisi.  Hivi sasa Tume inaandaa mapendekezo ya Rasimu ya Pili ya Katiba itakayopelekwa kwenye Bunge Maalum.  Baada ya tafakuri zake, Bunge Maalum litatoa rasimu ya mwisho ya Katiba ambayo itapelekwa kwa wananchi kwa ajili ya uamuzi wa mwisho kupitia kura ya maoni.  Baada ya hatua hiyo, ndipo tutakapokuwa tumepata Katiba Mpya.
Ndugu Wananchi;
Baada ya Bunge la Novemba, 2011 kupitisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, kulikuwepo na madai ya kutaka sheria hiyo iboreshwe kutoka vyama vyote vya siasa vikiwemo vyama vya upinzani na Chama tawala.  Majadiliano yalifanyika baina ya Serikali na vyama hivyo pamoja na shirikisho la asasi za kiraia.  Makubaliano yalifikiwa kuwa marekebisho yafanyike kwa awamu.  Awamu ya kwanza ihusishe Tume ya Mabadiliko ya Katiba kisha hapo yafanyike marekebisho yanayohusu Bunge Maalum na mwisho Kura ya Maoni.
Kama ilivyokuwa kwa mabadiliko yaliyohusu Tume ya Mabadiliko ya Katiba, safari hii nayo vyama vya siasa vilitoa mapendekezo yao.  Yalifanyika mazungumzo kati yao na Serikali na maelewano kufikiwa kuhusu maeneo ya kufanyiwa marekebisho. Serikali ilitayarisha rasimu ya Muswada na kuuwasilisha kwa wenzetu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Ndugu Wananchi;
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilitoa mapendekezo yake na ushauri kwenye maeneo mawili. Kwanza kwamba uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalum ufanywe na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushauriana na kuafikiana na Rais wa Zanzibar.  Pili walishauri kwamba kama Bunge Maalum litashindwa kufikia maamuzi ndani ya siku 70 zilizopendekezwa, liweze kuongezwa muda hadi kufikia siku 90.  Maeneo mengine ya Muswada waliafikiana nayo.
Ndugu Wananchi;
Kwa kuzingatia utaratibu wa kutunga Sheria, Serikali ilifikisha Muswada kwa Spika wa Bunge ambaye nae aliuwasilisha kwenye Kamati ya Kudumu ya Katiba, Sheria na Utawala.  Kama ilivyo ada, Kamati hiyo ilifanya vikao na wadau na kupokea maoni yao kuhusu Muswada.  Nimeambiwa kulikuwa na mjadala wa kina na mapendekezo mazuri yalitolewa na wadau.  Kisha hapo Wajumbe wa Kamati walikaa wenyewe kujadili Muswada walikuwepo pia Wabunge ambao si Wajumbe wa Kamati walioshiriki kwa vile Kanuni zinaruhusu.  Nimeambiwa pia kwamba mjadala ulikuwa mpana na wa kina zaidi.  Mapendekezo kadhaa yalitolewa na Wajumbe kuhusu vifungu mbalimbali vya Muswada.
Ndugu Wananchi; 
Nimefahamishwa kuwa Wabunge wa vyama vyote walichangia na kwamba baadhi ya nyakati mambo yalipokuwa ugumu mawazo mazuri ya baadhi ya Wabunge wa upinzani yalisaidia kupata ufumbuzi.  Nimeambiwa pia kwamba Wajumbe wa Kamati na upande wa Serikali walikubaliana kwa maeneo mengi isipokuwa machache ambayo walikubaliana kwa pamoja wayapeleke Bungeni ili Wabunge nao wayajadili na kuyapatia ufumbuzi.
Ndugu Wananchi;
Baada ya Kamati kumaliza kazi yake, Waziri wa Katiba na Sheria, Mheshimiwa Mathias Chikawe aliwasilisha Muswada Bungeni.  Akafuatiwa na Mheshimiwa Gosbert Blandes kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, kutoa maoni ya Kamati. Baadaye Msemaji wa Kambi ya Upinzani, Mheshimiwa Tundu Lissu  alitoa maoni yake.
Ndugu Zangu;
Baada ya watu hao watatu kutoa maoni yao ilitarajiwa kuwa Wabunge wangeanza kujadili Muswada.  Naambiwa mambo hayakuwa hivyo.  Badala yake kukazuka malumbano baina ya Spika na baadhi ya Wabunge wa Upinzani wakitaka Muswada usijadiliwe.  Ilifikia wakati hoja hiyo ikabidi iamuliwe kwa kura ambapo ilishindwa.  Katika hali isiyotarajiwa, Wabunge wote wa upinzani wakatoka nje ya Bunge isipokuwa wawili.  Kitendo hicho kimewanyima Wabunge wengi wa upinzani fursa ya kutetea hoja zao walizozitoa kupitia hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani.  Pia wamejinyima nafasi ya kusema mambo mengine wakati wa mjadala na Kamati ya Bunge zima.
Wabunge waliokuwepo waliendelea kuujadili Muswada na kutoa hoja na mapendekezo ya kuuboresha.  Walifanya hivyo wakati wa mjadala na wakati wa kupitia kifungu kwa kifungu.  Baadhi ya hoja na mapendekezo yalikubaliwa na mengine yalikataliwa.  Miongoni mwa yaliyokubaliwa na Wabunge, kwa mfano, ni kuhusu elimu ya mtu atakayekuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum na lile la ukomo wa uhai wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Ndugu Wananchi;
Kwa maoni yangu madai ya Kambi ya Upinzani yanazungumzika na hata baadhi yangeweza kukubalika kama Wabunge wake wangekuwepo Bungeni na kushiriki mchakato wote wa kujadili na kupitisha Miswada Bungeni.  Bahati mbaya hawakuwepo, hivyo hapakuwepo na mtu wa kusema mawazo yao.  Baada ya kupoteza fursa yao halali, kutaka kupata ufumbuzi nje ya Bunge ni jambo lisilowezekana.  Haya ni masuala yanayohusu Bunge ambayo hujadiliwa na kuamuliwa Bungeni na si vinginevyo.  Kuandamana nchi nzima au kuchukua hatua za kutotii sheria kama Mwenyekiti wa CHADEMA, Mheshimiwa Freeman Mbowe anavyotaka, hakutaleta mabadiliko wanayoyataka katika sheria hii. Naamini na wao wanautambua ukweli huo.
Ndugu Wananchi;
Kuna msemo wa wahenga kuwa “historia hujirudia”.  Naomba hekima ziwaongoze viongozi wa CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi na zituongoze sote kutumia utaratibu tulioutumia mwaka 2012.  Kulipotokea mazingira kama haya pande zote zilikaa pamoja na kuzungumzia hoja moja baada ya nyingine na kukubaliana nini kifanyike na kifanyike vipi.  Baada ya kuridhiana hatua zipasazo za kisheria na kanuni zilichukuliwa na kumaliza mzozo.
Ndugu Wananchi;
Kufanya kinyume cha hayo hakutaleta ufumbuzi wa mzozo huu.  Tutaliingiza taifa kwenye matatizo yasiyokuwa ya lazima.  Tukikataa kufanya hayo Watanzania wanayo kila sababu ya kuhoji dhamira zetu na kutilia shaka nia zetu.  Watakuwa na haki ya kuuliza nia ni hii yetu sote ya kupata Katiba Mpya kwa kutumia njia za kikatiba na kisheria au tuna dhamira nyingine iliyojifisha?
Kama dhamira yetu ni kutaka kupata Katiba mpya kwa mujibu wa Katiba na Sheria, ushauri wangu na rai kwa ndugu zetu wa CHADEMA, CUF na NCCR-Maguezi ni kuwa waachane na mipango ya maandamano na kufanya ghasia.  Badala yake watumie njia halali zinazotambulika kikatiba na kisheria kujenga hoja za kufanya marekebisho wanayoyaona wao yanafaa kuboresha Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.  Tukifanya hivyo tutakuwa tunajenga badala ya kubomoa.  Tutaliponya taifa.  Sisi katika Serikali tuko tayari.
Ndugu Wananchi;
Napenda pia kuzisemea baadhi ya hoja zilizotolewa na Kambi ya Upinzani.   Kwanza kabisa nasema kuwa nimesikitishwa sana na madai na tuhuma za uongo eti katika uteuzi wa Tume ya Katiba sikuheshimu mapendekezo ya TEC, CCT na walemavu.  
Ndugu Zangu, Watanzania Wenzangu;
Siyo tu kauli hiyo ya Mheshimiwa Tundu Lissu ni uzushi na uongo mtupu bali pia ni ya unafiki, fitina na uzandiki wa hali ya juu.  Nasema hivyo kwa sababu, sipendi kuamini kuwa Mheshimiwa Mbunge amesema yale kwa kutokufahamu ukweli au kwa bahati mbaya.  Amesema yale kwa makusudi mazima ya kupotosha ukweli ili pengine isaidie kujenga hoja yake ya kutaka Rais asiteue wale Wajumbe 166 wa Bunge Maalum.
Napenda ieleweke kuwa siishabikii kazi hiyo, lakini kwa kutimiza wajibu na maslahi ya taifa nikiagizwa na Sheria za nchi nitafanya.  Nasema hivyo kwa sababu nafahamu ni kazi ngumu.  Kama kazi ya uteuzi wa Wajumbe 30 wa Tume haikuwa rahisi hata kidogo, hii ya uteuzi wa watu 166 itakuwa ngumu zaidi.  Ile ya Tume ilikuwa ngumu kwa namna mbili.  Kwanza, kwamba taasisi zilizoomba na waombaji walikuwa wengi mno kuliko nafasi za kujaza yaani 15 Zanzibar na 15 Bara.  Zanzibar ziliomba taasisi zaidi ya 60 na waombaji walikuwa zaidi ya 200 wakati Bara kulikuwa na taasisi zaidi ya 170 zikiwa na waombaji zaidi ya 500.  Kupata watu 30 kutoka orodha kubwa kiasi hicho si mtihani mdogo.  Pili kwamba tulitakiwa kuunda Tume inayoasili sura ya taifa, yaani watu wa nchi yetu kwa maeneo, vyama vya siasa, dini, wanawake, vijana, walemavu, wafanyakazi, wasomi, Wabunge, Wawakilishi, wanasheria, wafanyabiashara, wakulima, asasi za kiraia n.k.
Ndugu Wananchi;
Pamoja na changamoto hizo, lakini tulifanikiwa kuunda Tume iliyopokelewa vizuri na jamii na kufanya watu wengi hata wale ambao hawakuteuliwa wahisi kuwakilishwa.  Tulifanyaje? Kwanza kabisa tulihakikisha kuwa tunapata wawakilishi wa vyama vya siasa vyenye wawakilishi Bungeni na kwenye Baraza la Wawakilishi na tunapata wawakilishi wa mashirika ya dini zetu kubwa yaani, TEC, CCT na BAKWATA.    Ndiyo maana nikasema kuwa kwa Mheshimiwa Tundu Lisu kudai kuwa mapendekezo ya TEC na CCT hayakuheshimiwa ni uongo wa mchana usiokuwa na kichwa wala miguu.
Baada ya hapo ndipo tukaangalia waombaji wa makundi na taasisi nyingine.   Tulijitahidi sana kupata watu ambao wanawakilisha kundi zaidi ya moja.  Tulifikiria hivyo kwa sababu ni ukweli ulio wazi kuwa si kila taasisi iliyoomba itapata mwakilishi kwani hata tungependa iwe hivyo nafasi hazikuwepo.  Kwa kutumia utaratibu huu makundi mengi yamepata uwakilishi kutokana na watu waliopendekezwa na makundi mengi.  Tumefanya kazi kubwa sana ya kuwianisha mambo na makundi ya maslahi mbalimbali nchini.
Ndiyo maana naiona mantiki ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akishirikiana na Rais wa Zanzibar wa kuwateua Wajumbe wa Bunge Maalum.  Dhana kuwa kila kikundi kiteue chenyewe watu ingefaa sana kama kungekuwepo na nafasi za kutosha kila kundi nchini.  Hilo haliwezekani, labda tuwe na Bunge Maalum lisilokuwa na ukomo wa wajumbe.
Ndugu Wananchi;
Mimi na Rais wa Zanzibar tumekuwa tunajiuliza baada ya kazi ngumu na nzuri tuliyoifanya na iliyopongezwa na wengi ya kuteua Tume ya Mabadiliko ya Katiba nini kilichoharibika sasa hata tuonekane hatuaminiki kuteua hawa 166?  Kama ni kwa sababu za Mheshimiwa Tundu Lissu, nimeshasema hazina ukweli wowote.  Ninapojiuliza kwa nini aseme uongo nashindwa kupata jibu linaloingia akilini.  Wakati mwingine nafikiria kuwa ni hiana.  Lakini nadhani ni hila za kisiasa zenye nia ya kutaka kupata watu wa kutetea maslahi ya chama chake.  Kama hiyo ndiyo shabaha basi amekosea sana.
Ndugu Zangu, Watanzania Wenzangu;
Hatutengenezi Katiba ya Chama fulani bali Katiba ya nchi, Katiba ya watu wa vyama vyote na wasiokuwa na vyama ambao ndiyo wengi kuliko wote.  Lazima tuongozwe na ukweli huo na tuwe na msimamo huo wakati wote.  Lazima tukumbuke kuwa si watu wote wanaostahili au kuwa na sifa ambao wataomba na kupata nafasi ya kuwa Wajumbe, hivyo wale wachache watakao bahatika lazima wawasemee wote.  Wanatakiwa kusikiliza na kuwakilisha mawazo ya wote hata wale wasiokuwa wa Chama chao au kundi lao.
Ndugu Wananchi;
Bahati nzuri hii ndiyo sifa kubwa iliyooneshwa na Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.  Wamewasimamia na kuwasemea watu wote bila ya kubagua.  Natambua kuwepo kwa baadhi ya watu ambao hawafurahii msimamo huo na matokeo ya kazi yao.  Watu hao kuwalaumu Wajumbe wa Tume kwa ajili hiyo ni kuwaonea na kutowatendea haki.  Tunataka watakaokuwa Wajumbe wa Bunge Maalum nao waige mfano huu mzuri.  Wajali maslahi mapana ya taifa letu na watu wake badala ya kujali yale ya taasisi zao au makundi yao.
 Zanzibar Kutokushirikishwa
Ndugu Wanachi;
Nimeambiwa pia kuliwepo madai ya Zanzibar kutokushirikishwa ipasavyo.  Nimeeleza kwa kiasi gani Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeshirikishwa na kutoa maoni yake yaliyojumuishwa katika Muswada.  Hivyo basi napata tabu kuyaelewa madai kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar haikushirikishwa msingi wake nini!  Labda kuna kitu sikuambiwa!
Nimeulizia kuhusu hoja ya Kamati kutokufanya vikao Zanzibar kusikiliza maoni ya wadau wa Zanzibar.  Nimeambiwa kuwa Kanuni za Bunge hazina sharti hilo hivyo Kamati haistahili kulaumiwa.  Kama hivyo, nashauri kuwa suala hili lirudishwe Bungeni ili Wabunge walizungumze na kulifanyia uamuzi muafaka. Vinginevyo watu wataendelea kulauminiana isivyostahili.  Hivyo basi, kuligeuza jambo hili kuwa ni suala la kukataa Muswada au kususia vikao vya Bunge au kufanya maandamano sidhani kama ni sawa.
Ndugu Wananchi;
Nimeambiwa pia kuwa kulikuwa na hoja ya kutaka idadi ya Wajumbe wa kutoka Tanzania Bara na Zanzibar iwe sawa kama ilivyo kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba.  Sababu ya idadi ya Wajumbe wa Tume kuwa sawa inatokana na utaratibu wao wa kufikia uamuzi.  Ni kwa maelewano ya wote (consensus) na siyo kwa kupiga kura.  Ndiyo maana idadi imewekwa sawa ili sauti za pande zote zisikike sawia.  Bunge Maalum lina sharti la kufanya uamuzi kwa theluthi mbili ya kura za kila upande kukubali.  Bila ya hivyo hakuna uamuzi.
Hivyo basi, katika Bunge Maalum nguvu si uwingi wa kura ambazo upande fulani unaweza kupata bali ni ulinganifu sawa wa kura za kila upande peke yake.  Huu ndiyo msingi unaotumika katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivi sasa kwa lengo la kulinda maslahi ya Zanzibar.  Zanzibar ina Majimbo 50 ya uchaguzi na Tanzania Bara ina Majimbo 189, hivyo ukiamua kwa wingi kila wakati Wazanzibari watashindwa.  Lakini, hapajakuwepo madai ya Zanzibar nao kutaka kuwa na idadi sawa ya majimbo kama Bara au kupunguza majimbo ya Bara yawe sawa na ya Zanzibar kwa sababu wingi si hoja. Msingi unaotumika ni kutoa nguvu sawa za uamuzi kwa kila upande wa Muungano wakati wa kuamua masuala ya Katiba.  Hakuna mdogo wala mkubwa, wote wako sawa.  Hakuna mdogo kumezwa na mkubwa.  Ndiyo msingi unaopendekezwa kutumika kwenye Bunge Maalum hivyo hakuna kitakachoharibika kwa idadi ya Wajumbe kutokukulingana.  Nadhani inafaa ibaki ilivyo.  Lakini kama Wabunge wataamua waongeze idadi itakuwa kwa sababu nyingine siyo hii ya mfano wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Ndugu Wananchi;
Katika orodha ya madai ya ndugu zetu wa upinzani lipo suala la uhai wa Tume ya Katiba.  Wanataka usiishe wanapokabidhi rasimu ya pili kwa Bunge Maalum bali waendelee kuwepo mpaka mwisho wa mchakato.  Nimeulizia ilikuwaje?  Nimeelezwa kuwa jambo hili halitokani na mapendekezo ya Serikali wala ya Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala.  Limetokana na pendekezo la Mbunge katika Bunge wakati wa kupitia vifungu na kuungwa mkono na Wabunge wengi.  Kwa hiyo kuilaumu Serikali si haki.  Serikali inaweza kuwa mshirika katika hoja hii.
Nami naiona hoja ya Wajumbe wa Tume kuwa na wajibu wakati wa Bunge Maalum hasa wa kusaidia kufafanua mapendekezo ya Tume.  Je ushiriki huo uwe vipi? Je ni Wajumbe wote au baadhi yao ni jambo linaloweza kujadiliwa.
Ndugu Wananchi;
Naomba nimalizie kwa kuwasihi viongozi wa CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi kuongozwa na hekima iliyotumika wakati tulipokuwa na tatizo linalofana na hili kuhusu Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Mimi naamini kama iliwezekana kufanikisha mambo wakati ule inaweza kufanya hivyo hata safari hii. Itatufikisha pale tunapopataka salama salimini bila maandamano, kushupaliana au uvunjifu wa amani.  Kupanga ni kuchagua, naomba sote, mmoja mmoja na kwa umoja wetu tuchague njia ya mazungumzo na maelewano kwani itaihakikishia nchi yetu amani, usalama na utulivu. Tukifanya hivyo historia itatuhukumu kwa wema.
Mungu Ibariki Tanzania.  
Nawashukuru sana kwa kunisikiliza.

Thursday, October 3, 2013

BIG RESULTS NOW KATIKA MAZINGIRA KAMA HAYA, KAZI BADO IPO


Katika mazingira kama haya, tutapata Wakurugenzi, Wabunge, Mawaziri, Makatibu Wakuu, Mabalozi na  Maraisi kweli?










       Na hili nalo ni darasa ati. Mwalimu yupo kazini kama unavyoona



Waliponiona, wote waligeuka kuangalia ninavyowapiga picha. Walifurahi haoo!
 
Hili pia ni darasa.













Mdau unaionaje hali hii? kazi kwenu. Mi nshafanya yangu, na ninyi wadau mfanye yenu. Kila mmoja katika nafasi yake atimize wajibu ili kuwakomboa watoto waliokatika mazingira magumu kama haya.

GAIDI LA KIINGEREZA LAZUA TAHARUKI DAR

 

 Afananishwa na Samantha
  Akamatwa, ahojiwa Polisi
 
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam,Kamishna Suleiman Kova
Gaidi Samantha Lewthwaite maarufu kama ‘mjane mweupe’ raia wa Uingereza anayedaiwa kuhusika katika tukio la shambulizi la kigaidi jijini Nairobi, Kenya mwezi uliopita, amezua tafrani kubwa baada ya kuzuka uvumi kuwa ameonekana katika benki moja jijini Dar es Salaam.

Mjane mweupe ni gaidi anayehusishwa na tukio la ugaidi kwenye kituo cha biashara cha Westgate jijini Nairobi Septemba 14, mwaka huu na anatafutwa na vyombo vya usalama vya Kenya na polisi wa kimataifa (Interpol) kwa udi na uvumba.

Gaidi huyo anadaiwa kuwa ndiye aliyeongoza katika mashambulizi hayo yaliyoua watu 67 na  kujeruhi zaidi 200 katika kituo hicho na kufanikiwa kutoroka kwa kujifanya kuwa mmoja watu waliokuwa wakijiokoa.

Kutokana na kutoroka kwa gaidi huyo, vyombo vya usalama katika nchi za Afrika Mashariki vimekuwa macho kufuatilia watu ambao wanahisiwa kuwa wanahusika na shambulizi hilo linalodaiwa kusukwa na kutekelezwa na mtandao wa kigaidi wa al Shaabab kwa kushirikiana na Al Qaeda.

Kufuatia hali hiyo, mwanamke mmoja raia wa Uingereza, jana alikamatwa na Jeshi la Polisi Tanzania baada ya kutiliwa shaka akifananishwa na gaidi huyo mtukutu.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo NIPASHE imezipata ambazo pia zimesambazwa katika mitandao ya kijamii, mwanamke huyo alikamatwa katika benki ya Exim tawi la Tower jijini Dar es Salaam baada ya wafanyakazi wa benki hiyo kumtilia shaka.

Chanzo cha habari kutoka katika benki hiyo kilieleza kuwa mwanamke huyo shombe alifika katika ofisi za benki hiyo makao makuu kuomba tenda ya kusafisha jengo.

Mwanamke huyo ambaye Jeshi la Polisi bado halijataja jina lake, alifika katika benki hiyo Jumatatu ili aonane na meneja, lakini aliambiwa aende kesho yake yaani juzi.

Habari zinasema kuwa baada ya kufika makao makuu ya benki hiyo, aliambiwa meneja hayupo, ndipo alipoibua hoja mpya na kuwaambia wafanyakazi wa benki kuwa angelipenda kufungua akaunti kwenye tawi la benki hiyo.

Baada kukubaliwa aliambiwa awasilishe nyaraka za kumtambulisha, lakini akadai ni raia wa kigeni na hana nyaraka zozote na alipoulizwa anakaa wapi, alidai kwenye nyumba za kupanga za Uhuru Heights.

Wafanyakazi wa benki hiyo baada ya kuona maelezo yake hayajitoshelezi, walitoa taarifa polisi wanaolinda jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi jirani na benki hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Polisi walifika eneo hilo na kumkamata mwanamke huyo na kumpeleka Kituo Kikuu cha Polisi na alipofanyiwa uchunguzi, ilibainika alivaa lenzi kwenye macho na pia usoni alikuwa amejipaka vitu ambavyo vilikuwa havionyeshi vizuri uso wake.

Kufuatia hali hiyo, polisi walimwamuru anawe uso na baada ya kufanya hivyo, sura yake ya Kishombe ikapotea na kubaki kama Mzungu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Manongi, alipolizwa kuhusu tukio hilo, alisema hakuwa na taarifa.

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova, alithibitisha kukamatwa kwa mwanamke huyo katika benki ya Exim baada ya kutiliwa shaka na wananchi.

Alisema baada ya kumfanyia uchunguzi, ilibainika kuwa siyo gaidi kama ilivyokuwa inahisiwa, badala yake na ana mume ambaye yupo jijini Dar es Salaam.

“Huyu mwanamke ni raia wa Uingereza, alipokamatwa alikutwa amevaa hijab na kimsingi wananchi ndiyo waliomtilia shaka, lakini siyo gaidi kama yule anayetuhumiwa kufanya ugaidi jijini Nairobi, Kenya,” alisema Kova. Kamishna Kova alisema mwanamke huyo aliachiwa baadaye baada ya kubainika kuwa ameolewa na mume wake yupo Dar es Salaam.

Alisema kilichowafanya wananchi wamtilie wasiwasi ni uvaaji wake wa nguo ambao uliwafanya wahisi huenda anafanana na gaidi wa tukio la Kenya.

Kamishna Kova alipongeza wananchi kwa jinsi wanavyokuwa makini katika suala la ulinzi na usalama wa nchi yao kwa kuwashuku watu ambao hawawaelewi na kuwataka kuendelea kushirikiana na jeshi hilo.

Mwishoni mwa wiki iliyopita, Mkuu wa Rasilimali watu wa Jeshi la Polisi, DCP Thobias Andengenye, alitoa taarifa kuwa jeshi hilo litamsaka gaidi Samantha Lewthwaite anayedaiwa kupitia mpaka wa Namanga mkoa wa Arusha kabla ya kwenda kufanya tukio Nairobi ili kumzuia kufanya uhalifu zaidi.

Andengenye alikuwa akihojiwa katika kipindi cha kipima joto kinachorushwa na kituo cha televisheni cha ITV kilichokuwa kikijadili Watanzania wamejifunza nini katika kuchukua hatua juu shambulio la ugaidi lililotokea Nairobi.

Andengenye alisema Jeshi la Polisi limejipanga kumsaka gaidi huyo ili asije akatenda uhalifu zaidi na kwamba ufuatiliaji wa mwanamke huyo hautafanywa kwenye mipaka bali hata ndani ya nchi.
Chanzo: Nipashe    

PICHA ZA NDEGE ILIYOANGUKA NIGERIA LEO

Ndege iliyokuwa imebeba abiria wapatao ishirini imeanguka muda mfupi mara baada ya kuruka katika uwanja wa ndege wa Murtala Muhammed huko Lagos Nigeria mapema leo baada ya kupata hitilafu ya injini. Ndege hiyo ilikuwa inaelekea mjini Akure Kusini Magharibi mwa Nigeria.

Katika ajali hiyo, watu 8 wamefariki dunia. Angalia picha za ndege hiyo hapa chini.
Click for Full Image Size

          Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size
Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size Click for Full Image Size
Chanzo: Nigerian news

Friday, September 27, 2013

AJALI YAUA WATATU NA KUJERUHI WANNE TABORA

 

Samahani kwa picha utakayoiona hapo chini

Mwili wa kijana mmoja 
aliyefahamika kwa jina la
 Rashidi Seleman mkazi
 wa Isevya manispaa ya
 Tabora ambaye amepoteza
 maisha baada ya Lori walilokuwa
 wamepanda kuanguka eneo la
 Inala barabara ya kwenda 
Kigwa,Polisi wamesema chanzo 
cha ajali hiyo ni mwendo
 kasi wa dereva ambaye 
amekimbia huku watu
 wengine wanne wakiwa 
wamejeruhiwa vibaya ambao 
wamelazwa katika hospitali ya Rufaa ya Kitete.
Tatizo la ukosefu la ukosefu wa vifaa vya kuokolea vilisababisha maiti ya mtu huyo kukaa muda mrefu akiwa amebanwa na Lori hilo ambalo ni mali ya kampuni ya mkandarasi JOSSAM


Awali jitihada za Polisi na wananchi ziligonga mwamba na kubaki wakiiangalia maiti hiyo pasipo msaada wowote ajali ambayo imetokea majira ya saa kumi jioni hapo jana.

Askari wa usalama barabarani wakiongozwa na kamanda wa Polisi kikosi cha usalama barabarani wilaya ya Tabora Bw.Swaleh Digega hatimaye wakafanikiwa kuutoa mwili wa marehemu huyo na kuupeleka hospitali ya mkoa wa Tabora Kitete kwa ajili ya kuuhifadhi....Hata hivyo Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Sumatra wanakusudia kumfikisha mahakamani mmiliki wa Lori hilo kwa kitendo cha kusafirisha mizigo na wanadamu katika gari hilo lenye nambari za usajili T 702 ACR ambalo ni ISUZU TX

CHANZO:Mdodosaji