LATEST POSTS

Tuesday, January 28, 2014

Mnyukano mpya CCM

mawaziri ‘mizigo’

WAKATI Chama Cha Mapinduzi (CCM), kiko njia panda baada ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete, kuwarejesha mawaziri ‘mizigo’ waliopendekezwa na chama chake wang’olewe, makundi ya urais yameanza kupigana vikumbo kuwania nafasi tatu za ujumbe wa sekretarieti.

Nafasi hizo nyeti ndani ya chama hicho tawala, ziko wazi baada ya Rais Kikwete kufanya mabadiliko ya mawaziri na kuwaondoa wajumbe watatu wa sekretarieti na kuwaingiza kwenye Baraza la Mawaziri.
Nafasi za ujumbe wa sekretarieti, zinapiganiwa kwa udi na uvumba, kwani ndio wanaosukuma ajenda kwenda Kamati Kuu (CC), Halmashauri Kuu (NEC) na hatimaye Mkutano Mkuu.
Pia wajumbe wa sekretarieti wanapata fursa ya kuwa wajumbe wa Kamati Kuu na NEC taifa.
Wajumbe walioondolewa kwenye sekretarieti ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu (Bara), Mwigulu Nchemba, ambaye sasa ni Naibu Waziri wa Fedha, Wizara ya Fedha na Uchumi (Sera).
Wengine ni Asha-Rose Migiro, ambaye kwa mabadiliko hayo anakuwa Waziri wa  Katiba na Sheria na Jenista Mhagama, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, akichukua mikoba ya  Philip Mulugo, aliyetupiwa virago.
Chini ya utaratibu mpya wa CCM, wajumbe wa sekretarieti wanaoteuliwa kuwa mawaziri wanalazimika kuachia nafasi zao za chama ili wawe na muda zaidi wa kuitumikia serikali.
Kutokana na nafasi hizo kuwa wazi, habari zinasema vikumbo vya kujaza nafasi hizo vimeanza, huku makundi ya urais yakijipanga kuhakikisha wanapenyeza watu wao.
Kwa kawaida, nafasi hizo hujazwa baada ya Mwenyekiti wa CCM taifa, Rais Kikwete kuteua majina ya makada anaotaka waingie kwenye sekretarieti na kisha majina hayo huthibitishwa na Kamati Kuu (CC) na kupigiwa kura na wajumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM.
Licha ya mamlaka ya uteuzi kuwa chini ya Rais Kikwete kama ilivyo kwa mawaziri, vigogo na makada waliokaribu na rais wameanza kuhaha kutumia mbinu mbalimbali kuhakikisha majina ya watu wao yanateuliwa.
Pamoja na nafasi ya Migiro na Mhagama, nafasi ya Mwingulu, ya Naibu Katibu Mkuu Bara, ndiyo inayotolewa macho zaidi.
Duru za siasa ndani ya CCM zinataja majina mawili, mosi la aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi na Nape Nnauye, ambaye kwa sasa ni Katibu wa Itikadi na Uenezi taifa.
“Kuna uwezekano mkubwa kati ya mawaziri wanne waliong’olewa bungeni, wawili wanaweza kuingia kwenye sekretarieti. Nchimbi ana nafasi ya kuziba nafasi ya Nchemba kuwa naibu katibu mkuu,” alisema mtoa habari wetu.
Kwa mujibu wa habari hizo, mwingine anayetajwa huenda akateuliwa kuziba nafasi ya Waziri Migiro ni Balozi Khamis Kagasheki ambaye kabla ya mabadiliko ya mawaziri, alikuwa Waziri wa Maliasili na Utalii.
Duru za siasa ndani ya CCM z
inamtaja Balozi Kagasheki kufiti kwenye nafasi ya Migiro kutokana na uzoefu wake wa siasa za nje alipokuwa Balozi wa Tanzania katika nchi mbalimbali.
Hivi karibuni, Rais Kikwete alifanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri kwa kuwateua wajumbe watatu wa sekretarieti ya CCM kuwa mawaziri na kufanya kuwapo sura kumi mpya.
Pia aliwarejesha mawaziri ‘mizigo’ ambao hivi karibuni walipendekezwa na Kamati Kuu (CC) ya CCM kwamba wang’olewe kwa utendaji wao mbovu.
Chimbuko la mawaziri ‘mizigo’ lilitokana na ziara ya Katibu Mkuu, Abdulhaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi taifa, Nape Nnauye katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ambapo waliwataja baadhi ya waziri kuwa ni mizigo.
Mawaziri waliotajwa kuwa ‘mizigo’ ni pamoja na Waziri wa Kilimo na Chakula, Christopher Chiza, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia na Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: