LATEST POSTS

Wednesday, October 14, 2015

SHERIA YA MTANDAO YAMGUSA MWINGINE MKOANI DODOMA



Mtayarishaji wa vipindi, Sospiter Jonas amefikishwa katika Mahakama ya Mwanzo ya Dodoma Mjini akishtakiwa kwa matumizi mabaya ya mtandao.
Sospiter alisomewa mashtaka hayo na Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Mussa mbele ya Hakimu wa Mahakama hiyo Emmanuel Bwile.
Mshtakiwa huyo anadaiwa kuandika katika ukurasa wake wa Facebook ujumbe kuwa “Pinda utakuwa muhubiri wa injili tu.”
Mussa aliiambia Mahakama kuwa mshtakiwa huyo alibandika picha ya John Maliga kwenye ukurasa wake wa Facebook na kuandika ujumbe huo, kitendo ambacho ni kinyume cha kifungu namba 16 cha Sheria ya Mtandao ya Mwaka 2015.
Mlalamikaji katika shauri hilo la jinai namba 815/2015 litakalokuja tena mahakamani Oktoba 19, ni John Maliga.
Mshtakiwa yupo nje baada ya kutimiza masharti ya dhamana iliyomtaka kuwa na mdhamini mmoja na bondi ya Sh1 milioni.
Kesi hii imekuja baada ya wiki iliyopita, kijana mmoja, Benedict Ngonyani (24) kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam akituhumiwa kusambaza taarifa za uongo zinazomhusu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Davis Mwamunyange.
Kijana huyo anatuhumiwa kuandika katika ukurasa wake wa Facebook na WhatsApp kuwa, Mwamunyange, amelazwa kwenye hospitali moja mjini Nairobi, Kenya kwa madai ya kulishwa chakula chenye sumu

0 comments: