LATEST POSTS

Saturday, September 14, 2013

UFISADI MARUFUKU KALIUA- ASEMA MHE. IBRAHIMU KIFOKA MAKAMU MWENYEKITI WA HALMASHAURI YA WILAYA


HALMASHAURI ya Wilaya mpya ya Kaliua mkoani Tabora, imetoa onyo kali kwa watumishi wote wa halmashauri hiyo kutokuthubutu kujihusisha na vitendo vya kifisadi katika fedha za miradi ya maendeleo.
Onyo hilo limetolewa juzi na Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Mhe. Ibrahim Kifoka, alisema hayo alipokuwa katika kikao cha waandishi wa habari muda mfupi baada ya madiwani wa halmashauri hiyo kumaliza ziara ya siku moja jijini Mwanza.
Alisema siku zote vitendo vya kifisadi vimekuwa vikirudisha nyuma maendeleo ya wananchi, hivyo uongozi wa halmashauri hiyo utawachukulia hatua kali watumishi wote watakaobainika kujihusisha na hujuma hizo.
Kifoka ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Silambo, alisema jitihada zilizopo sasa ni kuhakikisha utekelezaji wa miradi na uwekezaji unatekelezwa kwa mujibu wa taratibu na sheria za nchi.
 
 
Wa kwanza kulia ni Mheshimiwa Ibrahimu Kifoka (mwenye tisheti ya rangi nyekundu na nyeupe) akiwa katika picha ya pamoja na Mheshimiwa diwani wa Kata ya Sasu Mhe. Jafael Lufungija na mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua Mhe. John Kadutu ( mwenye miwani.
“Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua inaamini kila kiongozi lazima asimamie majukumu yake vizuri kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.
“Hatutakubali fedha za maendeleo zitumike vibaya, tunataka zitumike vema kwa malengo yaliyokusudiwa,” alisema.
Naye Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Bw. Florence Mwale, ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Ardhi na Maliasili, alisema uongozi wa halmashauri hiyo umejizatiti kukabiliana na changamoto za kimaendeleo baina ya wananchi wake.
Alisema rasilimali na fursa za kimaendeleo zilizopo wilayani humo lazima zitumike kwa vitendo kutatua adha mbalimbali zinazowakabili wananchi.
Chanzo: Tanzania Daima


0 comments: