LATEST POSTS

Monday, January 27, 2014

Majambazi wateka magari, wafanya ukatili wa kutisha

WATU wanaodhaniwa kuwa majambazi, usiku wa kuamkia jana wameteka magari mawili ya mafuta na kuwadhuru watu waliokuwa kwenye magari hayo kwa kuwakata mapanga na wengine wakidaiwa kukatwa masikio.
Tukio hilo lilitokea katikati ya Kijiji cha Kitangili na Miguwa nje kidogo ya Mji wa Nzega, mkoani Tabora.
Inadaiwa kuwa, magari hayo yalikuwa yakitokea nchini Burundi kwenda Dar es Salaam ambapo watekaji hao walikuwa wakitaka fedha.
"Walipoambiwa fedha hakuna, hawa majambazi walisisitiza fedha wanazo kwani wametoka safari ya mbali hivyo wasipotoa watawadhuru, walianza kuwapiga kwa mapanga na kuwajeruhi.
"Tukio hili halikuwafurahisha wakazi wa Nzega na madereva wengine wa magari ya mizigo hivyo wamefunga barabara wakishinikiza kutaka waonane na Mkuu wa Mkoa Bi.Fatma Mwassa, wamueleze kilio chao," alisema mkazi wa eneo hilo katika eneo la tukio.
Madereva wa magari makubwa waliozungumza na Majira, walisema eneo hilo limekuwa likitumika kama kichaka cha kutekea magari na kujeruhi wananchi.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Dkt. Emmanuel Mihayo, alisema amepokea majeruhi watatu usiku wa kuamkia jana wakiwa wamejeruhiwa vibaya.
Alisema mmoja kati ya majeruhi hao alikuwa hajitambui na wengine wawili wakiwa mmoja kati yao amekatwa sikio na shavu la kushoto kwa mapanga na mwingine mguu.
Dkt. Mihayo alisema, bado wanaendelea na matibabu kwa majeruhi wote ambao hakuwataja majina yao.

Chanzo: Majira


0 comments: