LATEST POSTS

Wednesday, January 22, 2014

Wananchi wadaiwa kumuua mama, mtoto Tabora

Nzega. Licha ya Serikali kupiga vita kujichukulia sheria mikononi, unyanyasaji na mauaji ya wanawake, baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Uchama wilayani Nzega mkoani Tabora wamemuua mwanamke mmoja na mtoto wake wa kike kwa sababu zisizofahamika.
 
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoani Tabora, Peter Ouma alisema tukio hilo limetokea Januari 17 mwaka huu katika kijiji hicho.
 
Kamanda Ouma aliwataja mama na mtoto waliouawa kinyama na watu wasiofahamika kuwa ni Amina Kabingu(45) na mwanaye Shija Mtaki(12) ambaye ni mwanafunzi wa darasa la tano katika Shule ya Msingi Uchama.
 
Alisema kuwa Amina Kabingu na mtoto wake shija walikuwa wakisafisha majaruba ya kulimia mpunga katika mashamba yao majira ya jioni, ndipo watu wasio fahamika waliwavamia na kuanza kuwashambulia kwa vitu vyenye ncha kali kusababisha kupoteza maisha yao.
 
Diwani wa kata hiyo, Karoli Masanja alilitaka jeshi la jadi la Sungusungu kuwasaka wauaji hao kwa kushirikiana na Polisi ili kuwabaini wahalifu hao waliofanya ukatili.
 
Karoli alisema serikali ichukue hatua kali kudhibiti mauaji hayo ikiwa ni pamoja na vyombo vya dola kuzingatia wajibu wake wa kutenda haki kwa jamii husika.
 
Toka Januari 1 mwaka huu hadi Januri 18 mwaka huu wanawake watatu wameuawa kinyama huku mmoja akipigwa na kubakwa ikiwa ni pamoja na kuvunjwa baadhi ya viungo vya mwili wake.

Chanzo: Mwananchi

0 comments: