LATEST POSTS

Friday, March 21, 2014

Muswada wa kupinga ushoga

Mbunge wa Jimbo la Nyamagana, Ezekia Wenje amewasilisha bungeni kusudio la kupeleka muswada wa kukataza na kudhibiti vitendo vya ushoga nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mara baada ya kukabidhi kusudio hilo kwenye ofisi za Bunge, alisema amewasilisha kwa mujibu wa Kanuni za kudumu za Bunge kifungu cha 81 (1) na (2).
Wenje alisema ameamua kupeleka kusudio la muswada huo, ili kuwalinda watoto na vijana wa Tanzania dhidi ya mwenendo mbaya wa ushoga na usagaji.
Alisema watoto na vijana wamekuwa katika hatari ya kuharibiwa kimaadili, kimakuzi, kimalezi na kimaumbile.
“Muswada una lengo la kujaza mianya ya kisheria iliyoachwa na sheria ya Kanuni za Makosa ya Adhabu Sura ya 16 ya sheria zetu,” alisema. Mbunge huyo alifafanua kuwa katika kifungu cha 154 cha Kanuni ya Adhabu ni kosa kufanya tendo la ndoa kinyume cha maumbile.
Hata hivyo, alisema sheria haijatamka kuwa ni kosa kushabikia, kufundisha, kusambaza vifaa vinavyotumika kufanya vitendo hivyo, kuchapisha na kufanya mambo mengine ambayo yanahamasisha vitendo hivyo.
“Madhumuni ya muswada huu ni kutunga sheria mahususi inayolinda desturi na maadili ya kifamilia ya Watanzania,” alisema.
Alisema anakusudia jina la muswada huo liwe ni Muswada wa Kukataza na Kudhibiti Vitendo vya Ushoga na Usagaji 2014.

0 comments: