LATEST POSTS

Friday, April 11, 2014

Kikwete achaguliwa kiongozi bora Afrika

 
Rais Jakaya Kikwete akihutubia alipokuwa akifungua mkutano wa 19 wa mwaka wa Tafiti za sera na Maendeleo (Repoa) uliofanyika katika Hoteli ya Bahari Beach jijini Dar es Salaam.

Rais Jakaya Kikwete amechaguliwa kuwa kiongozi mwenye mchango mkubwa zaidi katika maendeleo barani Afrika kwa mwaka 2013.
Heshima hiyo kwa Rais Kikwete imetolewa na jarida la kimataifa la African Leadership Magazine Group na tuzo yake ilitarajiwa kutolewa jana jioni katika sherehe iliyopangwa kufanyika kwenye Hoteli ya St.Regis, Washington D.C, Marekani.
Taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu ilisema kuwa tuzo hiyo ilitarajiwa kupokewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe kwa niaba ya Rais Kikwete.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, tuzo hiyo hutolewa kwa viongozi wa Afrika ambao hutoa mchango mkubwa wa kiuchumi na kijamii kila mwaka kwa watu wao, kama ilivyokuwa kwa Rais Kikwete kutokana na mwelekeo wake wenye mafanikio kwa masuala ya utawala bora.
Taarifa hiyo ilisema kuwa jarida hilo limetambua utawala bora chini ya uongozi wa Rais Kikwete ambao limesema umeifanya Tanzania kuwa nchi ya kupigiwa mfano na kituo cha uhakika cha uwezeshaji kutokana na mageuzi yaliyofanywa katika sera na mifumo ya uchumi.
Ilisema kuwa, Rais Kikwete alikuwa chaguo la kwanza la wasomaji wa jarida hilo ambao walipiga kura kupitia njia mbalimbali za mawasiliano za jarida hilo.
“Kuhusu maoni ya wasomaji wetu juu ya kiongozi yupi wa Afrika ambaye ni hodari zaidi kwa maendeleo ya kiuchumi na maendeleo, matokeo ya majibu ya swali hilo yamedhihirisha bila shaka yoyote kuhusu nafasi ya Rais Kikwete katika uongozi wa nchi yake,” taarifa ya Ikulu imelinukuu jarida hilo na kuongeza: “Ushahidi uko kila mahali, ameweza kusimamia uchumi ambao umekuwa kwa wastani wa asilimia saba kwa miaka yote ya uongozi wake.”
Sherehe hizo za kukabidhi tuzo zilitarajiwa kutumiwa na jarida hilo kutangaza mafanikio ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Kikwete kwa jumuia ya kimataifa, taasisi za kibiashara na kwa wanadiplomasia.

0 comments: