LATEST POSTS

Tuesday, August 5, 2014

HAKIMU MLA RUSHWA AHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA MITATU - TABORA

ALIYEKUWA Hakimu wa Wilaya ya Urambo, Oscar Bulugu, aliyekuwa akikabiliwa na mashitaka matatu ya kuomba na kupokea rushwa, amehukumiwa kulipa faini ya shilingi milioni moja na nusu au kutumikia kifungo cha miaka mitatu jela.
Hukumu hiyo imetolewa mwishoni mwa wiki iliyopita na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Shinyanga, Massele Chaba, baada ya kuridhika na ushahidi wa upande wa mashitaka.
Katika hukumu hiyo iliyosomwa kwa saa mbili, Hakimu Chaba, alisema kuwa analazimishwa na matakwa ya sheria kutoa adhabu hiyo kwa mshitakiwa aliyetiwa hatiani, na ikiwa hajaridhika anaruhusiwa kukata rufaa.
Bulugu, alifikishwa mahakamani hapo mwaka jana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, akikabiliwa na mashitaka matatu, moja la kuomba rushwa na mengine mawili ya kupokea rushwa.
Upande wa mashitaka ukiongozwa na Wakili Mabula Mapalala ulidai kuwa mtuhumiwa alitenda makosa hayo kati ya Machi 15 na 22 mwaka jana akiwa ni hakimu mkazi wa Wilaya ya Urambo.
Ilidaiwa kuwa Machi 15  mtuhumiwa akiwa ni hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Urambo, alimshawishi Lucas Raymond Changala ampe sh milioni tano ili ampe dhamana ndugu yake aliyekuwa anakabiliwa na kesi ya wizi wa fedha za benki ya NMB.
Mapalala alidai katika shitaka la pili, Machi mtuhumiwa alipokea sh milioni moja kutoka kwa Changala kama malipo ya awali ili ampe dhamana Phillipo Raymond aliyekuwa mtumishi wa benki ya NMB  anayetuhumiwa kuiba zaidi ya sh. milioni 100.
Katika shitaka la tatu, mwanasheria huyo wa Takukuru alidai  kuwa Machi 21 mtuhumiwa huyo alipokea tena sh. milioni moja ikiwa ni muendelezo wa malipo aliyoomba ili ampe dhamana mtumishi huyo wa NMB.
Upande wa mashitaka uliiomba mahakama impatie adhabu kali mtuhumiwa ili iwe fundisho kwakuwa wananchi wamekuwa wakilalamikia vitendo vya rushwa hasa vinavyofanywa na watumishi wa umma.
Akijitetea, Bulugu aliiomba mahakama isimpatie adhabu kubwa kwa vile ni kosa la kwanza na anategemewa na zaidi ya watu 10 ikiwemo wazazi wake.
Baada ya utetezi huo, hakimu aliyesikiliza shauri hilo, alimhukumu kulipa faini ya shilingi laki tano kwa kila kosa au kutumikia kifungo cha miaka mitatu kwa kila kosa na adhabu hiyo ya kifungo itakwenda pamoja.

0 comments: