LATEST POSTS

Tuesday, December 17, 2013

FAMILIA 30 ZAKOSA MAKAZI



mafuriko

ZAIDI ya familia 30 za wakazi wa kijiji cha Kasense nje kidogo ya Manispaa ya Sumbawanga, wamekosa pahala kuishi baada ya nyumba zao kubomolewa na nyingine kuezuliwa mapaa kutokana na mvua kubwa iliyoambatana na upepo kunyesha.
Mvua hiyo iliyonyesha juzi kuanzia saa 9 alasiri na ilidumu kwa saa mbili huku upepo huo ukiangusha miti na kuwatia hofu wakazi wa kijiji hicho.
Diwani wa Kasense, Cretus Jumbe, alisema mvua hiyo pia iliharibu madarasa matatu na nyumba mbili za walimu katika shule ya Msingi Kasense ambazo nazo ziliangukiwa na miti kwenye mapaa yake.
Jumbe alisema hadi sasa kuna takriban nyumba 32 zilizopata madhara hayo ambapo familia zote zimehifadhiwa kwa ndugu na jamaa zao wakisubiri msaada zaidi toka serikalini.
Mkururugezni wa Manispaa ya Sumbawanga, William Shimwela, ambaye alifika eneo hilo muda mfupi baada ya maafa hayo, alisema timu ya wataalamu inatarajiwa kufika leo kufanya tathmini ya maafa na kuangalia ni msaada upi wa haraka unatakiwa.
“Tutakaa na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa ambaye ni Mkuu wa wilaya ili kuona hatua zingine zinazofuata kwani tayari tumejionea hali halisi ya wananchi walivyoathirika kutokana na tukio hilo na wanahitaji msaada wa haraka kwa sababu hawana sehemu za kuishi,” alisema Shimwela.
Alisema madarasa yaliyoharibika yanahitaji ukarabati kabla ya Januari mwakani, ili wanafunzi waweze kuendelea na masomo.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: