LATEST POSTS

Monday, January 6, 2014

SHAABAN ROBERT; Bingwa wa lugha na elimu- atuzwa London

Tanzania na Afrika zina mashujaa wengi. Baadhi yao hawatajulikana kwa sababu habari zao hazikutangazwa. Walitenda mema wakaondoka zao. Wengine tunao humu mitaani na vijijini, wanafanya mazuri kimya kimya.
Shaaban Robert alizaliwa mwanzoni mwa karne ya 20 akafariki Juni 1962, muda mfupi baada ya Tanganyika kupata uhuru, akiwa na miaka 53 tu.
Kazi zake zilitumika kukuza Kiswahili. Nikiwa shule ya msingi, tulikariri mashairi yake; hadi leo sijasahau Utenzi wa Haki. Ubeti wa 50 unazungumzia tabia:
“Usishiriki uongo.
Ijara upate hongo.
Mtu mwongo ni msungo.
Masuto mengi hupewa.”
Kikubwa ndani ya maandishi lukuki ya marehemu Shaaban Robert ni lugha na ujumbe. Miaka zaidi ya 75 tangu alipoandika kazi zake, bado inakuhitaji uchimbe sana ili kujua maana ya anachokisema, jambo linalokusaidia msomaji kujenga umahiri na msamiati wa Kiswahili .
Hapo juu ijara ni malipo, mshahara au kipato. ‘Msungo’ ni mtu asiyepewa malezi ya kutosha, kimila. Aliandika pia makala akiwa mwanasafu wa Gazeti la Mambo Leo, kisha akatoa mkusanyiko wa ‘Maisha Yangu Baada ya Miaka Hamsini’-Kitabu hiki kiliandikiwa utangulizi na aliyekuwa Waziri wa Elimu mwaka 1966, S. Eliufoo.
Mwaka 1991 Mkuki na Nyota chini ya mchapishaji mkongwe Walter Bgoya, ilitoa vitabu hivi tena. Tuna bahati sana kuwa na Walter Bgoya. Kazi anayoifanya kuendeleza vitabu, inafaa kuigwa na kufuatwa hasa na wafanyabiashara na viongozi wetu.
Ingawa Shaaban Robert anaelezea mambo yake ya binafsi- ndoa, wanawe na kazi, kitabu kinatathmini umaana wa kuishi, wajibu wetu katika jamii na masuala ya mapenzi kwa kina.
Mathalan, shuhudia binti yake alipofaulu darasa la nne kwenda la tano. Enzi hizo za ukoloni (kisa kilitokea 1945), haikuwa kawaida wanawake kusoma. Hivyo baba mtu anaomba ahamishwe kazi toka Mpwapwa kurudi Tanga kulikokuwa na shule.

Anasema, “Mtoto yeyote anyimwaye makusudi ya kusoma, kuandika na hesabu ana haki ya kuwalaumu wazazi wake katika maisha yake atakapojiona kuwa amefungiwa milango yote ya kusitawi baadaye.”
Mbali na kumwongelea binti, anamsifia mama yake ambaye hakupata elimu lakini akahakikisha yeye Shaaban anasoma. “Deni lake kwangu la wema alionitendea halilipiki kabisa.”
Mbali ya elimu anazungumzia ubaguzi wa rangi, unyanyasaji kazini na wajibu wa mwandishi. Huu ulikuwa wakati wa vita vikuu vya dunia. Anasema alikuwa mtu pekee, Afrika Mashariki, aliyeandika mashairi kupinga wauaji wa Kinazi chini ya Dikteta Adolf Hitler. Alipoulizwa vipi anafanya “kazi ya bure,” Akasisitiza haikuwa bure.
“Nilikuwa nikiandika habari ya tukio kubwa lililotokea katika dunia wakati wa karne ya maisha yangu.” Anazungumzia pia suala hilo hilo la kuwajibika kipindi Mwalimu Nyerere na TANU wakipigania uhuru wa nchi. Ilikuwa hatari hata kwenda mikutanoni. Lakini marehemu alihudhuria. Alipenda msimamo wa Nyerere na TANU. Anasema watu wa madhehebu na kabila mbalimbali waliungana “chini ya mtu huyu”. Yaani Nyerere.
Siyo ajabu akaunganisha jina lake la Kiislamu (Shaaban) na Kikristo (Roberts), kuunga mkono kauli ya umoja Tanzania. Leo wangapi wenye msimamo wa aina hii? Shaaban Robert alijali yaliyoendelea, si tu kitaaluma (kuandika) au kisiasa, bali akiwa na wenzake, kazini.
“Mapatano na amani kati ya watu yalikuwa ni mambo mawili ambayo niliyapenda na niliyoyafikiri kuwa ni muhimu katika maisha. Ndege wa manyoya hupatana katika kiota chao kidogo; ni aibu kubwa wanadamu hukosana katika nafasi pana.”
Shaaban Robert ni mmoja wa mashujaa wakubwa sana Afrika na ukweli hatujamheshimu ipasavyo. Ndiyo. Zipo barabara na shule zinazotumia jina lake. Lakini je, tumehifadhi na kuzitangazaje kazi zake? Je, kweli sisi tunaheshimu mashujaa? Je, kwa nini mashujaa ni watu muhimu? Tuangalie mifano miwili.
Takriban wanasiasa wote duniani hufuata kanuni zilizoandikwa na mwandishi wa Kiitaliano, Nicollo Machiavelli, aliyefariki mwaka 1527 akiwa na miaka 58. Aliandika ‘The Prince’ (Mwana wa Mfalme), kinachotoa mwongozo wa namna ya kuwatawala na kuwaongoza watu. Swali kuu linaloulizwa ni je, kiongozi anatakiwa apendwe au aogopwe? Machiavelli anadai yote mawili ; ila bora kuogopwa kuliko kupendwa, ili kutimiza malengo. Kimetafsiriwa takriban lugha zote kubwa duniani. Nadharia za Machiavelli zinafuatwa na wanasiasa na vile vile kampuni kubwa kama Google, Facebook, wanamuziki wa Rap, 50 Cent na marehemu Tupac aliyekitungia kitabu wimbo.
Ingawa ‘The Prince’ ilichapwa 1532 (miaka mitatu baada ya mwandishi kufariki) leo ukienda alikozaliwa, Florence, bado nyumba aliyoishi hata nakala ya kitabu alichoandika mwanzo kwa mkono imehifadhiwa. Miaka mingapi imepita? Piga hesabu msomaji. Lazima ulipie fedha kuingia ndani. Fedha inakwenda’api? Kwa familia yake na Idara ya Utamaduni. Mbali na maandishi, utatembezwa katika mashamba ya mizaituni, kunywa mvinyo maarufu, misitu mizuri na kuelezwa historia ya Italia miaka 500 iliyopita. Sasa fikiria hilo lingefanywa kuhusu Shaaban Robert- kama sehemu ya utalii na hazina kitaifa! Mwingine. Nimewahi kuingia jumba aliloishi mchoraji maarufu Van Gogh wa Uholanzi aliyejiua mwaka 1890 akiwa mwenda wazimu na umri wa miaka 37.
Leo ukifika mjini Amsterdam kuna jumba la makumbusho, mgahawa na mambo kibao yanayolipiwa fedha kutukuza kazi zake zinazopendwa ulimwengu mzima. Van Gogh ni fahari ya Waholanzi.
Majuma matatu yaliyopita kampuni mpya ya “New Deal Africa” chini ya uongozi wa mwanahabari Ayoub Mzee na mwenzake Enzy Larusai ilifanya tafrija ya kuwapa Watanzania mbalimbali wakazi wa Ughaibuni tuzo. Kati yao walikuwa Aseri Kitanga (anayeleta kompyuta kwa watoto Afrika), Dk Hamza Hassan na Mariam Kilumanga, kiongozi wa Chama cha Wanawake Uingereza.
Amina Waziri, mjukuu wake Shaaban Robert alipokea “Tanzania Achievement Award 2013,” kwa niaba ya babu- kwa kuendeleza elimu na lugha. Hii siyo zawadi za kwanza. Akiwa hai, Ustaadh alipewa tuzo ya MBE (Member of British Empire) na Margaret Wrong Memorial Prize na Waingereza waliomheshimu sana.

Mjukuu mwingine Aisha, alinieleza namna babu yake alivyokuwa muda mfupi kabla ya mauti. Mrefu, mcheshi, mtanashati, aliyependa sana watoto, vitabu na mpangilio wa vitu. “Aliweka chupa zake za wino kando ya vitabu, si unajua enzi hizo kalamu zilikuwa za kuchovya? Sasa ole wako uumwage ule wino!”
Wajukuu hawa wawili wanasema babu yao alipenda sana watu na familia yake. Haya jamani, tujivunie na kuwapamba mashujaa wetu.
 Chanzo: Mwananchi

0 comments: