LATEST POSTS

Friday, January 24, 2014

Uteuzi wa Kikwete waikoroga CCM


Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye akizungumza Dar es Salaam jana kuwataka mawaziri walioteuliwa kuendelea na nyadhifa zao kubadilika ili kuleta imani kwa wananchi. Picha na Fidelis Felix 

Dar es Salaam. Uamuzi wa Rais Jakaya Kikwete kuwaacha katika Baraza la Mawaziri, mawaziri wote waliotajwa na CCM kuwa wameshindwa kutekeleza majukumu yao umekichanganya chama hicho, baada ya jana kusema kuwa hakitasita kuchukua hatua kali dhidi ya mawaziri hao na wengine, iwapo watashindwa kurekebisha upungufu wa kiutendaji unaozikabili wizara zao.
Chama hicho kilitoa ufafanuzi huo jana ikiwa zimepita siku tano tangu Rais Kikwete alipofanya mabadiliko katika baraza hilo na kuwaacha mawaziri saba waliohojiwa na CCM wakidaiwa ni ‘mzigo’, baada ya utendaji wao wa kazi kulalamikiwa na wananchi pamoja na wabunge.
Desemba 14 mwaka jana CCM kupitia kikao chake cha Kamati Kuu iliwahoji mawaziri hao, kisha ikamtupia mpira Rais Kikwete kuamua hatima yao, huku kikifafanua kuwa “kilimshauri mambo matatu; ama kuwafukuza, kuwahamisha wizara au kuwahimiza wafanye kazi.”
Uamuzi huo ulikuja baada ya chama hicho kufanya ziara ya siku 26 iliyokuwa ikiongozwa na Katibu Mkuu wa chama hicho,  Abdulrahman Kinana, mwishoni mwa mwaka jana katika mikoa ya Ruvuma, Mbeya na Njombe na kukumbana na malalamiko ya wananchi kuhusu utendaji kazi mbovu wa wizara zinazosimamiwa na mawaziri hao.
Mawaziri walihojiwa na CCM na wamebakizwa katika Baraza la Mawaziri ni Dk Shukuru Kawambwa (Elimu), Christopher Chiza (Kilimo), Saada Mkuya (Fedha). Mkuya alihojiwa kwa niaba ya aliyekuwa Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa ambaye kwa sasa ni marehemu). Wengine ni Dk Abdallah Kigoda (Viwanda), Dk Mathayo David (Mifugo na Uvuvi), Celina Kombani (Utumishi wa Umma) na Hawa Ghasia (Tamisemi).
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye alisema;
 “CCM hakitasita kuchukua hatua kali dhidi ya mawaziri na watendaji wengine watakaoshindwa kurekebisha upungufu unaopigiwa kelele. Kushindwa kwao kutimiza majukumu yao ni hujuma kwa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, hivyo chama hakiwezi kuvumilia usaliti huo.”
Alisema CCM kuendelea kuwafumbia macho watu wasiopenda kuwajibika ni sawa na kujinyonga chenyewe, kusisitiza kuwa chama kitaendelea na utaratibu wa kuwahoji watendaji wa Serikali na wasiotaka kuhojiwa wajiondoe serikalini au watafute kazi nyingine za kufanya. “Wanalipwa mshahara kwa kodi za Watanzania lazima wakubali kuhojiwa, CCM katika hili tutakuwa wakali zaidi. Tunaungana na wabunge wa CCM na wananchi kuhusu maoni ya utendaji kazi wa mawaziri hao, malalamiko yao ndiyo yalizaa neno mawaziri ‘mzigo” alisema.
  Nape alisema chama hicho kitatumia wingi wa wabunge na madiwani wake kuisimamia Serikali na usimamizi huo kuanzia sasa utaimarishwa zaidi katika ngazi zote, “Tutaisifu Serikali ikifanya vizuri na tutaikosoa na kuishutumu ikifanya vibaya.
“Uwajibikaji wa kweli ndiyo msingi wa mafanikio na maendeleo ya nchi yetu. Tuna matumaini mawaziri hawatayaangusha matumaini ya wananchi kwa Serikali yao. Kuteuliwa kwao upya au kuachwa kwenye Baraza la Mawaziri hakufuti upungufu wao uliotokea siku za nyuma.”
Alisema ziara za chama hicho pamoja na utaratibu wa kuwahoji watendaji wa Serikali umekuwa na mafanikio makubwa. Sasa urasimu uliokuwapo awali katika ununuzi wa pamba, korosho, msongamano wa magari katika mpaka wa Tanzania na Zambia (Tunduma) na upatikanaji wa mbolea umemalizika. “Tunaongeza ukali maana muda wa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya chama ni mdogo,  tukicheka na wasiopenda kuwajibika wananchi watatuadhibu. Hatuko tayari kuadhibiwa kwani tumetoa ahadi kwa Watanzania ni lazima tuzitekeleze,” alisema Nape.
Huku akiwataka Watanzania wawape muda mawaziri hao, Nape alisisitiza: “Kama mambo yasipoenda wananchi waseme na CCM itaungana nao kupiga kelele na kuhakikisha hatua zinachukuliwa.  Ndiyo maana hata wakuu wa mikoa na wilaya nao wanahojiwa na kutoa ufafanuzi katika masuala mbalimbali.”

Alipoulizwa kama CCM itaendelea kuwavumilia Dk Kawambwa na Chiza, Nape alisema, “Wamerudishwa, ila tunatumaini upungufu wameuona, wakishindwa CCM haitakaa kimya. Ila wananchi wanatakiwa kutambua kuwa kumfukuza waziri siyo suluhisho.”
Akitoa mfano, Nape alisema CCM haiwezi kuendelea kuvumilia kuona vinachapishwa vitabu vya shule za msingi na Sekondari vyenye makosa.
“Mabwana shamba wiki nzima wanavaa suti badala ya kwenda shambani. Angalia bosi wao anafanyaje (Chiza). Haiwezekani kwa muda wa miaka minne na nusu Waziri Chiza hajakwenda kutembelea ghala la taifa la chakula lililopo mkoani Ruvuma, nasema hivi, ukitaka usinyooshewe kidole kaa nyumbani kwako.”
Vilevile alizungumzia jinsi mawaziri wanavyofanya sherehe baada ya kuteuliwa, “Watu wanadhani kuteuliwa ni ulaji,  vijana wa nchi hii wabebe vita hii. Hivi sasa tukihesabu safari za mawaziri kwenda nje ya nchi na kuwatembelea wananchi, zipi zitakuwa nyingi?” alihoji.
Kuhusu madeni ya walimu, alieleza kushangaa kwa nini yanaongezeka kila mwaka na kuhoji iweje Serikali imefikia hatua ya kuwakopa wananchi badala la wananchi kuikopa Serikali.” Nape aliponda utaratibu wa watendaji wa Serikali kufanya vikao kila siku na kushindwa kuwahudumia wananchi, huku akisisitiza kuwa azimio la Sekretarieti ya CCM ni kuhakikisha kuwa chama hicho kinakuwa karibu na wananchi, kusikiliza changamoto zao na kuwasemea wanyonge.

Chanzo: Mwananchi

0 comments: