LATEST POSTS

Friday, January 24, 2014

USHAURI KWA MAMA WEMA

NIANZE kwa kumuomba radhi sana mama mzazi wa msanii mwenye jina kubwa Bongo, Wema Abraham Sepetu, aitwaye Mariam Sepetu. Ninafanya hivi kwa sababu ya jadi yetu waafrika, kwamba huwa siyo jambo la heshima, mwenye umri mdogo, kumweleza maneno ya ‘kuudhi’ mtu aliyemzidi umri.

Wema Abraham Sepetu.
 Lakini inabidi nimweleze kidogo maneno ambayo ingawa siyo mabaya, nina uhakika hata hivyo, hatayapenda kwa sababu nyingi, mojawapo ikiwa ni kuingilia uhuru katika malezi ya watoto wake.
Mama huyu anaingia katika orodha ya wazazi wachache ambao wametumia majina ya watoto wao waliojipatia umaarufu kutokana na kazi zao mbalimbali, ziwe mbaya au nzuri, nao kujikuta wanajulikana.
Wengine wa aina yake ni pamoja na mama mzazi wa marehemu Steven Kanumba, aitwaye Flora Mtegoa, mama mzazi wa Elizabeth Michael ‘Lulu’, Lucresia Kalugira na hata mama yake msanii wa Bongo Fleva, Diamond, Sanura Kassim ambaye amekwenda mbali zaidi kiasi cha kupata hadi a.k.a. Sandra.
Hawa tumewafahamu kwa sababu mbalimbali, lakini hasa zaidi ni skendo za watoto wao. Tunao vijana wengi wenye vipaji ambao wamekuwa maarufu kwelikweli, lakini kwa bahati mbaya sana, hatujaweza kuwafahamu wazazi wao kwa namna walivyo hawa. Tunaweza kuwa tunawajua kwa sababu tunafahamiana nao wenyewe, au na watoto wao, lakini hatuwaoni katika magazeti, redio wala televisheni.

 
Kuna jambo moja ambalo siliungi mkono kutoka kwa mama Wema. Jinsi anavyomlea mwanaye mbele ya jamii ya Watanzania. Anamlea kimatangazo, kizamani na tena kwa kusahau kabisa tabia, hulka na mienendo ya wazazi wa kibantu, hasa wanapozungumzia maisha binafsi ya watoto nje ya nyumba za wazazi wao.
Kimatangazo kwa sababu jambo la kukaa na mwanaye na kulizungumza, anakimbilia magazeti. Hata kama waandishi wanamfuata na kumuuliza kuhusu chochote, si busara kutoa maelekezo kwa kijana wako kupitia vyombo vya habari. Hapa inaonyesha uwepo wa tatizo, tena kubwa katika familia.
Labda ni kwa kuwa anajua mtoto wake ni staa, kwa hiyo ni sahihi kusema naye kupitia magazeti. Kama hivyo ndivyo anavyoamini, basi ni vizuri nimshauri kwamba mzazi aliye makini, hawezi kutoa maoni juu ya mtoto wake, hasa mwenye skendo za mara kwa mara kama Wema kupitia vyombo vya habari. Amekuwa akiongea mambo mengi kumhusu mwanaye.
Ana malezi ya kizamani kwa sababu amegoma kwenda na wakati. Huu si wakati wa kumchagulia mtoto wa kike mtu anayedhani anaweza kuwa mume wa maisha yake. Kila siku anazungumza kupitia magazeti jinsi gani hampendi Diamond na kwamba hayuko tayari kuona mwanaye akiolewa naye.
Ni sawa, huenda anazo sababu za msingi za kusema hivyo, lakini kwani ni lazima apige mayowe? Kuna tatizo gani kumwita mwanaye na kumweleza sababu hasa za kumkataa mpenzi wake?
Huu si wakati wa wazazi kuamua mtoto aolewe au amuoe nani, bali ni muda wa kujadiliana kwa kila mmoja kutoa hoja na mwisho wa siku, mtoto anatakiwa apewe nafasi kubwa kwa sababu maisha anayokwenda kuishi ni ya kwake, siyo ya wazazi!
Siku zote tumekua kwa kuamini kuwa wazazi ni wenye hekima na busara, vitu ambavyo nahisi kama ninavikosa kwa mama yangu huyu. Vinginevyo, angemwita binti yake na kumuuliza kisa cha kumng’ang’ania mpenzi wake huyo. Huenda Wema anayo sababu ya msingi ya kutaka kuwa na Diamond.
Na hata yeye mama, huenda anazo sababu nzuri kabisa za kumkataa Diamond, angekaa chini na mwanaye na kumweleza kimya kimya, kuliko kama anavyofanya kutufaidisha. Hivi Wema akiwa ‘kauzu’ kama anavyoonekana, na ikatokea anafunga ndoa na mkali wa Number One, mama atafanyaje? Atasubiri binti apate laana? kwa lipi, mume wake amchagulie mama!!
Na labda huu uwe pia ujumbe kwa wazazi wangu wengine, popote walipo, watoto wanapenda kusikiliza ushauri wenu kwa sababu siku zote ni wenye busara, lakini pia ni vyema mkatoa nafasi kwao wapate kusikika na mheshimu mawazo yao!

Chanzo: GPL

0 comments: