LATEST POSTS

Friday, February 21, 2014

UZINDUZI WA FILAMU ZA SWAHILIWOOD ULIOFANYIKA CENTURY CINEMAX -OYSTERBAY JANA



wadau mbalimbali




Wadau wa filamu

Media For Development International (MFDI) – Tanzania usiku wa jana wamefanya uzinduzi wa aina yake katika sekta ya filamu Tanzania kwa kuzindua filamu tatu kupitia mradi wake wa Swahiliwood katika Ukumbi wa Century Cinemax uliopo Oysterbay, jijini Dar es salaam.
Uzinduzi huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya filamu hapa nchini pamoja na mashirika ya ya ndani na nje ya nchi ikiwa ni hatua ya kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya filamu hapa nchini.
Filamu zilizozinduliwa jana zikiwa na lengo la kuelimisha jamii ni Mdundiko iliyotengenezwa na Timothy Conrad, Sunshine iliyotengenezwa na Karabani na Network iliyotengenezwa na John Kallage.
Mradi wa Swahiliwood umewezeshwa kwa msaada wa Watu wa Marekani kupitia USAID kwa kushirikiana na Johns Hopkins University Center for Communication Programs pamoja na kampuni ya Proin Promotion inayokuwa kwa kasi katika usambazaji wa kazi za filamu nchini Tanzania.
Lengo la Swahiliwood ni kuongeza nguvu ya ubunifu kwa vijana watengeneza filamu wa Kitanzania, ili kupeleka maudhui kwa walengwa kwa njia ya burudani kwa kushirikiana na sekta binafsi kuhakikisha filamu zinawafikia walengwa mbalimbali kupitia mitandao ya wasambazaji. Mradi huu unafanya kazi pamoja kwa kushirikiana na wadau muhimu kutoka sekta ya umma pamoja na COSOTA (Chama cha haki miliki), Mamlaka ya mapato Tanzania, bodi ya filamu na BASATA, kama idara inayosimamia maendeleo ya Tasnia vya filamu.
Akizungumza wakati wa uzinduzi John Riber, mkurugenzi MFDI Tanzania alisema kwamba “Tulizindua mradi wa Swahiliwood kwa sababu tuliona kwamba vijana wana uwezo mkubwa wa kutengeneza filamu. Muundo wa Swahiliwood unazingatia nguvu ya vijana katika kuhakikisha tasnia ya filamu inasambaa ikielimisha jamii juu ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi. Na hiyo imetambuliwa na Serikali ya Tanzania kama ni changamoto kuu ambayo inalikabili Taifa”.
Muundo wa Swahiliwood unatoa mafunzo na ushauri kwenye uzalishaji wa filamu. Pia ni sekta ambayo inaongoza kwa kutoa ajira kwa vijana wa Tanzania. Serikali ya Tanzania na sekta binafsi pamoja na Watanzania wabunifu wenye vipaji vya utengenezaji wa filamu wameshirikiana, kwa msaada wa Serikali ya Marekani. Wamekuwa nyenzo katika kukuza biashara na uchumi unaokuwa haraka, na kuhakikisha kwamba filamu zinawafikia watazamaji wa Afrika ya Mashariki kwa ujumla.
MDUNDIKO: Ni hadithi ambayo inazungumzia mfarakano wa imani za kimila, maadili, na hoja za maisha katika jamii.
NETWORK: Ni hadithi inayohusu kuwindwa kwa mhalifu anae tuhumiwa kufanya mauaji ya mwendelezo ambayo yanawahusisha wapelelezi, askari mzee na kijana mwenye mvuto.
SUNSHINE: Ni hadithi ya uraiani yenye mguso kuhusu majaribu ya uhalifu na mapenzi yasiyokuwa na mashariti kati ya mama na mtoto.

0 comments: