LATEST POSTS

Thursday, March 27, 2014

Watanzania wafanyishwa ukahaba China

WIZARA ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, imebaini kuwepo mtandao wa wanaosafirisha wasichana wenye umri mdogo kutoka nchini na kuwapeleka China kisha kuwafanyisha vitendo vya ukahaba pasipo ridhaa yao.
Hayo yalisemwa jijini Dar es Salaam jana na Waziri wa Wizara hiyo, Bernard Membe, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na masuala mbalimbali yanayohusu wizara yake.
Alisema mtandao huo ukishasafirisha wasichana hao na kuwafikisha China, huwanyang'anya hati zao za kusafiria na kujikuta wakishindwa kurejea nyumbani, hali inayowalazimisha kujikuta wakitumbukia kwenye biashara hiyo.
Membe alisema, taarifa ambazo wizara yake inazo ni kwamba, tayari mmoja wa wasichana hao amefariki kwa kuuawa. Alisema mwezi uliopita walialikwa kwenda nchini China, ambapo walibaini kuwepo kwa vitendo hivyo vya kusafirisha wasichana kutoka Tanzania na kuwapeleka nchini humo ili kuwafanyisha ukahaba.
"Inaelekea kuna Watanzania wanaokwenda nchini China kwa kutumia nyaraka bandi, huku wengine wakitumia paspoti ya nchi zingine wakati wao ni Watanzania ili kusafiri nje ya nchi kwa lengo la kufanya biashara ambazo ni haramu," alisema Membe.
Alisema kutoka na kukithiri kwa hali hiyo, Rais Jakaya Kikwete, atakuwa na ziara ya kutembelea nchi hiyo ambapo pamoja na mambo mengine ataenda kujionea hali halisi ya kuwepo kwa vitendo hivyo.
Kwa mujibu wa Waziri Membe, zaidi ya Watanzania milioni 3 wanaishi nje ya nchi, lakini baadhi yao wapo wanaofanya ukabaha, biashara za dawa za kulevya na ugaidi. "Kufanya vitendo hivyo ni kuivunjia heshima nchi yetu," alisema na kuwataka Watanzania wasirubuniwe kwenda nje ya nchi kwa kudhani kuwa maisha ya huko ni rahisi.
Aliwataka wenye mitandao ya kuendesha madanguro ya ukahaba nje kwa kutumia wasichana wa Kitanzania wajue kwamba kufanya hivyo ni kosa la jinai. Aliwataka Watanzania wanaoishi huko waishi kwa kufuata misingi ya nchi na taratibu husika ili kulinda heshima ya nchi.

0 comments: