LATEST POSTS

Friday, April 4, 2014

Isipotumika busara, Bunge EAC litasambaratika

Kwa muda mrefu sasa, Bunge la Afrika Mashariki limekuwa katika mizozo isiyoisha kiasi cha wananchi wengi katika nchi wanachama kuhofia kwamba Bunge hilo linaweza kusambaratika. Tulishuhudia miezi michache iliyopita mzozo mkubwa ukiibuka, ambapo wabunge kutoka katika baadhi ya nchi wanachama walisusia vikao wakipinga vikao hivyo kufanyika katika makao makuu ya jumuiya hiyo pekee yaliyopo jijini Arusha, Tanzania.
Hata hivyo kwa busara za wakuu wa nchi wanachama na uongozi wa Bunge hilo wakati huo, mzozo huo ulimalizika kwa kuboresha kanuni husika na kuweka utaratibu wa kuwezesha vikao hivyo kufanyika kwa mzunguko katika kila nchi mwanachama. Pamoja na kumalizika kwa mgogoro huo pasipo madhara makubwa kisiasa na kiuchumi, sasa umejitokeza mgogoro ambao wananchi wengi wa nchi wanachama wanahofu kwamba utalisambaratisha Bunge hilo.
Wengi wa wabunge wamesema hawana imani na Spika, Dk Margareth Zziwa na wanataka ang’oke kwa madai kwamba ameshindwa kutimiza wajibu wake kwa mujibu wa Kanuni za Bunge. Tofauti na ilivyokuwa katika migogoro iliyotangulia, mgogoro huu hauna dalili au hisia zozote za utaifa. Wabunge wanaompinga Spika na kutaka aondolewe siyo tu ni zaidi ya theluthi mbili ya wabunge kama Kanuni zinavyoelekeza, bali pia wanatoka katika nchi zote wanachama, ikiwamo nchi yake ya Uganda. Pia hoja ya kumng’oa madarakani haina harufu yoyote ya ubaguzi wa kijinsia kwa sababu wabunge wengi wanawake ndio wako mstari wa mbele kutaka kiongozi huyo aachie madaraka.
Inasemekana kwamba Serikali ya Uganda nayo imeridhia Spika huyo ang’olewe kutokana na sababu mbili kubwa. Kwanza, ni madai kwamba Spika huyo hakuwa chaguo la chama tawala cha NRM ingawa ni mwanachama wake. Pili, ni ukweli kwamba sasa ni zamu ya Uganda kutoa Spika, hivyo hata kama Spika Margareth Zziwa aking’olewa atakayechaguliwa lazima atokane na wabunge kutoka katika nchi hiyo. Pamoja na hali hiyo, mzozo huo unakuzwa na utata unaotokana na Kanuni ya 9 ya Bunge hilo inayoeleza utaratibu wa kumwondoa Spika madarakani iwapo itatokea haja ya kufanya hivyo.
Kwa vyovyote vile, hali hiyo haiashirii vyema hali ya baadaye ya Bunge hilo, hasa kutokana na ukweli kwamba Spika huyo sasa ameahirisha Bunge kwa muda usiojulikana kutokana na mvutano kati ya wabunge wanaomuunga mkono na wale wanaotaka aachie madaraka. Mpaka anachukua hatua hiyo, wabunge 33 kati ya 45 walikuwa wametia saini tamko la kutaka ang’oke, lakini akatumia Kanuni ya 82(2) kuahirisha Bunge, ambalo lilipangwa kumaliza shughuli zake hapo kesho.
Wapinzani wa Spika Zziwa wanamtuhumu kwa mambo mengi, yakiwamo madai ya: Kuendesha Bunge kwa ubabe; kuwagawa wabunge; kiburi; kuchukulia mambo kirahisi; na kuchelewa mara kwa mara katika vikao vya Bunge. Tuhuma nyingine ni: Kuonyesha dharau kwa wabunge; na Matumizi mabaya ya fedha. Hoja ya kumng’oa Spika Zziwa ilianza kuzungumzwa kwenye vyombo vya habari vya Afrika Mashariki kwa wiki kadhaa sasa kabla ya Mbunge Peter Mathuki kutoka Kenya kuiwasilisha bungeni.
Sisi tunasema mzozo huo unahitaji kutatuliwa kwa busara, vinginevyo Bunge litasambaratika na kuirudisha Jumuiya ya Afrika Mashariki katika zama za kiza. Maoni yetu ni kwamba Spika ataonyesha ustaarabu kwa kuheshimu uamuzi wa wabunge walio wengi ambao wanataka aachie madaraka.

0 comments: