LATEST POSTS

Friday, May 9, 2014

BREAKING NEWS MAHABUSU AVUA NGUO HUKU AKISHIKILIA MLINGOTI WA BENDERA AKISHINIKIZA KESI YAKE KUSIKILIZWA.....MAHAKAMANI










MAHABUSU wawili kati ya sita wanaotuhumiwa kwa kesi za mauaji, wameleta kizaazaa baada ya kujaribu kutoroka na kukimbilia kwenye mlingoti wa Bendera ya Taifa nakuing’ang’ania kisha kuvua nguo na mmoja wao kubaki mtupu.
Tukio hilo limetokea leo majira ya saa 4:00 asubuhi katika Mahakama ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza, wakati mahabusu hao walipofikishwa kwa ajili ya kusikilizwa kwa kesi zao, lakini ghafla walipofika kwenye viwanja vya mahakama hiyo walitimua mbiyo kuelekea kwenye mlingoti wa Bendera hiyo ya Taifa na kuvua nguo.
Wananchi waliokuwa katika viwanja vya mahakamani hapo waliachwa midomo wazi na hali ya mshangao, mara baada ya mmoja kati ya hao wawili wakifanikiwa kuufikia mlingoti huo na kuvua nguo kisha kuanza kupiga kelele kwa kupaza sauti kudai haki itendeke.
 
Tukio hilo pia lilishuhudiwa na watumishi wa Mahakama ya Wilaya, Mahakama ya Mwanzo, Mamlaka ya Maji Safi na Majitaka ya jijini hapa (MWAUWASA), Askari wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), na taasisi zingine zilizo jirani na majengo ya mahakamani hapo na wananchi waliokuwa wakisubilia kesi zao kutajwa.
 
Mahabusu hao sita waliojaribu kutoroka na kuishia kudhibitiwa vyombo vya dola, walitajwa kwa majina kuwa ni Thobiasi Warioba (35), aliyeamua kuvua nguo zote na kubaki mtupu eneo la mlingoti wa Bendera ya Taifa, ambaye anakabiliwa na kesi ya mauaji Na. 32/2012.
 
Watuhumiwa wengine waliojaribu kutoroka ni Hamis Ramadani (30), AnthonyPetro (35), Marwa Mwita (38), na Chacha Wangwe (35), na mwingine ambaye hakufahamika majina yake mara moja, wote wanakabiliwa na kesi ya Jinai Na. 215/2013  na walikamatwa tangu mwaka 2011.
Wakiwa katika viwanja vya mahakama hiyo baada ya kudhibitiwa na askari polisi, mmoja wa mahabusu hao walisikika wakisema:
“Haiwezekani, tangu mwaka 2011 tulipokamatwa hadi sasa kesi zetu hazijasikilizwa. Wengine tumebambikiziwa kesi.  “Tunaomba haki zetu, polisi mnatuonea, vyombo vya habari tunaomba mtusaidie  tumekaa muda mrefu bila kusikilizwa na hatujui hatma yetu tangu 2011 tulipo kamatwa tumechoka kukaa mahabusu, tunaomba kesi zetu zisikilizwe”.
 
Baada ya malalamiko yao, ndipo askari  mmoja aliyejitambulisha kuwa ni Inspekta Henry akiwa na wenzake sita waliokuwa wakiwadhibiti wasikimbie na kuwahoji kuhusiana na madai yao, huku askari hao wakiwataka kuondoka katika mlingoti huo na kumtaka Warioba avae nguo ili waweze kuingia mahakamani.
 
“Pamoja na maamuzi yenu haya, lakini mtambue mnavunja sheria na hili ni kosa jingine la jinai, hivyo ni vema mkaondoka kwenye mlingoti huu na kuingia mahakamani. Malalamiko yenu tumeyasikia na yatashughulikiwa,” alisema Inspekta Henry.










0 comments: