LATEST POSTS

Thursday, January 9, 2014

CHADEMA yamfunga Zitto

John Mnyika
 Mhe. John Mnyika

SIKU moja baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kukubali pingamizi la Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kuizuia Kamati Kuu (CC) ya CHADEMA isimjadili hadi kesi yake ya msingi itakapokuwa imesikilizwa, chama hicho kimemfungia rasmi kushirikiana na wabunge wenzake katika shughuli za kisiasa.

Sambamba na hilo, chama hicho kimesema kuwa kuanzia sasa kinasahau mjadala kuhusu Mbunge huyo wa Kigoma na badala yake kinajikita kuchapa kazi kwa ajili ya malengo waliyojiwekea mwaka huu 2014.

Shughuli ambazo Zitto amefungiwa nazo ni pamoja na zile za nje na ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano, hususani zinazohusu kambi rasmi ya upinzani bungeni, inayoongozwa na CHADEMA.

Akizungumza na Tanzania Daima jana, Mkurugenzi wa Mawasiliano Habari na Uenezi, CHADEMA, John Mnyika, alisema uamuzi wa mahakama haujaelekeza kwamba Zitto apewe ushirikiano na chama chake, hivyo uamuzi wa CC wa kutoshirikiana naye uko pale pale.

Katika uamuzi wa CC uliosomwa na Katibu Mkuu, Dk. Willibrod Slaa, pamoja na kutangaza uamuzi wa kuwavua uanachama Samson Mwigamba na Dk. Kitila Mkumbo, alisema: “Kwa vile Zitto Zuberi Kabwe amekishitaki chama kinyume na matakwa ya katiba ya chama na kanuni zake, na kwa vile Mahakama Kuu imeamuru vikao vyote vya chama visijadili wala kuamua suala lolote linalohusu uanachama wa Zitto, viongozi wa ngazi zote za chama wanachama, washabiki na wapenzi wa CHADEMA popote walipo katika nchi yetu na nje ya Tanzania, wasishiriki wala kusaidia kwa namna yoyote mikutano yoyote ya nje au ndani au shughuli nyingine yoyote ya kisiasa itakayofanywa na Zitto na mawakala wake kwa jina la CHADEMA.”

Mnyika alisema Kamati Kuu ilishapitisha azimio la kumtenga Zitto na shughuli za siasa na kuwataka wanachama wao kote nchini, wasitoe ushirikiano kwa kazi au shughuli yoyote itakayofanywa na mbunge huyo.

“Uamuzi huo upo pale pale, na mahakama haijaelekeza kwamba apewe ushirikiano,” alisema Mnyika wakati akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu.

Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo, aliwataka wafuasi wa CHADEMA kutambua kuwa kilichoamriwa na mahakama ni pingamizi la awali tu kwani kesi ya msingi bado haijaanza kusikilizwa.

“Unajua kilichoamriwa ni pingamizi la awali. Huko ni sawa na kushangilia bao wakati mpira ndio kwanza umeanza na unaendelea. Mfano mzuri ni kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Simba na Yanga. Yanga walishangilia mabao matatu ya kipindi cha kwanza wakijua wameshinda, walipoingia kipindi cha pili unajua kilichotokea… Kwa hiyo kesi ya msingi bado, na hatuoni sababu ya kushangilia kwa sasa,” alisema.

Mnyika aliwataka wanachama wao kutambua kuwa CHADEMA iko imara na inaendelea na kazi zake kama kawaida, huku ikiwa na ajenda muhimu na mikakati mizito kwa ajili ya mwaka 2014.

Alizitaja baadhi ya ajenda ambazo wananchi wataanza kuzifanyia kazi kuwa ni pamoja na suala la katiba ambapo chama hicho kimepitisha maazimio sita mazito ya kuyafanyia kazi kuelekea mchakato wa katiba mpya na maandalizi ya mpango kazi wa mwaka 2014.

“Kamati Kuu iliyopita, mbali ya kushughulikia suala la wanachama wetu wasaliti, pia ilikuwa na mambo mengi ya kujadili. Kuna maazimio sita ya mchakato wa katiba mpya ambayo tutawaeleza, kuna suala la kupanda kwa bei ya umeme na maazimio yake. Watanzania wasubiri waone CHADEMA imeazimia nini katika suala la kupanda kwa gharama za umeme ambapo wameanza kuumizwa na ongezeko hilo,” alisema Mnyika.

Kwa msimamo huo wa kumfungia rasmi Zitto kushiriki shughuli za chama, ni wazi kuwa unazidi kumuweka njia panda Zitto  ambaye sasa atabaki kuwa mwanachama kwa nguvu ya mahakama hadi hapo itakapoamriwa vinginevyo.

Sasa Zitto ataungana na wabunge wenzake wawili, David Kafulila wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi) na Hamad Rashid Mohammed wa Wawi (CUF) ambao pia ubunge wao upo kwa nguvu ya mahakama.

Zitto alifungua kesi Mahakama Kuu siku moja kabla ya CC kuanza vikao vyake ambavyo vilikuwa vijadili utetezi wa tuhuma zake za kuendesha mkakati wa siri wa kusaliti chama, akiomba mahakama izuie suala la uanachama wake lisijadiliwe hadi kesi yake isikilizwe.

Akitoa uamuzi wa awali, Jaji John Utamwa, alisema kuwa mahakama imeridhia ombi la Zitto kuwa CHADEMA au chombo chochote kisijadili uanachama wake hadi kesi ya msingi itakapomalizika.

Katika kesi ya msingi, Zitto anaiomba mahakama ikizuie chama hicho kumchukulia hatua, ambapo kesi hiyo inatarajiwa kutajwa Februari 13, mwaka huu.

Zitto aliwasilisha maombi dhidi ya Baraza la Wadhamini la CHADEMA pamoja na Katibu Mkuu wa chama, Dk. Slaa, akiiomba mahakama itoe zuio la muda kwa Kamati Kuu kutojadili uanachama wake.

Katika kesi hiyo, Zitto ameiomba mahakama iizuie Kamati Kuu kujadili uanachama wake hadi rufaa yake itakaposikilizwa na Baraza Kuu la chama na kuomba mahakama imwamuru Dk. Slaa ampe nakala za taarifa za vikao vilivyomvua uongozi ili akate rufaa.

Katika hatua nyingine, Janeth Josiah anaripoti kuwa CHADEMA imemtaka Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova, kuacha propaganda za kisiasa na badala yake awakamate na kuwachukulia hatua za kisheria, waliohusika kumteka, kumtesa na kumuumiza mwenyekiti wa chama hicho Wilaya ya Temeke, Josephat Yona.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu wa CHADEMA, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Henry Kilewo, alisema kama Kamanda Kova amechoka kuwa mtumishi ndani ya jeshi hilo na kufanya siasa, atoke hadharani na kujitangaza.

“Tunamtaka Kamanda Kova atoke hadharani atangaze kuwa anatumikia chama gani cha siasa ili tukutane kwenye majukwaa ya siasa na siyo kwenye vyombo vyetu vya ulinzi na usalama,” alisema Kilewo.

Alisema polisi inapaswa kuyachukulia kwa uzito mkubwa na unaostahili matukio ya namna hii ambayo yanaanza kuota mzizi kwenye jamii.

Kilewo alisema  mwaka 2012/2013 yalitokea matukio yenye sura ya aina hiyo ya kutekwa na kuteswa kwa watu mbalimbali, wakiwamo wanaharakati, wanahabari na wanasiasa, lakini hakuna hatua zilizochukuliwa hadi sasa.

Alitoa mfano kuwa Jeshi la Polisi walimkamata kijana Evodius Justinian na wenzake, waliwatesa  vikali na kuwarubuni katika jitihada za kuwashinikiza wakiri kuwa viongozi wa CHADEMA ndio waliowatuma kutekeleza matukio ya uhalifu.

Alisema bado Watanzania wanataka kujua taarifa na hatua zilizochuliwa kisheria katika matukio ya kutekwa na kuteswa kwa Dk. Steven Ulimboka na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda.

Hata hivyo, alisema CHADEMA ipo mstari wa mbele kutetea haki za binadamu, kupinga ukatili, uhuni na vitendo kama hivyo na hakiwezi kumtuma mtu yeyote kufanya utekaji, utesaji au udhalilishaji.

Kwa mujibu wa Kova, uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa tukio la kutekwa kwa kiongozi huyo wa CHADEMA, lina uhusiano na ugomvi unaoendelea ndani ya chama hicho, hivyo ameunda tume ya wataalamu kuchunguza.

Yona alikutwa usiku wa juzi akiwa katika hali mbaya ya kujeruhiwa huko Ununio wilayani Kinondoni.
 
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: