LATEST POSTS

Saturday, January 25, 2014

Lady Jaydee; anastahili umalkia wa Bongo Fleva?


Jay Dee anatajwa kuwa msanii mwenye tuzo nyingi kuliko wasanii wengine wa kike kwani hadi sasa amenyakua tuzo mbalimbali ndani na nje ya nchi zinazofikia 26.  

Mpaka sasa panaweza kuwapo makundi mbalimbali yanayofikiri kwa mitazamo tofauti. Kuna wasiotaka kuamini mpaka leo hii mafanikio waliyofikia, wanajiuliza maswali pasipo kupata majibu.
Hata hivyo kuna wale ambao ni mashabiki wafuatiaji wa Bongo fleva hapa nchini ambao wanaweza kujibu vyema endapo wataulizwa swali la kupima bora wa msanii huyu wa kike anayeonekana kuwa na sifa zote za kuvalishwa heshima ya Malkia wa Bongo fleva.
Judith Wambura maarufu pia kwa jina la Komando, Binti machozi au Anaconda ndiye anayezungumziwa leo hasa kutokana na mafanikio yake katika tasnia ya muziki hata kudumu kwa muda mrefu kwenye ushindani wa soko la muziki huo.
Starehe imefanya uchunguzi na tathmini kuangalia, kulinganisha na kujiridhisha kwamba Lady Jay Dee anaweza kuwa ndiye Malkia wa Bongo Fleva akilinganishwa na wasanii wengine wote wa kike nchini katika muziki huo.
Tathimini ya Starehe imezingatia vigezo katika maeneo mbalimbali kupitia heshima yake kimuziki, kudumu kwake muda mrefu(ukongwe) na tuzo nyingi alizowahi kutunukiwa. Pia Lady Jay Dee kuwa msanii ndiye aliyeshirikishwa zaidi na wasanii wengine, kuwa na mafanikio ya kipato kikubwa na kufanya shoo kubwa za ndani na kimataifa. Sifa na vigezo hivyo vinaweza kukuachia swali hili; hivi Jay Dee hafai kutawazwa rasmi kuwa Malkia wa Bongo Fleva kwa sasa?. Hapana shaka jibu zuri unalo wewe mpenzi wa muziki na msomaji.
Tuzo alizochukua
Jay Dee anatajwa kuwa msanii mwenye tuzo nyingi kuliko wasanii wengine wa kike kwani hadi sasa amenyakua tuzo mbalimbali ndani na nje ya nchi zinazofikia 26. Mwaka mwaka 2000/01 alifanikiwa kupata tuzo ya mwanamziki bora wa kike katika Tuzo za M-NET, kabla ya  kutunukiwa tuzo tatu za Video Bora za Channel O maarufu kama ‘Channel O Music Video Awards’.
Tuzo hizo ni pamoja na ile ya Video Bora Afrika Mashariki kupitia albamu yake ya Machozi (mwaka 2003), na mwaka uliofuata wa 2005 pia wimbo huo ulishinda Tuzo ya Video Bora ambapo pia alipata Tuzo ya Video Bora ya Kushirkishwa kwa video iliyoitwa Makini Wanadamu, iliyochezwa na msanii Titi wa nchini  Uganda mwaka huo huo wa 2005.
Jaydee alipata pia tuzo ya Wimbo Bora wa Distance(mwaka 2004 hii ilikuwa ya BBC))
Mbali na tuzo hizo kuna nyingine tano alizofanikiwa kutunukiwa nchini Uganda moja ikitambulika kama ‘Pearl of Africa Music Awards’ ambapo Jay dee aliibuka Mwanamziki Bora wa Kike kwa mwaka 2006, 2007, 2008, 2010 na 2011.
Katika upande wa tuzo za Kilimanjaro hapa nchini, Jay Dee ametunukiwa tuzo 10 katika kipindi cha miaka 12 iliyopita. Baadhi ya tuzo ni pamoja na Tuzo ya Mwimbaji Bora wa Kike na Video ya mwaka(2002, 2009, 2010, 2011, 2012 na 2013.
Nyingine ni pamoja na Tuzo ya Albamu Bora kwa mwaka 2004, Mwimbaji Bora wa Kushirikishwa(2008), Wimbo Bora Afrika Mashariki(2011), akishirikishwa na mwanamuziki Kidumu kutoka nchini Burundi. Hadi sasa hakuna msanii wa kike nchini aliyefikia idadi hiyo ya tuzo.
Wasanii aliofanya nao ‘kolabo’
Kuna wanamuziki nyota wa nyumbani akiwemo Mr II, AY, Profesa Jay na wengine kadhaa waliofanikiwa  kushirikishwa katika nyimbo nyingi kuliko wasanii wengine.
Hata hivyo, Jay Dee ni kuwa mmoja kati ya wasanii watatu wanaoongoza kushirikishwa katika nyimbo za wasanii mbalimbali za wasanii wa ndani na nje. Baadhi ya nyimbo alizoshirikishwa kimataifa ni pamoja na wimbo Nitafanya wa msanii Kidumu wa Burundi,  Sirimba wa Ngoni kutoka Uganda,  Njalo na Wadubadubaza za Mina Nawe wa Afrika Kusini, Mimi ni mimi wa Oliver Mtukudzi wa Zimbabwe na Africa wa Salif Keita wa nchini Mali.
Kwa upande wa Bongo Jay dee ameshirikishwa katika zaidi ya nyimbo 50 na wasanii tofauti ambapo baadhi zikiwa Bongo Dar es Salaam wa Profesa Jay na  Machoni Kama Watu wa AY
Nyingine ni Mambo ya Fedha wa msanii Joseph mbilinyi (Mr Sugu), ambaye sasa ni mbunge, Mambo bado wa Chege, Nimpate Wapi wa Rich Longomba na Sikiliza wa marehemu Ngwair.
Hapo pia ni wazi kwamba hakuna msanii mwingine wa kike ambaye amefanikiwa kushirikishwa kama Lady Jay Dee.
Matamasha makubwa aliyofanya
Akizungumza na Starehe, meneja wa msanii huyo Gadna G Habash, anataja onyesho la kwanza na kubwa alilowahi kufanya Jay Dee kuwa ni pamoja na fainali za kumtafuta mshindi katika mashindano ya ubunifu ‘Kora All Africa Designers Competition’ ya mwaka 2001.
 “Yalifanyika Sun City, Afrika Kusini, kulikuwa na wasanii wakubwa aliyoshiriki nao kama vile Shaggy wa Marekani na Oliva Mutukuzi wa Zimbabwe, ikiwa ni tamasha lake kubwa la kwanza kushiriki,” anasema na kuongeza:
Tamasha lingine ni uzinduzi wa Tuzo za Kora lililofanyika nchini Benin mwaka 2007, ambapo pia alifanikiwa kukutana na wasanii wengine wakubwa kama vile P Squire.
Wenzake wanamzungumziaje?
Mbali na tathmini hiyo, mwanamuziki wa kike kutoka Kundi la Wakilisha,  Sara Kiasi maarufu kwa jina la Shaa anakiri kwamba Jay Dee anastahili sifa zote za kuitwa Malkia kutokana na jinsi alivyomfahamu. “JAY Dee alinishtua na kuniongezea ujasiri wa kuamini hata mimi ninaweza kufika mbali baada ya kuona video yake ya Machozi katika Kituo cha Channel O’, wakati huo nikiwa shule ya msingi,” anasema Shaa na kuongeza:
“Lakini mpaka sasa anaonekana kufanya vizuri zaidi tofauti na wasanii wengine wa kike alioanza nao, kwa hivyo nasema; ‘Mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Sista Jay Dee anastahili heshima hiyo.
Historia yake kimuziki
Binti huyu wa mzee Mbibo kutoka kijiji cha Manyamanyama, wilaya ya Bunda,  mkoani Mara, alianza muziki akiwa na umri wa miaka saba kupitia huduma za uimbaji wa kwaya katika Kanisa la Kisabato mkoani humo, kabla ya kumaliza elimu yake ya msingi katika miaka 1990.
Jay Dee alijiunga na huduma hiyo bila kujua kwamba leo angeweza kuwa mmoja kati ya nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini.
Juhudi zake kimuziki zilichangia kumjengea heshima katika medani hiyo tangu mwaka wa 2000 na hadi sasa amefanikiwa kuwa na kapu lenye albamu tano ambazo ni Machozi aliyoitoa mwaka 2000, Binti (2003), Moto (2005), Shukrani (2007), Best of Jaydee(2011) na Nothing But The Truth(2013). Rekodi hiyo ya kuwa na albamu tano pia haijafikiwa na msanii mwingine yoyote wa kike nchini.
Mafanikio yake
Albamu ya Machozi ilifanikiwa kumweka katika thamani ya kuwa msanii wa kwanza wa Bongo Fleva ikitajwa kutumia gharama kubwa kuiandaa katika historia ya muziki wa kizazi kipya nchini kwa wakati huo. Jay Dee kwa sasa anamiliki studio yake ijulikanayo kama Jag Records.
Pamoja na mengi aliyofanikiwa katika maisha kupitia muziki, kipimo chake  kwa sasa kimezua gumzo katika ukurasa wa wasanii wenye utajiri mkubwa baada ya kununua usafiri mpya wa gari la kifahari aina ya Range Rover Evoque..

 jide new ride


0 comments: