LATEST POSTS

Sunday, January 12, 2014

Usafiri treni Bara wasitishwa

KAMPUNI ya Reli Tanzania (TRL)

KAMPUNI ya Reli Tanzania (TRL), imesitisha kwa muda huduma ya usafiri wa treni kwenda mikoani.

Kusitishwa kwa usafiri huo unaotegemewa na Watanzania wengi nchini, kumetokana na kujaa maji katika stesheni za Godegode na Gulwe mkoani Dodoma na kuharibu tuta la reli.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kaimu  Mkurugenzi Mtendaji Mhandisi wa TRL, Paschal Mafikiri, alisema: “Uongozi wa Kampuni ya TRL unawaomba radhi abiria wote na wananchi kuwa usafiri wa treni unasitishwa kwa muda kutokana na kujaa maji katika stesheni za Godegode na Gulwe mkoani Dodoma na kuharibu tuta la reli.

“Kutokana na uharibifu huo, tunaomba radhi kwa usumbufu  unaojitokeza, tunasitisha kwa muda  huduma ya usafiri  wa abiria kuanzia  Ijumaa Januari 10, 2014 hadi itakapotangazwa tena, kwa wasafiri waliokuwa Dodoma tumeshawatafutia usafiri wa mabasi na abiria waliokuwa Dar es Salaam tumeamua kuwarudishia nauli zao,” alisema.

Mafikiri aliwataka wasafiri wote wenye tiketi halali wafike katika stesheni walizokatia kwa ajili ya kurejeshewa fedha zao.

Alisema kampuni hiyo tayari imetuma mainjinia wake kwa ajili ya kufanya tathmini ili wajue ukubwa wa tatizo na kulishughulikia.

Mafikiri alisema tatizo la kuharibika reli linatokana na mvua zinazoendelea kunyesha kwenye mikoa ya Dodoma, Morogoro na Iringa ambazo zinasababisha  kuharibika kwa  miundombinu ya reli.
Aliwaomba wateja wa usafiri wa treni wawe na subira wakati kampuni ikijitahidi kumaliza tatizo hilo ndani ya muda mfupi.

Abiria zaidi ya 1,600 waliokuwa wakitoka Kigoma kuelekea Dar es Salaam walishindwa kuendelea na safari baada ya reli eneo la Gulwe na Godegode wilayani Mpwapwa kujaa maji kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma jana, Mkuu wa Stesheni ya Reli Dodoma, Zacharia Kilombele, alisema kulingana na tathimini iliyofanyika, eneo hilo wameamua kusitisha usafiri wa reli kwa njia hiyo.

Mkuu huyo alisema kwa kushirikiana na serikali ya mkoa walikubaliana kuwasafirisha abiria hao kwa mabasi ambapo hadi mchana zaidi ya mabasi 17 yalipakia abiria kuwapeleka jijini Dar es Salaam huku mabasi mengine 10 yakisubiriwa kusafirisha abiria waliobaki.

Kilombele alieleza kuwa changamoto kubwa iliyopo ni baadhi ya abiria kuwa na mizigo mingi na mikubwa hali inayowapa ugumu katika kuwasafirisha.

“Usafiri wa treni ya abiria kwenda bara umesitishwa mpaka hapo itakapotangazwa tena,” alisema.

Alisema kinachofanyika sasa ni abiria kurudishiwa nauli zao ili wakatafute usafiri mwingine.

Baadhi ya abiria hao waliiomba serikali kuboresha miundombinu ya reli kwa kuwa usafiri wa treni utegemewa na wananchi wengi wa kipato cha chini.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: