LATEST POSTS

Friday, January 3, 2014

Wananchi wa Kaliua wagoma kuhamia Katavi

UONGOZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua, mkoani Tabora na wananchi wa kata mbalimbali wilayani humo wamesisitiza kupinga mpango wa wilaya hiyo kutaka kuhamishiwa Mkoa mpya wa Katavi
Wamesema mpango huo wa kutaka kuwahamishia wananchi wa wilaya hiyo katika mkoa mwingine wa Katavi hauna tija katika suala zima la mustakabali wa maendeleo yao na taifa kwa ujumla, hivyo hawapo tayari kuhamia Katavi.
Wakizungumza hivi karibuni katika ziara ya kikazi ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kaliua, Mhe. John Kadutu, wananchi wengi wakiwemo viongozi wa chama tawala (CCM) walisema mpango huo utarudisha nyuma maendeleo ya wananchi.
“Sisi hatutahama kutoka Tabora kwenda Katavi. Haiwezekani serikali itutoe karibu na makao makuu ya Mkoa wetu wa Tabora halafu watupeleke Katavi, umbali wa zaidi ya kilometa 70. Tunasema hatuondoki Tabora ng’o,” alisema mzee mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Musa Samuel, kauli ambayo iliungwa mkono na wananchi wengi wa kata 16 kati ya kata 18 za wilaya hiyo.
Akisisitiza hilo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kaliua, John Kadutu, alisema halmashauri yake haipo tayari kuondoka Mkoa wa Tabora na kuhamia Mkoa mpya wa Katavi.
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua, Ibrahim Kifoka, ambaye pia ni Diwani wa Silambo, alieleza kusikitishwa na mpango huo na kusema wananchi wake hawakubaliani na mpango huo.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: