LATEST POSTS

Tuesday, January 21, 2014

Watumishi Wizara ya Ardhi watimuliwa kikaoni

WATUMISHI kutoka Wizara ya Ardhi na wale wa Halmashauri ya Bagamoyo wamejikuta katika  wakati mgumu baada ya kutimuliwa katika kikao kilichoandaliwa na wakazi wa Kijiji cha Makaani Gama, Kata ya Magomeni, wilayani humo kwa lengo la kujua hatima ya ukazi wao katika eneo hilo.
Hali hiyo ilitokea mwishoni mwa wiki, saa 7 mchana baada ya watumishi hao kufika ambako awali walisubiriwa kwa hamu na wakazi hao ambao walijua wangeendelea na ufafanuzi mzuri kuhusu hatima yao na eneo hilo linalotakiwa kupewa mwekezaji ambaye ni Kampuni ya Ecoenergy.
Baada ya kufika kwa ugeni huo kikao kilianza vizuri, lakini hali ya hewa ikaanza kuchafuka pale Mthamini kutoka Wizara ya Ardhi, Eveline Mugasha, alipowasilisha mada ya ujazwaji wa fomu ya fidia inayojulikana kama fomu namba 69, ambayo ilikataliwa awali na wakazi hao kwa madai mpaka wapate ufafanuzi na kuwashirikisha wenzao waishio mjini.
“Jamani mlishakuja na fomu hiyo majumbani kwetu siku kadhaa zilizopita tukawakatalia suala lenu hilo, moja ya sababu ikiwa ni  mkanganyiko wa kichwa cha habari kinachosomeka katika fomu hiyo kuwa ni fomu kwa ajili ya fidia, huyo aliyewaambia tunataka fidia nani wakati kesi yetu bado ipo mahakamani? Tuna imani tutashinda kwa kuwa mahakama ndio muamuzi wa mwisho.
“Kama hamjaja na jambo jipya la kutuambia ni vema mkaondoka  na mkatuachia kikao chetu, ili tuendelee kuweka mikakati ya kuendelea kubaki na eneo letu ambalo tunajua ni haki yetu na mwekezaji analinga’ang’ania kwa masilahi yake binafsi,” alisema Mwenyekiti wa Kamati maalumu iliyoundwa na wananchi hao, Ally Mbawe.
Kutokana na hali hiyo, Ofisa Ardhi, Utalii na Mazingira wa Bagamoyo, Clement Nkusa, alitumia busara kuwapoza wananchi hao ili kuweza kusikilizana na ugeni huo ambako walimpa dakika chache  Kamishna wa Ardhi, Gasper Luhanga, kutoa ufafanuzi kuhusu fomu hizo.
Katika maelezo yake, Luhanga aliuhakikishia umma huo kwamba ujazaji wa fomu hizo hauingiliani na wala hautaathiri kesi iliyopo mahakamani, kwani lengo lao ni kutaka kujua jumla ya wakazi na mali zinazopatikana katika eneo hilo.
“Wananchi mnapaswa kuelewa ili kijiji kiwe kijiji kuthaminiwa ni muhimu, na jambo hili msidhani tunalifanya kwa ajili ya kuwaondoa, badala yake tunataka tujue nani yuko wapi na anamiliki nini, sasa msichanganye na kutathminiwa kwa ajili ya kulipwa fidia na wala kichwa cha habari cha fomu kisiwachanganye kwa kuwa ndivyo ilivyotengenezwa na watunga sheria wetu,” alisisitiza kamishna huyo.
Pamoja na ufafanuzi huo bado baadhi ya wakazi walikuwa wagumu kuelewa  huku wakishauriana kuwa mtu asikubali kujaza fomu hizo mpaka pale watakapowasiliana na mwanasheria wao.
Wananchi hao waliwataka watumishi hao kuondoka na kuwaacha wenyewe katika kikao hicho mpaka pale watakapojadiliana na kuja na jibu moja ambako ilipendekezwa pia kuunda kamati ya ufuatiliaji itakayokuwa inawasiliana kwa karibu na halmashauri.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: