LATEST POSTS

Wednesday, April 9, 2014

Mkwe wa Lowassa afutiwa usajili CRB

http://freemedia.co.tz/daima/wp-content/uploads/2013/11/severe.jpg

MIEZI minne tangu gazeti hili lifichue taarifa za Kampuni ya ukandarasi ya Visual Storm Co. Ltd kuwa imesajiliwa Bodi ya Wakandarasi (CRB) kwa kutumia nyaraka za kughushi, hatimaye kampuni hiyo imefutwa rasmi.
Msajili wa CRB, Boniface Muhegi, amethibitisha kufutwa kwa kampuni hiyo inayomilikiwa na Noel Severe (31), mtoto wa mkurugenzi wa zamani wa Wanyamapori, Emmanuel Severe.
Noel pia ni mkwe wa Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, akiwa amemuoa bintiye aitwaye Dk. Adda Lowassa.
Akizungumza na Tanzania Daima Jumatano, Muhegi alisema kuwa baada ya kujiridhisha wameifuta kampuni na kwamba ikibainika kuendelea kufanya kazi mahali popote nchini, taarifa zifikishwe CRB ili hatua zichukuliwe.
Kwa mujibu wa tangazo la CRB kwa umma, Visual Storm ni ya 52 katika orodha ya makampuni 379 yaliyofutwa tangu Januari Mosi mwaka huu kwa mujibu wa kifungu cha 13 (1) (b) (c) na (d) na 15 (1) (c) cha sheria namba 17 ya 1997 kama ilivyorekebishwa kwa sheria namba 15 ya 2008.
CRB ni chombo cha serikali kilichoanzishwa kwa sheria ya Bunge Na. 17 ya mwaka 1997 ili kusajili wakandarasi wote na kusimamia kazi zao kwa lengo la kuwalinda watumiaji wa huduma za wakandarasi nchini.
Awali gazeti hili katika uchunguzi wake lilijiridhisha pasipo shaka kwamba CRB imeisajili Visual Storm Co. Ltd kwa kutumia nyaraka za kughushi, na hivyo ikaendelea kutekeleza miradi yake ya ujenzi.
Katika kile kilichoonyesha kuwepo kwa nguvu ya viongozi nyuma ya pazia, Visual Storm ilipewa mkataba wa ukarabati wa tawi la Benki ya Biashara ya Dar es Salaam (DCB) mwaka 2011 ikiwa bado haijasajiliwa na CRB kwa mujibu wa sheria.
Visual Storm ilisajiliwa kwa Msajili wa Makampuni (Brella) mwaka 2009 kwa No. 71362 na kisha CRB Februari 23, 2013 kwa No. B5/0674/2/12 daraja la tano.
Kampuni hiyo kabla ya usajili CRB, iliingia mkataba na DCB Oktoba 3, 2011 wa kujenga ukumbi wa mikutano katika tawi la Ukonga kwa gharama ya sh 56,676,580 kwa muda wa wiki tano.
Hadi kufikia Januari 9, 2013, kampuni hiyo ilikuwa imeshindwa kukamilisha kazi hiyo, hatua iliyomlazimu Mkurugenzi Mkuu wa DCB, Edmund Mkwawa, kuiandikia akiitaarifu kusudio la kutaka kuvunja mkataba huo.
Nakala ya barua hiyo pia ilipelekwa kwa msajili wa CRB, Boniface Muhegi, ambapo Februari 12, 2013, bodi hiyo kupitia kwa Kaimu Meneja wa Kanda ya Mashariki, D. J. Karugendo, ilijibu kwa kuiandikia Visual Storm na kuipa siku saba itoe maelezo ya kushindwa kutimiza mkataba huo.
Mkwawa alipotakiwa kufafanua ni kwanini benki yake iliingia mkataba na kampuni ambayo haikuwa imesajiliwa CRB, alisema kuwa suala hilo aulizwe Visual Storm.
“Tunawasubiri hao CRB tukutane mahakamani, lakini kwanini usiwaulize Visual Storm wakakupa majibu?” alisema.
Hadi tuhuma hizo zinafikishwa CRB mwaka jana, bodi hiyo ilidai kutokuwa na taarifa ya kasoro hiyo, japo kulikuwa na kumbukumbu za kuonyesha kuwa walipata barua ya malalamiko ya DCB.
Kwa hatua hiyo, msajili wa CRB, Muhengi alisema kampuni hiyo inapaswa kuadhibiwa kwa kutozwa faini pamoja na DCB kwa kutoa zabuni kwa kampuni ambayo haikuwa na usajili wa bodi yake.
Katika uchunguzi huo, ilibainika kuwa Visual ilikimbilia CRB kujisajili baada ya kushindwa kutimiza mkataba wa DCB kwa wakati, na hivyo kuhofia kukumbwa na rungu la adhabu baada ya benki hiyo kuanza kulalamika.
Hata hivyo, kampuni hiyo ilitumia nyaraka za kughushi hatua ambayo Muhegi alisema kuwa wamiliki wake watapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria baada ya kufutiwa usajili.
Ili kampuni iweze kusajiliwa CRB, Muhegi anasema ni lazima itimize vigezo kadhaa kulingana na daraja husika ambapo wamiliki wanatakiwa kuwa na wataalamu, ofisi na vifaa vya ujenzi.
Kwa upande wa wataalamu, kampuni inapaswa kuwa na mkurugenzi wa ufundi ambaye amesajiliwa na Bodi ya Mainjinia (ERB) ambaye atakuwa ameajiriwa na kampuni husika na kuwa mmoja wa wanahisa.
Kampuni ya Visual Storm awali iliwasilisha vielelezo vya vyeti vya Loserian Sokonoi ambaye hata hivyo alitofautiana na Severe na kuamua kuondoka na kuajiriwa serikalini akiwa ni mhandisi wa wilaya mkoani Shinyanga.
Baadaye kampuni hiyo iliwasilisha CRB cheti cha Kent Kissima na kumtambulisha kama mkurugenzi wa ufundi ilhali ni mwajiriwa wa serikali akifanya kazi kama meneja wa Wakala wa Barabara (Tanroads) makao makuu.
Katika majibu yao ya awali, CRB walisema mkurugenzi wa ufundi wa kampuni hiyo ni Sokonoi na baadaye wakasema ni Kissima ambaye kwa sasa amehamishwa makao makuu (Tanroads) na kupelekwa kuwa meneja wa Mkoa wa Simiyu.
“Tumekwenda huko TRA (Mamlaka ya Mapato) tumekuta kadi za vifaa walizowasilisha huko sio vya kwao, kinachofuata sasa ni kuifuta na kuanza utaratibu wa kuwasiliana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na vyombo vingine vya kisheria,” alisema.
Alipotafutwa Sokonoi kuthibitisha kama ndiye bado mkurugenzi wa ufundi wa kampuni hiyo, alijibu: “Huyo jamaa tulifanya naye kazi, lakini wakati tukiwa kwenye mchakato wa usajili alionekana kunizika fedha zangu nikajiondoa.
“Mimi kwa sasa niko Shinyanga nimeajiriwa serikalini na nilikwishawaandikia CRB kuwaarifu kuwa vyeti vyangu visitumike popote kwenye taasisi yao kwa namna yoyote, maana sifanyi kazi huko tena.”
Naye Kissima kwa maelezo yake mbele ya viongozi wa Tanroads na Wizara ya Ujenzi, alikana kuwapa Visual Storm vyeti vyake ili vitumike kumtambulisha kama mtaalamu wao wa ufundi.
Gazeti hili linayo nakala ya mkataba kati ya Visual Storm na Kampuni ya Fabec/Home base (T) Ltd.
Mkataba huo ulitumiwa na Visual kuwalaghai CRB wakati wa kukaguliwa vifaa vyao vya ujenzi, ili kuonyesha kwamba wameikodishia Fabec iliyokuwa na kazi ya ujenzi wa barabara ya Sumbawanga-Mpanda wakati huo.
Msemaji wa Fabec, aliyejitambulisha kwa jina moja la Ziota, alipotafutwa alilieleza gazeti hili kuwa kampuni yao haijawahi kuwa na mkataba wa aina hiyo na Visual.
“Kampuni hiyo wala sijawahi kuisikia, inamilikiwa na nani?” alihoji Ziota na kufafanua kuwa hata kama wangekuwa wamekodishwa vifaa hivyo, CRB walitakiwa kutembelea mradi wao kujiridhisha kama vipo kweli.
Baada ya kusajiliwa CRB, Kampuni ya Visual Storm imeendelea kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo ile ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) bila kuisajili kwenye bodi kama sheria inavyosema wala kufuata taratibu za kupata vibali vya ujenzi.
Utetezi wa Severe
Mkurugenzi Mkuu wa Visual Storm, Severe, alikiri na kuonyesha mshangao akihoji nani alivujisha suala hilo kwenye vyombo vya habari.
Alidai kuwa ameshangaa kuona nyaraka sahihi alizompatia mshirika wake kwa ajili ya kushugulikia usajili, zilibadilishwa na kupachikwa zile za kughushi.
“Kaka yaani nashangaa kwanini jambo hili linakuwa hivi, mimi hivi vifaa unavyonionyesha hapa kampuni yetu haina na sijui hawa walivitoa wapi,” alisema.
Alipoulizwa kuhusu utata wa mkurugenzi wao wa ufundi, Severe alimtaja Sokonoi kuwa ndiye waliyewasilisha jina lake CRB. Lakini alipobanwa aeleze inakuwaje mhusika anafanya kazi serikalini, alisema walikuwa kwenye mkakati wa kumbadilisha.
Alipoelezwa kuwa CRB wanamtambua Kissima kama mkugenzi wa ufundi wa kampuni hiyo, Severe alidai kutomtambua mtu huyo, huku akionyesha kushangaa alichomekwaje na kuwa mmoja wa wanahisa.
Severe katika kujitetea alimtwisha lawama mtu aliyemtaja kwa jina la Ruben, ambaye alidai kuwa alikuwa mshirika wake kwamba ndiye alivujisha siri hiyo kwa sababu wakati wa usajili CRB alihusishwa kwa ukaribu.
Tanzania Daima lilimtafuta Emmanuel Ruben, ambaye alikiri kushirikiana na Severe katika usajili wa kampuni hiyo CRB, lakini akasema kuwa baadaye walihitilafiana katika mgawanyo wa rasilimali na hivyo akajitoa na kuanzisha kampuni yake.
“Mimi pale CRB nina power of attorney (nguvu ya kisheria) kwa Kampuni ya Visual Storm kwa vile tulikuwa pamoja, lakini kwa sasa niko kivyangu, sasa hayo ya kwamba nimeleta siri hiyo kwenu ndiyo nasikia kwako,” alisema Ruben.

Uchunguzi wa habari hii umefadhiliwa na Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF).

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: