KATIBU wa Taasisi na Jumuiya ya Kiislamu, Sheikh Issa Ponda, 
ameendelea kusota rumande hadi pale jalada la kesi yake litakaporejeshwa
 kutoka Mahakama Kuu.
Akiahirisha kesi hiyo jana hadi Aprili 16, Hakimu mkazi mkoani 
Morogoro, Marry Moyo, aliitaka Idara ya Upelelezi kufuatilia jalada la 
mtuhumiwa Mahakama Kuu ili kesi ianze kusikilizwa.
Sheikh Ponda anayetetewa na wakili wa kujitegemea, Batheromeo 
Tharimo alifikishwa mahakamani hapo chini ya ulinzi mkali licha ya 
kutokuwepo umati mkubwa wa wafuasi wake.
Mara baada ya kufikishwa, wakili wake Tharimo alidai kuwa 
amewasiliana na wakili mwenzake Juma Nassoro ambaye alimweleza kuwa kuna
 ombi waliliwasilisha Mahakama Kuu la kutaka shauri hilo kutoendelea 
kusikilizwa katika Mahakama ya Mkoa wa Morogoro.
Katika ufafanuzi wake juu ya madai hayo, Tharimo alisema kuwa ombi 
hilo linatokana na rufaa namba 98 ya mwaka 2013 waliyoikata mbele ya 
Mahakama Kuu kuhusu Mahakama ya Kisutu kwa shitaka la kwanza la kutotii 
amri halali linalomkabili Ponda mahakamani hapo.
Wakili huyo ambaye alidai kuwa uendeshaji wa kesi hiyo hautaendelea 
hadi uamuzi wa rufaa waliyoikata Mahakama Kuu utakapotolewa, aliiomba 
mahakama kupanga tarehe ya kutaja kesi hiyo.
Hata hivyo, uliibuka ubishano wa kisheria baina ya wakili Tharimo na 
wakili wa serikali, Sunday Hiela, aliyedai ana kumbukumbu za kuonyesha 
mshtakiwa alimkana wakili Tharimo.
Katika maelezo yake Hiela aliongeza kuwa mahakama inashindwa kujua 
kama anamwakilisha Sheikh Ponda au anatoa maelezo ya wakili Juma Nassoro
 ambaye hakuwepo mahakamani hapo.
Wakili huyo wa serikali aliendelea kumwekea pingamizi akidai kuwa 
hakuna nakala yoyote ya ombi ambalo wakili Tharimo alidai kuwa 
waliliwasilisha Mahakama Kuu na kwamba dhamira ya upande wa utetezi ni 
kuchelewesha kesi hiyo ambayo ipo mahakamani hapo kwa zaidi ya mwaka 
mmoja sasa.
Kufuatia kuwepo kwa mapingamizi katika kesi hiyo, hakimu Moyo 
alilazimika kuingilia kati akisema hadi sasa mahakama bado haijapokea 
jalada hilo kutoka Mahakama Kuu ili ipate muongozo wa kuendelea na kesi 
hiyo.
Baadaye aliihairisha kesi hiyo hadi Aprili 16 itakapotajwa tena, 
ingawa wakili Tharimo aliomba kesi hiyo itajwe Aprili 14 kwa madai kuwa 
hatakuwepo kutokana na kuwa na kesi nyingine.
Sheikh Ponda alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Agosti 
10, 2013 akikabiliwa na mashitaka matatu likiwemo la kutotii amri halali
 iliyotolewa Mahakama ya Kisutu, kutoa maneno yenye nia ya kuharibu 
imani za dini na kushawishi watu kutenda kosa.
 
 






 
 
0 comments:
Post a Comment