LATEST POSTS

Wednesday, April 9, 2014

Sheikh Ponda akwama tena

ponda
KATIBU wa Taasisi na Jumuiya ya Kiislamu, Sheikh Issa Ponda, ameendelea kusota rumande hadi pale jalada la kesi yake litakaporejeshwa kutoka Mahakama Kuu.
Akiahirisha kesi hiyo jana hadi Aprili 16, Hakimu mkazi mkoani Morogoro, Marry Moyo, aliitaka Idara ya Upelelezi kufuatilia jalada la mtuhumiwa Mahakama Kuu ili kesi ianze kusikilizwa.
Sheikh Ponda anayetetewa na wakili wa kujitegemea, Batheromeo Tharimo alifikishwa mahakamani hapo chini ya ulinzi mkali licha ya kutokuwepo umati mkubwa wa wafuasi wake.
Mara baada ya kufikishwa, wakili wake Tharimo alidai kuwa amewasiliana na wakili mwenzake Juma Nassoro ambaye alimweleza kuwa kuna ombi waliliwasilisha Mahakama Kuu la kutaka shauri hilo kutoendelea kusikilizwa katika Mahakama ya Mkoa wa Morogoro.
Katika ufafanuzi wake juu ya madai hayo, Tharimo alisema kuwa ombi hilo linatokana na rufaa namba 98 ya mwaka 2013 waliyoikata mbele ya Mahakama Kuu kuhusu Mahakama ya Kisutu kwa shitaka la kwanza la kutotii amri halali linalomkabili Ponda mahakamani hapo.
Wakili huyo ambaye alidai kuwa uendeshaji wa kesi hiyo hautaendelea hadi uamuzi wa rufaa waliyoikata Mahakama Kuu utakapotolewa, aliiomba mahakama kupanga tarehe ya kutaja kesi hiyo.
Hata hivyo, uliibuka ubishano wa kisheria baina ya wakili Tharimo na wakili wa serikali, Sunday Hiela, aliyedai ana kumbukumbu za kuonyesha mshtakiwa alimkana wakili Tharimo.
Katika maelezo yake Hiela aliongeza kuwa mahakama inashindwa kujua kama anamwakilisha Sheikh Ponda au anatoa maelezo ya wakili Juma Nassoro ambaye hakuwepo mahakamani hapo.
Wakili huyo wa serikali aliendelea kumwekea pingamizi akidai kuwa hakuna nakala yoyote ya ombi ambalo wakili Tharimo alidai kuwa waliliwasilisha Mahakama Kuu na kwamba dhamira ya upande wa utetezi ni kuchelewesha kesi hiyo ambayo ipo mahakamani hapo kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa.
Kufuatia kuwepo kwa mapingamizi katika kesi hiyo, hakimu Moyo alilazimika kuingilia kati akisema hadi sasa mahakama bado haijapokea jalada hilo kutoka Mahakama Kuu ili ipate muongozo wa kuendelea na kesi hiyo.
Baadaye aliihairisha kesi hiyo hadi Aprili 16 itakapotajwa tena, ingawa wakili Tharimo aliomba kesi hiyo itajwe Aprili 14 kwa madai kuwa hatakuwepo kutokana na kuwa na kesi nyingine.
Sheikh Ponda alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Agosti 10, 2013 akikabiliwa na mashitaka matatu likiwemo la kutotii amri halali iliyotolewa Mahakama ya Kisutu, kutoa maneno yenye nia ya kuharibu imani za dini na kushawishi watu kutenda kosa.

0 comments: