Mambo yamebadilika. Ukimya ulitawala jana katika Ukumbi wa Bunge
 mjini Dodoma, baada ya wabunge zaidi ya 200 ambao ni wanachama wa Umoja
 wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kususia vikao vya Bunge hilo.
                
              
Ilikuwa ni saa 10:31 jioni baada ya Mjumbe wa 
Bunge hilo ambaye pia ni Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba 
alipohitimisha uchangiaji wake akisema: “Ukawa hatuwezi kuendelea 
kushiriki dhuluma dhidi ya wananchi kwa kupitisha Katiba ambayo ni 
kinyume cha matakwa yao.”
                
              
Baada ya kauli hiyo aliondoka akifuatiwa na 
Mwenyekiti wa Ukawa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, 
Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, James Mbatia na wajumbe wao kutoka nje ya 
Bunge.
                
              
Ukimya ulitawala takriban dakika mbili hivi na 
baada ya wajumbe hao kutoka, Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samia 
Suluhu Hassan aliwaelekeza makatibu kuhesabu wajumbe ili kuona kama 
akidi imetimia ili waendelee na kikao.
                
              
Baadaye aliliambia Bunge kuwa makatibu wamemweleza
 hawahitaji akidi kwa kuwa kikao kilikuwa kinaendelea wakati Ukawa 
walipotoka nje ya ukumbi.
                
              
Hotuba ya Lipumba
                
              
Profesa Lipumba alianza kwa kunukuu Gazeti la 
Mwananchi la Aprili 14, mwaka huu katika sehemu inayosema; “Waziri wa 
Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Uratibu na Bunge) ameanza kampeni 
kanisani kwa kuwataka wananchi kupinga serikali tatu zilizopendekezwa na
 Tume ya Mabadiliko ya Katiba, vinginevyo nchi itatawaliwa na jeshi kwa 
kuwa serikali ya muungano itashindwa kuwalipa mishahara wanajeshi.”
                
              
Alisema yeye ni muumini wa dini ya Mwenyezi Mungu 
lakini anaafiki mapendekezo yaliyoletwa bungeni hapo na Tume ya 
Mabadiliko ya Katiba iliyoundwa na Rais.
                
              
“Hii ni kauli ya Waziri Lukuvi ndani ya Kanisa la 
Methodist wakati wa sherehe ya kumsimika Mchungaji Joseph Bundala kuwa 
Askofu na Waziri Lukuvi alikuwa anamwakilisha Waziri Mkuu.”
                
              
Alisema inasikitisha kwa sababu kauli hiyo inafanana na ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa wakati akihutubia Bunge Maalumu.
                
              
Alisema kauli za Lukuvi zinatisha baada ya kusema 
Wazanzibari ambao wanataka kuwa na nchi yao hawawezi kujitegemea, bali 
wanataka wapate nafasi ya kujitangazia kuwa ni nchi ya Kiislamu.
                
              
“Waziri anaweza kusema hivyo ndani ya kanisa? 
Kawahamasisha mpaka yule kiongozi wa kanisa akasema ili kudumisha 
Muungano bora Katiba ya Zanzibar ifutwe ili iwepo moja ya nchi moja 
ambayo inadumisha Muungano,” alisema.
Alisema Lukuvi alikuwa akiwaaminisha kuwa mfumo wa serikali tatu
 ukipita kutakuwa na mapinduzi na nchi haitatawalika na hivyo watu 
watashindwa kwenda kusali makanisani.
“Kama ndugu zetu wa Zanzibar wangekuwa wanahitaji 
serikali moja tungekuwa na utaratibu mzuri tu, lakini siyo wanachama wa 
CUF, siyo wa CCM, Wazanzibari wote hawataki muungano wa serikali moja,” 
alisema.
Alisema Tume ya Mabadiliko ya Katiba imetoa 
mapendekezo ya serikali tatu kutokana na ukweli huo. “Hoja zilizoletwa 
hapa ni hoja za serikali moja, si hoja za serikali mbili lakini wenzetu 
moja hawataki, kwa hiyo tunahitaji Muungano ambao tutakuwa na maridhiano
 ya pande zote mbili,”
“Wengi wamenukuu makala niliyoitoa katika kituo 
cha TCD (Kituo cha Demokrasia Tanzania), ambayo iliunda Baraza la Katiba
 na mimi nilichambua mapendekezo ya Tume nikasema kwa mapendekezo 
yaliyomo ndani ya Rasimu ya Katiba hayatakidhi mapato ya shirikisho.”
Alisema wajumbe wanaomnukuu wanaishia hapo bila kwenda katika mapendekezo aliyoyatoa.
“Wamenisifu sana ni mchumi mahiri, basi waendeleze
 sifa hizo kwa mapendekezo niliyoyatoa ya mapato ya kukidhi uendeshaji 
wa serikali ya shirikisho.
“Nimeeleza katika hali halisi kuwa utaratibu mzuri
 ni mapato ya kila serikali kuchangia katika shirikisho na mambo haya 
yaandikwe katika Katiba. Katiba inaweza ikasema wazi asilimia 20 ya 
mapato yote yanayokusanywa Zanzibar au Tanganyika yataenda kwenye 
shirikisho.”
Alitaka pia kuwekwa kwa misingi mizuri ya 
kukusanya kodi na kutumia fedha za wananchi ndani ya katiba ya muungano 
ambayo ndiyo katiba mama.
“Lakini ndugu zangu mjadala wetu unavyokwenda 
utadhani kuwa Rasimu ya Katiba iliyoletwa imeletwa na CUF au na Chadema 
au na NCCR-Mageuzi, au Wapemba,” alisema.
Alisema ukurasa wa kwanza wa Rasimu ya Katiba 
unaeleza kuwa toleo hili la Rasimu ya Katiba lilichapishwa katika Gazeti
 la Serikali kwa mujibu wa Kifungu cha 20(2) ya Sheria ya Mabadiliko ya 
Katiba Sura ya 83.
Alisema hiyo ni rasimu ya Tume ya Rais na si rasimu ya Wapemba.
Hata hivyo, alisema mjadala unaoendelea bungeni 
umekuwa na utaratibu wa ubaguzi... “Watu wamebaguliwa humu na viongozi 
wakubwa wanapiga makofi, Bunge hili limekuwa kama Bunge la Intarahamwe. 
Hii ni hatari kwa nchi yetu. Wapemba, Waarabu, Wahindi, Wakongo,” 
alisema.
“Hii hatuhitaji, tunahitaji katiba ambayo itahakikisha kila 
mwananchi anapata haki yake wote tuwe sawa bila kujali rangi zetu, 
jinsia zetu, makabila yetu, huu ndiyo msingi aliotuachia Mwalimu Nyerere
 tuenzi msingi huo.”
Alilalamikia kile alichokiita kuwa ni ubaguzi 
ndani ya Bunge na kwamba kama Serikali haikutaka Katiba Mpya kwa nini 
imepeleka wabunge Dodoma? Pia alihoji ni kwa nini ilitumia Sh70 bilioni 
katika Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
“Kwa nini mmetufikisha hapa? Jengo hili nimeambiwa
 limekarabatiwa kwa Sh8.2 bilioni hali hamuamini Rasimu ya Katiba ama 
ilikuwa ni utaratibu wa kupata hizo asilimia 10, ndiyo maana mmekarabati
 kwa gharama kubwa?” alisema.
“Tunataka CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu 
za Serikali), akague matumizi ya fedha zilizotumika. Utatumiaje fedha 
nyingi wakati hiyo katiba iliyowasilishwa kumbe huitaki kabisa.
“Hakuna utaratibu wowote wa kupiga kura na kufanya
 maamuzi kuhusu sura hizi mbili. Tumechoka kusikiliza matusi. Tumechoka 
kudharau mawazo ya wananchi, tumechoka ubaguzi, hatuwezi kuwa sehemu ya 
kundi linalohamasisha ubaguzi ndani ya Tanzania hili hatukubali,” 
alisema.
 
 






 
 
0 comments:
Post a Comment