LATEST POSTS

Friday, July 11, 2014

AIRTEL YAWAWEZESHA MAFUNZO KUPITIA MTANDAO

Airtel yawawezesha mafunzo kupitia mtandao WALIMU na wanafunzi wa shule za sekondari za Ibiri na Ilongalulu za mkoani Tabora, wamefurahi baada ya kuwezeshwa kupata mafunzo kupitia mtandao kutokana na ushirikiano wa Kampuni ya Airtel Tanzania na mradi wa Millennium Village.
Shule hizo zimefaidika kupitia mradi wa Connect to Learn unaowawezesha wakufunzi na wanafunzi waliopo nje ya nchi kuwasiliana na kupata mafunzo kwa mtandao ambapo Airtel kupitia huduma yake ya intaneti ya 3.5G inaziwezesha shule hizo kuunganishwa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Mkuu wa Shule ya Sekondari Lolangulu, Cleophas Bugombo, alisema wanashukuru kwa mpango huo wa kibunifu unaowezesha kupata nyenzo za ziada za kufundishia.
Alisema kupitia mpango huo wanapata nafasi ya kuwaunganisha wanafunzi wao na wanafunzi wengine kutoka maeneo mbalimbali ya ulimwengu kwa njia ya Skype ambapo wanapata nafasi ya kujifunza na kupeana uzoefu.
“Hiki ni kitu muhimu katika kuongeza upeo wa kufahamu, kwani kuna mambo mengi wanayoweza kuyaona ulimwenguni kuliko wanavyoona sasa kila siku,” alisema.
Chiku Ramadhani, mwanafunzi wa Sekondari ya Ibigiri, alisema anafurahi kuunganishwa na wanafunzi waliopo Marekani kupitia Skype na kuweza kushirikiana na kusoma pamoja.
“Ni ajabu kuona teknolojia inavyotuwezesha sisi watoto wa vijijini kuona mambo ya nje na kujifunza kutoka kwa mataifa mengine, nafurahia sana na ni mengi mazuri ya kujifunza kupitia mtandao,” alisema.
Mkurugenzi wa Mradi wa Millennium Village, Dk. Gerson Nyadzi, alisema kwa kuwekeza kwenye teknolojia ya 3.5G na kutoa huduma ya intaneti ya vifurushi vya mwezi bila gharama yoyote, Airtel imewezesha mradi wa Connect to Learn kuwaunganisha mamia ya wanafunzi kutoka shule zilizo na uhaba wa vifaa zilizoko vijijini.
“Ni matumaini yetu kuwa teknolojia hii itakuwa chachu ya maendeleo na kutoa mwanya kwa wanafunzi kufanya vizuri katika masomo yao,” alisema.
 
Chanzo;Tanzania Daima  

0 comments: