LATEST POSTS

Tuesday, July 15, 2014

Mtuhumiwa tindikali Zanzibar anaswa

MAKACHERO wa Jeshi la Polisi Zanzibar, wamefanikiwa kumtia mbaroni mmoja wa washukiwa wa matukio ya tindikali visiwani hapa, Alawi Mohammed Silima (25), mkazi wa Fuoni Melinne, nje kidogo ya mji wa Zanzibar.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari Mkuu wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Inspekta Mohammed Mhina, mtuhumiwa anahusishwa na tukio la kummwagia tindikali Sheha wa Shehia ya Tomondo mjini Zanzibar, Mohammed Omar Saidi Kidevu kabla ya kutoweka.
Inspekta Mhina alisema mtuhumiwa huyo ambaye kwa muda mrefu alikuwa akisakwa na polisi kuhusu tukio hilo, alikamatwa juzi usiku akiwa mafichoni katika eneo la Fuoni, baada ya taarifa za kiintelijensia kubaini kuwepo kwake.
Alisema bado makachero hao wanaendelea kumhoji mtuhumiwa huyo kwa lengo la kuubaini mtandao mzima wa matukio mbalimbali, yakiwemo ya tindikali yaliyotokea siku za nyuma visiwani hapa.
Alibainisha kuwa kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kunatokana na taarifa za siri za raia wema, ambapo Jeshi la Polisi lilikuwa likiendelea na upelelezi wa chini kwa chini wa kumbaini mtuhumiwa na mahali alipojificha.
Baadhi ya wananchi wa Zanzibar, wamepongeza kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo na kuliomba Jeshi la Polisi kuendelea na juhudi zake za kuwasaka watuhumiwa wengine wanaohusika katika matukio mengine kama hayo siku za nyuma visiwani hapa.
Tukio la kumwagiwa tindikali kwa sheha huyo, lilitokea majira ya saa 2:45 usiku Mei 22 mwaka jana, wakati alipokuwa akirudi nyumbani akitoka kuchota maji nyumba jirani. Alijeruhiwa vibaya mgongoni, kifuani, sikio na jicho la upande wa kulia.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: