LATEST POSTS

Tuesday, July 15, 2014

CHADEMA yajipanga

HUKU Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kikijipanga kuweka safu mpya ya uongozi kitaifa ifikapo Agosti 31, imebainika kuwa mafanikio makubwa yaliyopatikana ndani ya chama hicho chini ya Mwenyekiti, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, Dk. Willibrod Slaa.
Kwamba viongozi hao ni mwiba mkali kwa wapinzani wa chama hicho, hasa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015, ndiyo maana wamekuwa wakisakamwa kila mara katika wiki za hivi karibuni, Tanzania Daima Jumatano limedokezwa.
CHADEMA ndicho chama pekee cha upinzani nchini ambacho tangu kurejea kwa mfumo wa vyama vingi kinazidi kuimarika hatua kwa hatua kila wakati licha ya kuwapo taarifa za CCM kujaribu kukisambaratisha kwa kutumia vyombo vya dola, na wasaliti wa ndani ya chama hicho.
Hata hivyo, jitihada hizo za CCM zimekuwa zinagonga mwamba kwa sababu ya uthabiti wa uongozi wa sasa wa CHADEMA.
Tangu kuanzishwa mwaka 1992, CHADEMA imeongozwa na wenyeviti watatu; Edwin Mtei, Bob Makani na Mbowe ambaye alishika wadhifa huo mwaka 2004 na kufanikiwa kukipa chama hicho haiba na sura mpya, na kukieneza katika kila kona ya nchi akishirikiana na Dk. Slaa na viongozi wengine.
Rekodi za CHADEMA zinaonyesha kuwa katika uchaguzi mkuu wa kwanza wa mfumo wa vyama vingi mwaka 1995, kiliunga mkono mgombea urais wa NCCR-Mageuzi, Augustine Mrema, lakini kilipata viti vinne vya ubunge na madiwani 42. NCCR – Mageuzi ilipata wabunge 27.
Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2000, CHADEMA kiliunga mkono mgombea urais wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba, lakini kikapata wabunge watano na madiwani 75.
Kasi ya CHADEMA ilizidi kuongezeka katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, ambapo kwa mara ya kwanza kiliweka mgombea urais, Freeman Mbowe, kikapata msisimko mkubwa kitaifa na kupata wabunge 11 na madiwani 103.
Kitisho kwa CCM ulikuwa uchaguzi mkuu wa 2010, ambapo Dk. Slaa aligombea urais na kukiwezesha chama hicho kupata wabunge 49 na madiwani 467.
Chama hicho kina wenyeviti katika vijiji, mitaa na vitongoji vingi nchi nzima huku pia kikiwa na mameya na wenyeviti katika halmashauri na majiji mbalimbali.
Ni dhahiri kasi ya CHADEMA inazorotesha uhai wa CCM.
Na kama CCM ilivyofanikiwa kusambaratisha vyama vingine vya upinzani kama NCCR-Mageuzi, CUF na TLP, imeendelea kutumia mbinu hizo hizo dhidi ya CHADEMA, lakini zimegonga mwamba.
CHADEMA kimepitia kwenye dhoruba ya propaganda za udini, ukabila, ugaidi na sasa mkakati umehamia kwenye usaliti wa kupandikiziwa mamluki ndani ya chama ili kuwachafua Mbowe na Dk. Slaa waachie ngazi.
Tukio la karibuni lilikuwa la kutimuliwa kwa viongozi kadhaa wa chama hicho waliobainika kutumiwa na CCM kusambaza nyaraka za mapinduzi ya viongozi kupitia mitandao ya kijamii, mkakati ambao nao umeshindikana.
Na katika kutegua kitendawili cha uchaguzi mkuu wa chama hicho, ambao baadhi ya wasaliti walikuwa wakidai viongozi walivunja katiba kwa kujiongezea muda, Katibu Mkuu, Dk. Slaa ameweka bayana ratiba nzima.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana, Dk. Slaa alisema uchanguzi wa taifa wa kumchagua mwenyekiti na makamu wake wa Bara na Visiwani utafanyika Agosti 31.
Uchaguzi huo ambao wanachama wengi wameonyesha nia ya kumtaka Mbowe agombee tena nafasi hiyo, utakwenda sambamba na chaguzi nyingine za ngazi mbalimbali katika chama.
Kwa mujibu wa Dk. Slaa, baada ya kukamilisha chaguzi ndani ya chama kuanzia ngazi za chini, sasa wanaelekea katika uchaguzi mkuu.
Alisema katika ngazi ya vitongoji wamepata viongozi 196,000 kati ya 256,000 na wataendelea kuchagua viongozi hadi idadi itakapotimia, na kwamba ngazi ya matawi tayari wana viongozi 16,000 kwa awamu ya kwanza.
Dk. Slaa alisema katika awamu ya pili uchaguzi utaanza Agosti 3 hadi 8, na kuendelea katika ngazi ya majimbo pamoja na mikoa ukifuatiwa na mkutano wa siku saba.
Alisema kuwa Agosti 27, utafanyika uchaguzi wa viongozi wa Baraza la Vijana (Bavicha) na Baraza la Wazee, ambapo Agosti 28 ni uchaguzi wa Baraza la Wanawake (Bawacha) huku Agosti 29 ni uchaguzi wa Kamati Kuu ya kwanza.
Agosti 30, Baraza Kuu jipya litakutana ambalo litawezesha Mkutano Mkuu wa Agosti 31 pamoja na kuwapata mwenyekiti na makamu.
Kwa mujibu wa Dk. Slaa, Septemba mosi, Baraza Kuu litakutana kuchagua katibu mkuu na manaibu wawili, na Septemba 2 ni Mkutano wa Kamati Kuu.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: