LATEST POSTS

Tuesday, January 21, 2014

Wakosoa uteuzi wa manaibu wizara ya fedha

Mawaziri na Manaibu Waziri katika picha ya pamoja na Rais Jakaya Kikwete, Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue (wanne kushoto mbele), baada ya Rais kuwaapisha Ikulu jijini Dar es Salaam jana. Picha na Emmanuel Herman.  

Dar es Salaam. Wadau mbalimbali wa uchumi, wamekosoa uteuzi wa Manaibu Waziri wa Wizara ya Fedha, wakisema uteuzi huo haujalenga mikakati ya kuleta maboresho ya kuondoa changamoto zilizopo katika wizara hiyo.
Manaibu walioteuliwa juzi na Rais Jakaya Kikwete ni pamoja na Mbunge wa Iramba Mashariki, Mwigulu Nchemba na Mbunge wa Mkuranga, Adam Malima.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Ajira nchini (TAESA), Eliezer Mwasele alisema viongozi hao wamewekwa kwa lengo la kutimiza malengo ya kisiasa.
“Ni mwaka mmoja tu umebakia tuingie kwenye uchaguzi mkuu na ukiangalia Mwigulu ni mtu wa kusimamia sera na mipango ya chama, nadhani hiyo ni ‘strategic Plan’ (mkakati maalumu) ili kujipanga kisiasa,” alisema Mwasele.
Mwasele amepongeza uteuzi wa Waziri mpya wa Fedha, Saada Mkuya akisema: “Sina shaka naye, ila hao manaibu hakuna lolote katika suala la uwajibikaji, hawana uwezo wa kiutendaji ila ni siasa tu,” alisema.
Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Maofisa Watendaji Wakuu wa Kampuni binafsi (CEO’s Roundtable), Ali Mufuruki alisema viongozi hao wanatakiwa kuwa makini na changamoto kubwa zinazohitaji kupatiwa majibu kwa sasa.
Mufuruki alitaja changamoto kubwa mbili ambazo ni juhudi za ukusanyaji wa kodi pamoja na mvutano wa suala la mafuta na gesi kwa Watanzania.
Kuhusu ukusanyaji wa kodi, Mufuruki alisema mpaka sasa wafanyabiashara wengi bado hawajawa tayari kukubaliana na matumizi ya mashine za EFD.
“Binafsi sioni tatizo kwenye matumizi ya mashine kwa sababu ili kukuza uchumi ni lazima kila mtu alipe kodi, lakini cha kushangaza suala hilo mpaka limekuwa likipingwa na viongozi wa CCM, ni makosa,” alisema.
Kwa upande wake, Profesa Humphrey Mushi kutoka kitengo cha Uchumi, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) alitaja maeneo makubwa matatu ya kuzingatiwa na mawaziri hao ambayo ni kuhakikisha serikali inapunguza matumizi yasiyokuwa ya lazima, kuwekeza bajeti kubwa katika sekta nyeti za Kilimo na Reli.
Chanzo: Mwananchi

0 comments: