LATEST POSTS

Tuesday, July 21, 2015

MAUAJI YA RISASI, TAJIRI J4 MWANZA ABANWA

IKIWA ni takriban zaidi ya wiki moja imepita baada ya Mkurugenzi wa Mabasi ya J4 Express, Juma Mahende ‘J4” kudaiwa kuua kwa kuwapiga risasi wafanyabiashara wenzake wawili, kigogo huyo amebanwa na polisi kuhusiana na mauaji hayo.


Ally Mohamed enzi za uhai wake.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, DCP Charles Mkumbo amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa polisi bado wanafanya uchunguzi wa ndani juu ya tukio hilo huku mtuhumiwa wakimshikilia.
“Tunafanya uchunguzi wa ndani ili kubaini sababu za J4 kuwaua watu hao…waliuawa kikatili na silaha iliyotumika ni bastola aina ya Brown yenye namba 00092890,” alisema Mkumbo.
J4 ambaye mabasi yake yanayofanya safari kutoka Mwanza kwenda mikoa mbalimbali hapa nchini na nje ya nchi, anadaiwa kuwapiga risasi wafanyabiashara wawili, Ally Mohamed Abeid na Claude Steven Sikalwanda wakazi wa Jiji la Mwanza Julai 13, mwaka huku chanzo cha tukio hilo kikitajwa kuwa ni kudhulumiana katika biashara.

Cloud Steven enzi za uhai wake.
Gazeti hili lililifuatilia tukio hilo ambalo limekuwa gumzo mjini Mwanza ambapo  liliweza kumpata Ramadhan Mohamed Abeid ambaye ni mdogo wa Ally Mohamed  aliyeuawa na alisimulia kama ifuatavyo:
“Siku ya tukio hilo kaka yangu  alinipigia simu saa 8:30 mchana akinitaka nimpelekee gari alilotaka kununua wakati huo akiwa Nyakato, wilayani Nyamagana jijini hapa.
“Nilipofika nilimkuta kaka yangu akiwa na Claude pamoja na mtu ambaye namfahamu kwa sura  ambapo waliku    wa wakimsubiri J4 ili awapatie fedha kutokana na biashara waliyokuwa wamefanya, tulikaa hapo mpaka saa 11 jioni.
“Walipoona J4 amechelewa kaka yangu aliomba twende mjini kutengeneza simu yake wakati huo wakiendelea kuwasiliana na J4 kuhusu biashara zao lakini alisikika kulalamika sana juu ya fedha zake, ilipofika saa moja kasoro  jioni nikaomba kwenda kufuturu, nikawaacha wakisubiri simu kwa fundi huyo ndiyo ukawa mwisho wa kuonana nao kwani walikuwa pamoja,” alisema Ramadhani.

Ally mohamed akizikwa.
Naye dada wa Claude,  Aziza Steven alisema usiku huo marehemu waliwahi kurudi nyumbani wakiwa katika hali ya kawaida na waliandaliwa chakula cha usiku wakala lakini Ally Abeid wakati anakula alikuwa anapigiwa simu na J4 akimtaka wakaonane ili kupeana pesa walizokuwa wamefanya biashara zao.
“Marehemu hakukubali kwenda usiku huo, akamtaka waonane kesho yake asubuhi, kutokana na mvutano huo Ally alivaa suruali na shati jeupe na  miguuni alivaa ndala wakaondoka wote huku Ally akisema wanaenda kuchukua shilingi milioni 25 kwa J4 walizokuwa wamekubaliana katika biashara zao, ikawa mara yao ya mwisho kuongea na kaka yao.
Baada ya Ally na Steven kuuawa ndugu zao Ramadhani na Aziza wakiwa pamoja mmoja wao alisema: “ Sisi tulipata taarifa usiku kuwa ndugu zetu wameuawa, tulikusanyika na saa 12 asubuhi tulikwenda Hospitali ya Rufaa Bugando tukaona miili yao ndipo tukaanza kufuata taratibu za kuweza kupata maelezo ya kitaalamu.
“Daktari mmoja alisema baada ya kuchunguza miili ya ndugu zetu, iligundulika Ally alipigwa risasi tatu kifuani na Steven alipigwa risasi moja kifuani na kusababisha vifo vyao papo hapo,” alisema Ramadhani.
Inadaiwa kuwa mara baada ya J4 kuwaua watu hao maeneo ya Nyakato kulikuwa na baadhi ya majirani ambao hawakuwa mbali sana na eneo la tukio waliliambia gazeti hili kwa masharti ya kutotaja majina yao kuwa risasi ndizo zilizowashitua wakaenda eneo la tukio.
“Tulipofika nyumbani kwa J4 tulimkuta  akiwa amesimama karibu na hao marehemu na baada ya muda mfupi polisi walifika eneo la tukio wakamkamata na  kumuingiza kwenye gari na maiti kisha wakaelekea Hospitali ya Bugando,” alisema shuhuda mmoja kwa sharti la kutotajwa jina.
Marehemu Claude alikuwa ni mkazi wa Nyansaka nje kidogo ya Jiji la Mwanza, alikuwa mfanyabiashara wa nafaka, ameacha mke pamoja na watoto wa nne, kwa upande wa Ally alikuwa akiishi maeneo ya Igoma na alikuwa akijishughulisha na shughuli za ujenzi lakini pia alikuwa mfanyabiashara wa  baa na gesti maeneo ya Igoma, ameacha watoto watatu na mke.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Malongo (pichani) amezihakikishia familia na ndugu wa marehemu waliouawa kuwa watahakikisha haki inatendeka kwa mshtakiwa kwani hakuna mtu ambaye yupo juu ya sheria.

0 comments: