LATEST POSTS

Tuesday, July 21, 2015

UKWELI MAUAJI POLISI STAKISHARI

TAKRIBANI siku 9 tangu kutokea kwa uporaji wa silaha na mauaji ya askari wanne na raia watatu katika Kituo cha Polisi Stakishari jijini Dar es Salaam, moshi mweupe wa ukweli umenza kufuka.

Gaston polisi aliyenusurika.

Uchunguzi na vyanzo mbalimbali vya habari wakiwemo polisi ambao hawakutaka kutajwa majina yao, umesaidia timu ya waandishi wetu kubaini jinsi tukio hilo la kinyama lilivyofanyika.
“Wavamizi inaonesha walipanga zoezi hilo mapema, walijua wapi ghala la silaha lipo, walisoma pia mazingira ya ulinzi yalivyo pale kituoni nyakati za usiku,” polisi mmoja wa Stakishari aliyeomba hifadhi ya jina lake alisema.

UVAMIZI ULIVYOKUWA
Imeleezwa na mashuhuda wa tukio hilo kwamba majira ya saa 5 usiku, Julai 12, mwaka huu, watu zaidi ya 16 wakiwa na bunduki huku wakiwa wamevalia makoti meusi, walifika kituoni hapo kwa staili ya kutaka huduma lakini ghafla walifanya shambulizi la kushtukiza.
“Niliona pikipiki kama saba zinaingia eneo la kituo, nikadhani ni bodaboda wana shida kituoni, ghafla nikaanza kusikia milio ya risasi.“Nikakimbia kuelekea nyumbani kujifungia, baada ya hali kutulia nikarudi kituoni nikakuta askari na raia wameuawa,” alisema shuhuda wa tukio hilo ambaye hakupenda kutajwa jina lake.

POLISI, RAIA WALIVYOUAWA
Habari zinadai kuwa baada ya wahalifu hao kufika kituoni hapo, watatu kati yao walitengeneza mzozo wa kuigiza ili kuwahadaa askari waliokuwepo kituoni kuwa kufika kwao kulikuwa ni kupata huduma na siyo vinginevyo.
Inaelezwa kwamba wakati wahalifu hao wakizozana kuelekea mapokezi ya polisi, wenzao walitawanyika kuzunguka eneo lote la kituo kwa lengo la kudhibiti usalama.
“Askari mwenye silaha alikuwa mmoja pale kituoni, alipowaona wale watu watatu aliwauliza shida yao, kabla hajawajibu wakamfyatulia risasi zilizomjeruhi begani na kifuani.“Alipodondoka chini waliingia mapokezi, wakakuta polisi wawili na raia watatu, wakawaua wote kwa risasi.
“Askari wengine wawili waliwafuata vyumbani walikokuwa wamekimbilia kujificha, wakawaua, baadaye wakavunja ghala la silaha na kuiba,” chanzo chetu kilisema.


RAIA WALIFUATA NINI KITUONI?
Uchunguzi unaonesha kuwa raia watatu waliouawa katika tukio hilo, walikwenda kituoni hapo usiku kwa ajili ya kupata msaada wa polisi kufuatia tuhuma za kuibiwa kwa shilingi laki nne kwenye eneo walilokuwa wamekaa.
Inaelezwa kwamba, Jackline Mdume (marehemu) mkazi wa Manzese, Dar aliitwa na rafiki yake aliyetajwa kwa jina la utani la Mchakarikaji mwenyeji wa Tabata Kisukulu ili wakabadilishane mawazo ya kimaisha.
Akiwa na rafiki yake kwa mazungumzo, muuzaji wa vinywaji baridi aliyekuwa akiwahudumia, alilalamika kuibiwa kiasi cha shilingi laki nne ambapo mtuhumiwa wake mkuu alikuwa ni Jack.“Baada ya mzozo wa muda mrefu wakakubaliana waende polisi, Erick Swai (marehemu) alijitolea gari la kuwapelekea kituoni.
“Baadaye Swai akamuomba kijana mwingine (jina halikupatikana) amsindikize, wakamchukua na Jack. Mlalamikaji na mwenyeji wa Jack wakasema wataenda kwa usafiri wao, wakiwa kituoni ndiyo yakatokea hayo mauaji,” alieleza mtoa habari wetu.

 
ASKARI MAJERUHI AONGEA
Akiongea  na gazeti hili katika Hospitali ya Taifa  Muhimbili wiki iliyopita, askari aliyejeruhiwa katika tukio hilo la kikatili, PC  Gaston Shadrack alisema  kupona kwake ni  mipango ya Mungu.Akiongea  kwa masikitiko huku Mkuu wa Kituo (OCS) wa Stakishari akiangua kilio baada ya kumuona  askari wake aliyenusurika, Gaston alisimulia kuwa walitangulia watu wanne wakiwa  wamevaa makoti huku wakilumbana kama  watu waliodhulumiana.
Majeruhi huyo alipojaribu kuwahoji, ghafla  walichomoa silaha na kuanza mashambulizi makali.
“Mimi baada ya kupigwa risasi niliangukia tumbo hivyo walidhani nimekufa, hawakuhangaika na mimi tena, waliingia kituoni, wakaua askari wenzangu  pamoja na raia.
“Mmoja kati ya watu wale alikuja nilipokuwa nimeanguka, akanipiga teke, akawaambia wenzake ‘amekufa’, niliendelea kujilegeza huku nikiilalia bunduki yangu wasiione.
“Sikuwa na nguvu za kuinuka, walipomaliza uhalifu wao walitoka kwa tahadhari kubwa, niliendelea kutulia pale chini.
“Wakati wanaondoka pikipiki moja iligoma kuwaka, nikafyatua risasi mbili zilizompiga mmoja wao, akadondoka,” alisema PC Gaston.

 
WAHALIFU WALIONDOKAJE?
Habari kutoka eneo la tukio zinadai kuwa baada ya kufanya mauaji na kukusanya silaha, wahalifu hao walitoweka kupitia njia tofautitofauti.
Aidha, inadaiwa kuwa rundo la bunduki walizopora waliziingiza kwenye gari aina ya Toyota Noah la rangi nyeusi ambalo lilikuja na kuegesha karibu na kituo hicho.Inaelezwa kuwa mbali na bunduki, wahalifu hao walifanikiwa kuiba pia radio ya mawasiliano ya kipolisi (radio call) ambayo waliitumia kujua namna walivyokuwa wakifuatiliwa na vyombo vya usalama.

SILAHA ZINAZOIBWA ZINAPELEKWA WAPI?
Kitendawili cha wapi silaha zinazoibwa zinapelekwa na kwa kazi gani, bado hakijateguliwa ingawa yamekuwepo madai kuwa kuna kundi la watu ambalo linakusanya silaha hizo kwa lengo la kufanyia uhalifu mkubwa.

 
Baadhi ya wananchi ambao hawakupenda kutajwa majina yao, waliviomba vyombo ya usalama kuyachunguza mapori ya Kisarawe na Mkuranga, Mkoa wa Pwani na mkoani Morogoro kwa madai kuwa misitu hiyo inatumiwa na wahalifu kupata mafunzo na kuhifadhi silaha.
“Mambo mengine tunaogopa kuyazungumza waziwazi lakini serikali ikiamua kufanya uchunguzi kwenye misitu mikubwa pamoja na kufuatilia nyendo za baadhi ya mashirika ya dini, watabaini mambo mazito sana,” alisema mwananchi mmoja mkazi wa Kisarawe alipozungumza na gazeti hili.

FAMILIA ZA ASKARI WALIOUAWA ZANENA
Mke wa marehemu CPL Peter Sabuni mwenye namba E 1279, Mary Sabuni alishangazwa na mauaji ya mumewe huku akijiuliza kama ataweza kuwatunza watoto akiwa peke yake.“Nipo kwenye wakati mgumu, mtu niliyekuwa namtegemea ameuawa kinyama, sijui nitawalea vipi wanangu,” alisema Mary huku akiangua kilio.
Naye ndugu wa CPL Gaudiani Cyprian ambaye alijitambulisha kwa jina moja la David, alisema wamepata msiba mzito na ambao hauelezeki.“Nafikiri unajua kuwa baada ya msiba wa ndugu yangu kutokea, mama yetu alipopata taarifa alidondoka na kufariki dunia, hivi ninavyokwambia tuna misiba miwili mizito.”
Aidha mke wa SGT Adam Nyamuhanga mwenye namba D 69652, Jesca Adam alisema haamini kilichotokea, anaona kama ni ndoto ya mchana.“Mume wangu aliniaga anakwenda kazini atarudi kesho, mpaka usiku saa tatu siku ya tukio niliwasiliana naye, leo naambiwa ameuawa! Siamini,” alisema.
Naye mdogo wa marehemu H 1030, PC Antony Komu aliyejitambulisha kwa jina la ‘Komu Mdogo’ alisema amepokea kwa masikitiko makubwa kifo cha kaka yake.“Kaka yangu alikuwa ndiyo kila kitu kwangu, ndiye alikuwa akinisomesha, sasa sijui nitasomaje, naona giza kwenye maisha yangu,” alisema.

KAMISHINA KOVA HUYU HAPA
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Kipolisi Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova wakati anawaaga wapiganaji hao, alisema: “Nakemea na kulaani kitendo hiki cha kinyama na tutahakikisha waliohusika wanakamatwa wote kwa muda mfupi. Pia tutahakikisha serikali inalipa mafao kwa kila askari  aliyepoteza maisha.”
 
OMBI KUTOKA KWA POLISI
Baadhi ya maofisa wa polisi wameiomba serikali kuangalia namna ya kuwasaidia watoto wa marehemu ili kuwawezesha kupata haki zao za msingi likiwemo suala la elimu.
“Tumesikia Kamishna Kova amesema atasimamia mafao ya marehemu, hilo ni sawa lakini waangalie jinsi ya kuwasaidia watoto hasa wale wadogo ambao wazazi wao wamepoteza maisha wakilitumikia taifa,” alisema polisi mmoja kwa sharti la kutotajwa jina lake.

Source: Global publishers

0 comments: