LATEST POSTS

Wednesday, December 18, 2013

MARUFUKU HALMASHAURI KUFANYA VIKAO VYA HALMASHAURI BILA WABUNGE

HALMASHAURI zote za wilaya nchini zimepigwa marufuku kuandaa vikao vya halmashauri bila kutoa taarifa kwa wabunge kwa sababu nao wana haki ya kuhudhuria vikao hivyo Kikatiba.
Hayo yalielezwa Bungeni  mjini hapa jana na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri, alipokuwa akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR-Mageuzi).
Mbunge huyo alitaka kujua, Serikali inazichukulia hatua gani baadhi ya halmashauri nchini zikiwemo za Kasulu na Kibondo, ambazo huandaa vikao vya halmashauri bila kuwaita wabunge na  hasa wakati vikao vya Bunge vikiendelea.
Mbunge huyo pia, alihoji ni kwa nini makatibu wa wabunge hata wakiingia kwenye vikao hivyo hawalipwi posho kwa madai kuwa si wajumbe wa vikao wakati maofisa tarafa na watendaji wanalipwa posho hizo pindi wanapoingia kwenye vikao hivyo.
Akijibu swali hilo, Mwanri alisema tayari Serikali imeandaa taarifa itakayopelekwa kwa halmashauri zote nchini kuhakikisha kuwa zinaandaa vikao kulingana na ratiba za Bunge ili wabunge ambao ni wajumbe wa vikao hivyo nao wapate fursa ya kuhudhiria.
Alisema kikatiba Wabunge  nao ni madiwani wana haki zote za kuhudhuria vikao vya halmashauri, na kupiga marufuku halmashauri zote nchini kuandaa vikao vya halmashauri bila kumpa taarifa mbunge.
“Huyu mbunge ana mchango mkubwa kwenye vikao hivi, anahudhuria vikao vikubwa kama Bunge, hivyo ana uzoefu na uelewa mkubwa,” alisisitiza Mwanri.
Aidha Kuhusu posho kwa maofisa tarafa, Naibu Waziri huo alikiri kuwa huwa wanalipwa posho wakiingia kwenye vikao hivyo, kwa sababu wao ni wasaidizi wakubwa wa Mkuu wa Wilaya na wanatambulika kisheria wakati makatibu wa Bunge pamoja na kuwa na sifa ya usaidizi kwa mbunge bado hawajatambulika kisheria kuweza kulipwa posho katika vikao hivyo.
Alisema upo uwezekano wa suala hilo kushughulikiwa  kwa wabunge kuwasilisha maoni na mapendekezo ya kuibadilisha Sheria iliyopo ya halmashauri ambayo itaweza kuwatambua makatibu wa Bunge kama wasaidizi wa wabunge na walipwe posho kwenye vikao hivyo.

0 comments: