LATEST POSTS

Friday, January 24, 2014

Barabara ya Moro -Dom yatengamaa

Kilosa. Hatimaye Daraja la Magole la Mto Mkundi ambalo tuta zake zilisombwa na maji na kusababisha huduma ya usafiri kati ya Morogoro na Dodoma kukatika kwa siku tatu, limefunguliwa kwa kuruhusiwa magari ya mizigo yenye uzito wa zaidi ya tani saba kupita.
Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli aliyefungua daraja hilo jana saa 4.45 asubuhi alisema, kazi ya kutengeneza tuta hizo zilizokuwa zimesombwa na mafuriko yaliyotokea Januari ya kuamkia 22, saa 11 alfajili,ilifanyika kuanzia Alhamisi asubuhi kwa wahandisi wa Wizara ya Ujenzi kusimamia kazi hiyo.
Dk Magufuli alisema, kukatika kwa tuta za daraja hilo haijawahi kutokea tangu kujengwa kwa daraja hilo miaka ya 70 na kwamba tuta hizo lilisombwa kwa mita 50 upande wa Morogoro na mita 20 upande wa Dodoma.
“Kama hatua za haraka zisingechukuliwa, ujenzi huu wa tuta za daraja ungechukua miezi miwili hadi mitatu mpaka kukamilika kwake, lakini niliwataka mainjinia (wahandisi) wangu kufanyakazi usiku na mchana ili liweze kutumika na wananchi wapate huduma za kimsingi, kwani magari mengi ya mizigo yamebeba bidhaa zinazohitajika upande wa pili,” alisema Waziri Magufuli.
Waziri huyo wa ujenzi, pamoja na kuwapongeza wahandisi hao kukesha usiku na mchana, aliwataka wasafiri wa mabasi na magari madogo, kuendelea kutumia Barabara ya Melela-Kilosa kutokea Dumila hadi foleni ya malori itakapomalizika.
Pia Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Morogoro, Boniface Mbao alisisitiza uamuzi huo wa Waziri Magufuli kuzingatiwa na madereva ili zoezi hilo liweze kukamilika kwa haraka.
Kwa upande wao madereva wa magari makubwa na ya masafa marefu, walimwomba Waziri Magufuli kuwaruhusu kupita mizani bila kupima kwa kuonyesha risiti walizokwishapima katika mizani ya Kibaha.
Pia waliomba ili kukabiliana na foleni iliyojitokeza kwa sasa na kwa baadaye, malori yasiyo na mizigo yapite bila kupima, rasta katika milima ziondolewe, yabaki matuta na mizani ya Kihonda iondolewe au kutengenezwa kutokana na kushindwa kufanya kazi nyakati za mvua, mambo ambayo Dk Magufuli aliahidi kuyafanyia kazi ila la kuacha kupima mizani alisema ni vigumu kwa vile lipo kisheria.
Baada ya kujibu maombi ya madereva hao wa malori, Dk Magufuli aliwataka wahandisi hao wa wizara kuendelea kubaki katika eneo hilo hadi daraja litakapo kamilika, kutokana na barabara hiyo kutegemewa kupitisha zaidi ya magari makubwa 3,000 kwa siku.
Barabara ya Morogoro-Dodoma imekuwa ikipitisha magari madogo na mabasi zaidi ya 25,000 kwa siku kupitika hali ya waathirika wa mafuriko katika eneo hilo bado si shwari kutokana na kulala nje ya nyumba zao na wengine kulala barabarani.
Akizungumza na gazeti hili mmoja wa waathirika Haruna Rajabu alisema, kama misaada hiyo haitasimamiwa kikamilifu upo uwezekano wa kuzuka kwa migogoro kwani kwa kiasi kikubwa waathirika wa mafuriko hayo wamepoteza vyakula na mavazi.
Alisema yanapotokea majanga ya aina hiyo mara nyingi, kunazuka migogoro baada ya misaada inayotolewa kutolewa kwa kujuana na.

Wakati mwingine kutolewa kwa watu walionusurika badala ya kuwapa kipaumbele watu walioathirika kwa kiasi kikubwa pamoja na watu wasiojiweza kama wazee, wajane na watoto.
Hata hivyo Haruna aliiomba Serikali na wasamaria wema kuwa pamoja na kupeleka misaada ya vyakula pia misaada ya sare za shule, viatu na madaftari vinahitajika kwani wanafunzi wengi nao wamepoteza vifaa hivyo muhimu.
Vilevile aliiomba Serikali kupeleka misaada ya mbegu za mahindi, mpunga na mazao mbalimbali kwani mafuriko hayo yamesababisha mbegu na mazao yaliyopandwa kwenye mashamba nazo kuzolewa na maji na hawana mbegu za kupanda.
Naye Fatuma Mbonde mjane mwenye watoto wanne ambaye pia ni mwathirika wa mafuriko hayo aliiomba Serikali kupeleka dawa za magonjwa ya milipuko kwani kutokana na mafuriko hayo vyoo vingi vimebomoka na hivyo vinyesi kuelea juu ya maji.
Aliomba pia msaada wa majisafi na umeme kwani kwa sasa visima vya asili na mabomba yameziba na mengine kung’oka kabisa, huku eneo hilo la Magole likiwa gizani kutokana na nguzo za umeme kuanguka na kuzolewa na maji.

0 comments: