LATEST POSTS

Friday, January 24, 2014

Mvua yaharibu miundombinu reli


Nyumba ikiwa imeharibiawa na mvua iliyoambatana na upepo mkali mkoani Dodona. Mpigapicha wetu 

Dar es Salaam. Wakati timu ya wahandisi ikiendelea kufanya tathimni na marekebisho ya awali ya kipande cha reli reli kilichoharibika eneo la Godegode kutokana na mvua kubwa zilizoanza kunyesha mwanzoni mwa Januari mkoani Dodoma, hali imekuwa mbaya zaidi baada ya kipande kingine kuharibika upya.
Kufumuka upya kwa kipande kingine cha reli kumetokana na mvua zilizonyesha alfajiri ya juzi na kusababisha maji kufunika eneo la reli hali iliyopelekea maji kufurika na kusababisha uharibifu huo.
Hali hiyo imetokea baada ya muda wa wiki mbili ambapo Kampuni ya Reli ilitangaza kukamilisha ukarabati wa kipande hicho ili kuruhusu njia ya reli kupitika.
Akizungumza na gazeti hili, Kaimu Mkurugenzi wa Kampuni ya Reli, Mhandisi Paschal Mafikiri alisema kuwa njia ya reli katika eneo la Godegode imezidi kuwa mbaya zaidi kutokana na mvua hizo kusababisha kufumuka kwa kipande kingine.
“Tathimini na marekebisho ya awali yamefanywa na wahandisi wetu na tukakubaliana tuweke tuta lingine, lakini kabla hilo halijafanyika mvua zimeharibu eneo lingine,” alisema.
Mkurugenzi huyo alisema kwamba marekebisho hayo yanaweza kuchukua wiki mbili zaidi kukamilika kwake mpaka kurejesha huduma za usafiri kwa watumiaji wa reli hiyo.
“Siwezi kusema kwa usahihi njia hii itaanza kutumika lini, ila baada ya kurudi timu ya wataalamu iliyokuwa eneo la tukio hapo ndio tutakuwa na taarifa zaidi, lakini kwa sasa ninachoweza kusema hali ni mbaya eneo la Godegode na Gulwe.”
Januari 10 mwaka huu Kampuni ya Reli ilitanganza kusimamisha safari zote za reli ya kati kwa muda usiojulikana kufuatia kuwepo kwa uharibifu mkubwa wa kipande cha reli eneo la Godegode na Gulwe uliotokana na mvua.

0 comments: