LATEST POSTS

Monday, January 13, 2014

Wakulima, wafugaji vitani Kiteto



Majeruhi Kiteto
MZAHA na uzembe unaodaiwa kufanywa na baadhi ya viongozi wilayani Kiteto na mkoani Manyara katika kusuluhisha mgogoro wa wafugaji na wakulima, umesababisha mauaji ya watu zaidi ya 13 usiku wa kuamkia jana.

Mbali ya vifo hivyo, vita hiyo iliyaonza majira ya saa 11 alfajiri kwa kutumia silaha za moto na jadi, imesababisha majeruhi zaidi ya 50 huku wengine wakiachwa na ulemavu wa kudumu.

Baadhi ya wakulima waliozungumza na gazeti hili jana, walisema wafugaji wa jamii ya Kimasai walivamia nyumba zao alfajiri ya kuamkia jana na kuzichoma moto, huku wakitoa kipigo kwa kila mtu waliyemuona mbele yao.

Habari hizo zinasema wakulima waliokuwa wabishi na kujaribu kupambana na kundi hilo la wafugaji wa Kimasai, walipigwa risasi na kupoteza maisha.

Hali ya baadhi ya vijiji wilaya Kiteto ilionekana kama uwanja wa vita kwani milio ya risasi na milipuko ya moto ilisikika kila kona.

Kuona hivyo, baadhi ya familia hasa wanawake na watoto, walilazimika kukimbilia porini ambako wafugaji hao waliwafuata na kuwaua.

Taarifa za awali zilizotolewa na wakulima zilisema kuwa mapigano hayo sasa yameingia katika hatua mbaya kwani kuna kundi kubwa la jamii ya wafugaji wa Kimasai wakiwa na silaha za kivita.

Mmoja wa wakulima, Machite, alisema eneo la Laitimi lenye wakulima wengi, ndilo lililoathirika zaidi na mapigano hayo.

“Sasa ngogoro huu unazidi kukua na unazidi kutumaliza sana na hiyo inasabaishwa na viongozi kupokea rushwa kutoka kwa wafugaji kwa madai kuwa watawafukuza wakulima ili Wamasai wachunge mifugo yao.

“Juzi tulifanya mkutano na Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Erasto Mbwilo juu ya kutatua migogoro na mfugaji mmoja wa Kimasai alieleza kuwa kiongozi mmoja wilayani Kiteto anachangisha fedha kwa ajili ya kuwapa maeneo ya kuchungia,” alisema.

Akizungumzia mgogoro huo, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alisema tangu kuanza kwa mapigano hadi sasa watu zaidi ya 20 wamepoteza maisha.

Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Mkilamali Mpwapwa, alisema idadi ya waliofariki ambao miili yao imeshapatikana ni sita, lakini kuna uwezekano wa kuwapo wengine porini, hivyo wanaendelea kuwatafuta.

Kamanda huyo alisema bado wanafanya tathimini kujua idadi ya nyumba zilizochomwa na hasara iliyopatikana.

Alisema jeshi lake limeimarisha ulinzi na linawasaka wanaodaiwa kuhusika na mauaji hayo.

0 comments: