LATEST POSTS

Monday, January 13, 2014

Nyalandu: Ripoti ya Lembeli uongo mtupu

         http://freemedia.co.tz/daima/wp-content/uploads/2014/01/nyalandu1.jpg

NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, ameilalamikia Kamati ya Bunge ya Ardhi, Mazingira na Maliasili iliyoongozwa na James Lembeli kuwa taarifa iliyowasilisha bungeni na kuwang’oa mawaziri wanne ilikuwa ya uongo. 

Nyalandu alitoa kauli hiyo juzi alipozungumza na viongozi wa taaluma mbalimbali pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dodoma na Manyara juu ya mgogoro wa mipaka kati ya hifadhi ya taifa ya Tarangire, Pori la Akiba Nkungunero na vijiji vya jirani uliofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara.
Alieleza kutokana na taarifa hiyo Tanzania kwa sasa imeonekana kushuka kwa kiwango kikubwa  katika utawala bora ikiwa ni pamoja na ukiukwaji wa haki za binadamu.
Alisema kuna taarifa ambazo zilionyesha kuwa wapo watu ambao walibakwa jambo ambalo halikuwa la kweli.
Hata hivyo, alisema kwa sasa Rais Jakaya Kikwete amekubali kuunda tume ya kimahakama ambayo itafanya uchunguzi juu ya kuwepo kwa matukio hayo na itakapabainisha kuwa kuna watu walipotosha ni wazi watachukuliwa hatua kali za kisheria bila kujali cheo cha mtu ambaye alihusika na uongo au ukiukwaji wa sheria.
Katika hatua nyingine, Nyalandu ametangaza kumsimamisha kazi ofisa wanyamapori mwandamizi katika pori la akiba la Maswa, Lawrence Kileo, kwa kutuhumiwa kupokea rushwa na kuwatoza faini wafugaji bila kuzingatia taratibu.
Hatua hiyo imekuja ikiwa ni siku chache tangu atangaze kusimamishwa kazi kwa watumishi 22 wa wizara hiyo.
Ofisa huyo anatuhumiwa kuwatoza faini wafugaji wanaoingiza mifugo yao katika pori hilo bila kutoa risiti za serikali, na hivyo fedha hizo kujinufaisha mwenyewe kinyume cha kifungu cha sheria namba 116[2]C cha sheria ya kuhifadhi wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009.
Nyalandu ametangaza kuanza kwa uchunguzi kwa Ofisa Wanyamapori wa Wilaya ya Kasulu, Benjamini Mkosamali, kabla ya kuchukuliwa hatua za kinidhamu kwa kuwaruhusu watuhumiwa wa ujangili kuondoka na nyara za serikali walizokamatwa nazo kabla ya kukamatwa tena kwa msaada wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Nyalandu alisisitiza kuwa serikali itaendelea kuchukua hatua zaidi kwa maofisa wote watakaobainika kujihusisha na vitendo vyovyote vile vya kukiuka maadili ya kazi yao.
Watuhumiwa hao wa ujangili mkoani Kigoma ambao walikamatwa wakiwa wamebeba wanyama aina ya tohe 12, madume watano na majike saba wakiwa pia na insha wanne aina ya Oribi ambao hawakupaswa kuwinda kwa mujibu wa leseni yao ya uwindaji namba B59921 iliyotolewa Kigoma.
Alisema awali watuhumiwa hao walikamtwa na kikosi cha doria cha Kampuni ya Friedkin Conservation Fund  na kumuita ofisa huyo kwa ajili ya kuchukua hatua zaidi ambapo alipofika na kuzungumza na watuhumiwa aliwaruhusu kuondoka na wanyama hao.
Nyalandu alisema Benjamini akiwa na taaluma ya kusimamia wanyamapori huku akifahamu majangili waliokamatwa wamekutwa na nyara za serikali na wamekutwa katika kitalu cha uwindaji  sehemu ya Kibenge, baada ya kupata taarifa kwa wahusika, aliamua kwa makusudi kuwaruhusu majangili hao kuondoka.
“Hivyo nimeagiza mamlaka husika kukamilisha uchunguzi na kumchukulia hatua za kinidhamu na za kisheria haraka sana ofisa huyo,” alisema Nyalandu.
Alisema kuwa vita dhidi ya ujangili itaendelea kwa kasi na hata rais ameishaahidi kuwa operesheni ujangili awamu ya pili itarejea hivi karibuni baada ya kurekebisha kasoro zilizojitokeza katika awamu iliyomalizika.
Alifafanua kuwa kwa kipindi cha mwezi mmoja uliopita baada ya kusitishwa kwa operesheni hiyo, tembo 60 waliuawa na majangili hao kitendo ambacho hakitakiwi kuvumiliwa.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments: