LATEST POSTS

Wednesday, January 15, 2014

Wanasiasa marufuku kuongoza ushirika

MKOA wa Tabora umepiga marufuku viongozi wa kisiasa kuongoza vyama vya ushirika vya wakulima kwa madai ya kutanguliza maslahi yao badala ya kuwatetea wakulima.
Hayo yalibainishwa na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) katika kikao kilichofanyika mjini hapa juzi, ambapo wajumbe hao walisema wanasiasa wengi hawatetei maslahi ya wakulima ndiyo maana matatizo yanayowakabili wakulima hayaishi.

Mjumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Sikonge, Said Nkumba (CCM), alisema baadhi ya viongozi wa kisiasa wanaingiza siasa katika masuala yanayogusa maslahi ya wakulima jambo linaloathiri maendeleo ya vyama hivyo.

Alisema umaskini wa wakulima wa tumbaku hasa mkoani Tabora kwa kiasi kikubwa umechangiwa na kuingiza siasa katika masuala ya kilimo, huku akitolea mfano wa mauzo kufanywa kwa dola ya Marekani, mikataba ya ujanja ujanja ya mikopo iliyojaa ulaghai.

“Naomba viongozi wote wa kisiasa ambao wapo kwenye uongozi wa vyama vya wakulima ambao ni wenyeviti na watendaji wa vijiji au kata, madiwani, wabunge na wengineo waachie ngazi,” alisema na kuongeza kwamba Bunge limepitisha sheria mpya ya ushirika itakayoongoza masuala yote ya vyama hivyo.

Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Fatma Mwassa, aliutaka uongozi wa vyama vya ushirika kuboresha mfumo wa usambazaji pembejeo ili kumrahisishia mkulima upatikanaji wake.

0 comments: