LATEST POSTS

Sunday, April 13, 2014

Wanawake wa kitanzania wanavyohadaiwa ughaibuni

Leo tuangalie habari tatu zinazokabana kabali na maisha yetu magumu Waafrika. Ingawa ni za kuchoma moyo zitatupa azma ya kujaribu kujua nini hasa chanzo cha adha zetu na kutafuta ufumbuzi.
Mosi ni kisa cha kina dada wa Kitanzania wanaoendelea kukumbwa na hali za hatari sana baada ya kuahidiwa maisha bora kule China. Kwamba wangepewa kazi za kulipwa mishahara minono wayaboreshe maisha yao Bongo lakini wameishia gizani.
Giza totoro kiasi ambacho inadaiwa mmoja wao, Habiba Yusuf Ali Abdallah, aliuawa karibuni. Habiba alibakwa, akapigwa, figo yake ikanyofolewa kisha akarushwa mithili ya inzi toka ghorofani.
Ukweli wa madai haya umethibitishwa na dada mmoja aliyeshuhudia maiti na kero ikamzonga kiasi cha kujitolea kuzungumzia hatima ya wanawake vijana wanaokutwa na majanga nchini China.
Kwa woga wala jina hakuthubutu kulitaja. Kazungumzia kupitia blogu ya Mtanzania,Jestina George hapa London wiki mbili zilizopita.
Kisa nini?
Maisha magumu. Elimu duni. Ukosefu wa ajira...
Wanawake vijana wanaahidiwa ajira katika saluni, maana wanaifahamu sanaa ya nywele au kazi za dukani. Hughilibiwa na wanawake wenzao wa makamo waliokwishaishi China sasa wamepanga njama na midume toka Nigeria. Wanigeria ni kama washawajulia dada zetu. Wakiwaona ni kipepeo kuliona ua lenye asali. Na wanawake wa Kitanzania (hasa ughaibuni) wakionjeshwa maneno mazuri na vipesa vya uongo na kweli, hulegea na kulaghaika. Nauli za ndege chee, wanapofika China wanakuta ibilisi.
Pasi zinachukuliwa kusudi wasitoroke. Vitisho. Iliyobaki kulazimishwa kufanya ukahaba. Wanaokataa, madai yanaendelea, huletewa hawa washashi wa Kinigeria (waliokubuhu ukuwadi na maisha ughaibuni) huwabaka, huwapiga na baadhi kama Habiba kutolewa roho.
Labda tutadhani ni jambo geni maana hii ni mara ya kwanza kusikia limewakumba Watanzania. Mwaka jana mwanabloga wa Kenya anayeandika masuala ya safari kwa Kiingereza(“The African Traveller”)alieleza namna ambavyo wanawake wa Kenya, Uganda, Afrika Kusini, Ulaya na Bara Asia wanavyofanyiwa uanaharamu Bara Asia. Bloga Msafiri anatujuza kisa cha dada wa Kiganda aliyejirusha toka ghorofa ya nne mji wa Taman Kosas, Malaysia, akajiua.
Dada aliishi maisha ya kufungiwa, kupigwa na kulazimishwa kulala mkuku na wanaume. Anasema wanawake hawa hushurutishwa huo umalaya ili “kulipia” nauli ya dola 20,000.
Inapomalizika, siku za viza nazo zimekwisha, hawana njia, ila kubaki na pasipoti zimefichwa. Kazi ya ngono usiku mmoja ina rutuba ya dola 400 -mshahara wa mwezi saluni. Tamaa hii ya kipato cha haraka huishia puani.

“Wanawake wa Kiafrika huwa mateka wa biashara ya ngono. Kwa nini?” Anauliza Bloga Msafiri. “Nchi nyingi za Kiafrika ni maskini na wengi wanashindwa maisha na kuotea nyanda za majani mabichi ughaibuni....
Wanawake ndiyo walezi wa watoto na kutokana na mapenzi haya ya uzazi hufanya kila mbinu kutafuta namna. Kazi si nyingi na zile chache zinazopatikana zataka elimu...Kwa wasiosoma kwenda ughaibuni kufanya umalaya huonekana suluhisho.”
Suluhisho kweli?
Jestina George katika blogu yake anawaonya dada wenzake wanaoangukia jehanamu hii. Jestina anakumbusha hakuna mkataba wa kimaandishi. Ni hadaa inayopingwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji (IOM).
Jestina anashauri akheri uishi tu nyumbani na umaskini kuliko kuteseka ugenini. “Wito wangu ni kwa wale ambao mna ndugu huko na hamuelewi wanafanya nini, tafadhali fuatilieni ili muwasaidie.”
Chanzo: Mwananchi

0 comments: