LATEST POSTS

Tuesday, January 28, 2014

Urais wazidi kuigawa CCM

UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), umemrushia kombora aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, kuwa hana sifa za kuwa rais wa Tanzania, hivyo aache kukigawa chama hicho.
Kauli hiyo ya UVCCM imetolewa jijini Dar es Salaam jana na Katibu wa Uhamasishaji na Chipukizi, Paul Makonda, wakati alipozungumza na waandishi wa habari kuhusiana na kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na makada wa chama hicho kuhusiana na sakata la mawaziri mizigo.
Alidai kwa sasa umoja huo hauna muda wa kupoteza wa 'kupambana' na watu wanaotoa kauli za kubeza na kumkatisha tamaa Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Mnauye, kuhusiana na kazi walizofanya za kukijenga chama.
"Tunafahamu kuwa Guninita (John) na Mgeja (Khamis) hawana uwezo wa kumsema Kinana wala Nape, kilichopo nyuma yao na kinachowapa nguvu ya kufanya hivyo ni mtu anayewatuma na kuwafanya wao kumsaidia kutafuta madaraka...naye si mwingine ni Edward Ngoyayi Lowassa," alisema Makonda na kuongeza kuwa;
"Kama Mwalimu Nyerere (Baba wa Taifa Marehemu Julius Nyerere) angekuwepo, Lowassa asingepata nafasi ya kuyumbisha chama kiasi hicho...tunamweleza kuwa UVCCM haiko tayari kumuona anakibomoa chama kwa kupenda madaraka."
Aliongeza kwamba aendelee kuwasaidia viongozi wa dini na vijana wenye shida ya fedha, lakini sifa ya kuwa rais na amiri jeshi mkuu wa majeshi ya ulinzi na usalama hana. "Chama hakiwezi kukosea njia na kumpa urais mtu ambaye hana sifa," alisema Makonda.
Alisisitiza kuwa Chama ni sikio la wananchi na kiungo cha kuwaunganisha Serikali na wananchi wake, hivyo viongozi wa CCM wamefanya ziara na kubaini kero za wananchi.
"Inapofika hatua wasimamizi wa kanuni za chama wanapigwa vita kwa uamuzi wao wa kukisimamia chama UVCCM haiwezi kukaa kimya kwani wanaofanya hivyo hawakitakii mema chama chetu," alisema.
Alisema wanashangazwa na wanaomtuhumu Kinana na Nape kwa lengo la kuwachonganisha na Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, ili jamii ione kuna tofauti ndani ya sekretarieti, kwani lengo la kufanya hivyo ni kuwavunja moyo watendaji hao katika juhudi ambazo zinafanywa kwa kutupa mawe hata kwenye vyombo vya habari.
"Juhudi za kukiimarisha chama kutoka ngazi za chini kwa mabalozi ni mkakati bora kwani kukirudisha chama kwa wanachama ni kutimiza lengo la kuundwa kwa chama hicho cha wanyonge na maskini wa Taifa hili na haiwezekani matajiri watake kukihodhi na waratibu mikakati ya kukihujumu kwa pesa zao hali sisi vijana tukiwatazama tunasema tutakilinda chama chetu na kuwalinda viongozi wetu waadilifu."
 Aliwataka wanachama kuelewa kuwa viongozi hao wanaobezwa ndio wameweza kurudisha imani na matumaini ya wananchi kwa chama ambayo tayari ilishaanza kupotea na kuonekana si chama cha wanyonge, wakulima na wafanyakazi.
"Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliozunguka kwenda kukutana na wakulima wa pamba kule mikoa ya Kanda ya Ziwa kumpeleka Balozi wa China na kumshawishi kujenga viwanda ili kuboresha manufaa kwa wakulima".
Aidha alifafanua kuwa viongozi hao hao ndio wamepelekea kukutana na wakulima wa korosho na kushirikiana nao pamoja na bodi kutatua matatizo yanayowakabili na kuibua kero nyingine ikiwemo za wafugaji, walimu na wananchi kwa ujumla.
Alisema umoja huo tayari umewasilisha barua yake kwa Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho Bara, Philip Mangula kumtaka kuchukua hatua kwani mtu anayebeza ziara hizo na kuwaita viongozi waliozifanya waropokaji na wahuni ni mtu mjinga wa ovyo, hana maadili, asiyekipenda chama, mhaini na mzandiki anayepaswa kuchukuliwa hatua kali za kinidhamu ili iwe fundisho kwa wengine.
Mgeja ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, alipoulizwa kuhusiana na madai ya Makonda, alijibu kuwa hajapata taarifa hiyo. "Tunasubiri taarifa hiyo ili tujue tunavuruga chama kwa namna gani na sijui kama Lowassa anatumia fedha, anatumia fedha ili iweje?" Alihoji Mgeja.
Lakini baadaye Mgeja , aliwasiliana na gazeti hili na kusema kuwa yeye ni mtu mzima, hatishiwi nyau. Alisema Makonda anatafuta umaarufu kupitia migongo ya wakubwa.
"Kamwe mimi si saizi yake kwani ninaelewa kijana huyo anatumika kuwafurahisha wakubwa zake waliomtuma," alisema na kuongeza; "Hakuna asiyejua kuwa kijana huyo ana hasira za kuangushwa nafasi ya umakamu Mwenyekiti wa UVCCM na sasa anataka kulipa fadhila kwa waliotafuta njia kumpa nafasi katika umoja huo, hivyo ajiandae kula sahani moja na wazee wa chama hicho.
Mgeja alisema hatumwi na hatumiki kwa Lowassa, bali kijana huyo na wanaomtuma wanahangaika na kivuli cha Lowassa.
“Niliwaeleza na nawasisitiza tusichaguliane marafiki na wala wasichanganyikiwe, naelewa wana kiwewe kila siku Lowassa, Lowassa... kiwewe cha nini kwanza huyo Makonda bado mchanga sana kujibishana naye ni kuvunja heshima zetu ila kwakuwa damu inamchemka anatamani kula sahani moja na wakubwa sawa,” alisema.
Alisisitiza kuwa hakuna dhambi kumuunga mkono Lowassa na kama ni dhambi yeye yupo tayari kuhukumiwa kwa kuwa anakubaliana na utendaji wake hasa katika kumtakia heri kwa kazi anazozifanya katika kuwatumikia wananchi.
Alimtaka Makonda kufanya kazi za kujenga chama na umoja huo kwa kuzungumzia changamoto zilizopo ikiwemo tatizo la ajira na umaskini.

 

0 comments: