LATEST POSTS

Wednesday, February 19, 2014

bunge la katiba: Yametimia

MCHAKATO wa Bunge Maalumu la Katiba, umeanza mjini Dodoma jana ambapo wajumbe wa Bunge hilo, walimchagua Mwenyekiti wa muda ambaye atasimamia kazi ya kuandaa na kupitishwa kwa kanuni za Bunge hilo.
Katibu wa Bunge, Dkt. Thomas Kashililah, alimteua mjumbe wa Bunge hilo, Bi. Olivia Lwena kuwa Mwenyekiti wa muda aliyepewa jukumu la kusimamia upigaji kura.
Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Bw. Pandu Ameir Kificho, ndiye aliyeibuka mshindi katika uchaguzi wa kumpata Mwenyekiti wa muda akiwashinda wenzake wawili.
Awali, wagombea wa nafasi hiyo walikuwa watano ambao ni Bw. David Mbatia, Profesa Costa Mahalu, Bi. Magdalena Rubangira na Mbunge wa Jimbo la Donge, Sadifa Juma Khamis.
Bw. Mbatia aliondolewa katika kinyang'anyiro hicho baada ya kukosa sifa za kugombea kiti hicho ambapo Bw. Khamis, aliamua kujiondoa mwenyewe na kuwaachia wengine.
Katika uchaguzi huo, Bw. Kificho alipata kura 393, Prof. Mahalu (84), Bi. Rubangira 84.
Wajumbe wa Bunge hilo, walipiga kura mara mbili ambapo awali, wabunge walihesabiwa na idadi yao kuwa 549 lakini baada ya kupigwa kura, iliongezeka na kufikia 569.
Changamoto iliyojitokeza jana ukumbini humo ni baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo kuwasha vipaza sauti bila utaratibu baada ya kura za awali kuharibika wengine wakitaka upigaji kura usirudiwe bali zilizoongezeka ziondolewe.
Kutokana na mabishano ya muda mrefu, Mbunge wa Hai, mkoani Kilimanjaro, Bw. Freeman Mbowe alisimama na kusema kuwa, Bunge hilo linatengeneza historia, hivyo ni vyema upigaji kura ukarudiwa.
Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi wa nafasi hiyo, Bw. Kificho aliwashukuru wajumbe wote kwa kumpa kura nyingi na kuwapongeza wagombea wenzake ambao wote waliridhia ushindi wake bila pingamizi.
Alisema kifungu cha 22 A kifungu kidogo cha kwanza cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, pamoja na mambo mengine jukumu alilonalo mbali ya kusimamia kazi ya kuandaa na kupitishwa kanuni, pia atasimamia uchaguzi wa Mwenyekiti wa kudumu na makamu wake .
Aliongeza kuwa, leo kutakuwa na kikao cha kazi cha kawaida ambapo wajumbe wa Bunge hilo watapewa rasimu ya kanuni za Bunge waweze kuisoma na kuifahamu zaidi ambapo kikao rasmi cha Bunge hilo kitafanyika Jumatatu Februari 24 mwaka huu, saa 3 asubuhi.

0 comments: