LATEST POSTS

Friday, January 17, 2014

Madiwani, Mkurugenzi Arusha wavutana

KIKAO cha Baraza la Madiwani cha Jiji la Arusha kimeshindwa kufanyika baada ya madiwani kupitisha hoja ya kukaa kama kamati wakitaka kujadili nidhamu ya Mkurugenzi wa jiji hilo, Sipora Liana, ambaye naye aliamua kutoka pamoja na wataalamu wake akipinga kujadiliwa.
Aidha, baada ya kutoka nje ya kikao, inadaiwa mkurugenzi huyo alimwandikia “kimemo” Naibu Meya, Prosper Msofe (CHADEMA) aliyekuwa akiongoza kikao hicho akimweleza hawana uwezo kisheria wa kumjadili huku akigoma kurudi ili kuwezesha kikao hicho kuendelea.
Hayo yalitokea juzi kwenye kikao cha kawaida cha mwanzo wa mwaka cha kupokea taarifa ya robo ya kwanza ya mwaka ambacho  kilikuwa hakijaanza kujadili ajenda sita walizokuwa wamejipangia, pia Mkuu wa wilaya, John Mongela, alihudhuria.
Hoja ya kujadili nidhamu ya mkurugenzi huyo iliibuliwa na Diwani wa Sekei, Cripin Tarimo, (CHADEMA) ambayo iliungwa mkono na madiwani watano na kupingwa na diwani mmoja huku madiwani wengine wakiwa hawaungi wala kupinga hoja hiyo.
Diwani wa Viti Maalumu, Belinda Kabuje (CCM),  alisimama akitaka kupatiwa taarifa ya fedha ya Oktoba, Novemba na Desemba mwaka jana huku akipinga kitendo cha mkurugenzi huyo kutoka nje badala ya kukaa atoe majibu ya hoja za madiwani.
Madiwani waliwaomba waandishi wa habari kuwapisha ili wajadili suala hilo faragha ambapo walikaa kwenye ukumbi huo kuanzia saa 5 asubuhi mpaka saa 8 mchana.
Meya, Gaudence Lyimo ambaye aliingia kwenye ukumbi huo mkurugenzi akiwa tayari ameshatoka alisema kuwa wamekubaliana kuandika barua ya malalamiko kuipeleka kwenye mamlaka ya nidhamu ya mkurugenzi huyo pamoja na kwa Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) na Mkuu wa Mkoa.
Alisema hiyo itawezesha Mkuu wa Mkoa (RC) kutumia mamlaka yake kisheria kuitisha baraza la madiwani mapema kwani kwa sasa hakuna njia nyingine.
Tanzania Daima ilipomfuata mkurugenzi huyo ofisini kwake alijibu kupitia mmoja wa watumishi wa ofisi hiyo kuwa asubiriwe kwa muda kabla hajabadili msimamo kupitia mtumishi mwingine akisema hahitaji kuonana na mtu yeyote kwa muda huo. Hata hivyo  majina ya waleta majibu hayo hayakuweza kupatikana.
Sakata hili limeibuka kukiwa na mvutano mkubwa kati ya mkurugenzi huyo kwa upande mmoja na Meya, Lyimo, Mkuu wa Mkoa, Magesa Mulongo na Mkuu wa Wilaya, Mongela kwa upande mwingine, hali iliyolazimu Ofisi ya Waziri Mkuu kuingilia kati.

Chanzo: Tanzania Daima.

0 comments: