LATEST POSTS

Monday, January 27, 2014

Sakata mawaziri mizigo: CCM imdhibiti Nape-Guninita

MWANACHAMA mkongwe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye amewahi kuwa Mwenyekiti wa chama hicho mkoani Dar es Salaam, Bw. John Guninita, ameitaka CCM kupitia Idara ya Maadili, kumdhibiti Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Bw. Nape Nnauye.
Bw. Guninita aliyasema hayo Dar es Salaam jana katika taarifa yake kwa vyombo vya habari na kusisitiza kuwa, Bw. Nnauye ni kiongozi asiyefaa katika nafasi aliyonayo na kutaka aondolewe katika chama kwani amekuwa akifanya kazi za chama bila kujali mipaka yake.
Alisema hakuna kikao cha CCM kilichokaa na kutoa tamko la kuwepo 'Mawaziri Mizigo' wanaostahili kuchukuliwa hatua.
"Wamekwenda kwenye mikutano ya hadhara na kutaja majina ya Mawaziri wanaodai kuwa ni mizigo, mimi kama mwanachama mstaafu wa CCM, naamini waliotangazwa kwenye mikutano hiyo hawakuwatendea haki," alisema Bw. Guninita.
Aliongeza kuwa, Bw. Nnauye ni kiongozi anayeogopa demokrasia ya kuchaguliwa ndiyo maana hata nafasi aliyonayo hakugombea ameipata 'kimjomba mjomba'.
Majibu ya Nape
Akijibu tuhuma hizo, Bw. Nnauye alisema kitendo cha Bw. Guninita kudai amepewa nafasi hiyo 'kimjomba mjomba' ni kuwatukana wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), kutoka Wilaya zote nchini ambao walipitisha jina lake.
Bw. Nnauye alikwenda mbali zaidi na kudai kuwa, mbali ya Bw. Guninita kuwatukana wajumbe wa NEC pia amemtukana Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete ambaye ndiye aliyependekeza jina lake na kulipeleka kwenye kikao cha NEC ili liweze kupitishwa na wajumbe.
Alitolea mfano wa Waziri Mkuu, anapoteuliwa na Rais jina lake hupelekwa bungeni ili liweze kupitishwa na wabunge hivyo uteuzi wa nafasi yake nao ulizingatia vigezo hivyo na kumshangaa Bw. Guninita kwa kutojua mifumo ya utendaji kazi ndani ya chama hicho.
"Anasema nimepewa cheo kiujomba ujomba... Rais ni Mkwere na mimi ni Mmakonde huo ujomba unatoka wapi, hayo ni matusi makubwa kwa wajumbe wa NEC na Rais, namshangaa huyu mzee ambaye anajiita mstaafu wakati alifukuzwa na wanachama.
"Watanzania wanaijua vizuri historia ya Guninita kwani ndiye aliyehusika kuyauza majimbo ya Ubungo na Kawe kwa wapinzani katika Uchaguzi Mkuu uliopita," alisema Bw. Nnauye.
Alisema Bw. Guninita alikurupuka kusoma taarifa yake kwa vyombo vya habari kwani hakuna kipengele kilichoonesha amepinga uteuzi wa Rais katika Baraza la Mawaziri.
"Guninita hana kazi ya kufanya, alinyimwa kura na wana CCM ambao walimfukuza hivyo Watanzania wampuuze na kumsamehe kwa kauli zake," alisema.
Akizungumzia rai iliyotolewa na makundi mbalimbali ya kijamii na vyama vya siasa kumtaka Bw. Nnauye na Katibu Mkuu wa CCM,
Bw. Abdulrahman Kinana wajiuzulu nafasi zao baada ya Rais Kikwete kuwarudisha baadhi ya Mawaziri waliolalamikiwa, alisema "Sisi ni watu wazima, tumesikia maoni yao".
Pia Bw. Nnauye alitolea ufafanuzi kauli ya Mwenyekiti wa CUF Taifa, Profesa Ibrahim Lipumba, kuwa Mawaziri Mizigo wanatokana na chama mzigo, alisema kiongozi huyo ameanza kuzeeka vibaya.
"Huwezi kusema chama mzigo wakati watendaji ndiyo mizigo, Lipumba anastahili kupewa cheti cha mgombea bora wa urais anayeshindwa kila uchaguzi," alisema.
Aliongeza kuwa , C C M inamuandalia cheti cha kumpongeza Prof. Lipumba kwa kuwa mgombea bora anayeshindwa tangu mwaka 1995 hadi sasa hivyo Watanzania wamsamehe, waendelee kuiamini CCM kwani ndicho chama chenye uwezo wa kuwapigania na kushughulikia kero zao.

0 comments: